Thursday, June 28, 2018

Tume ya Madini yapokea ripoti ukaguzi migodi ya madini ya vito, Kinywe


Na Samwel Mtuwa, Dodoma

Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini Prof. Shukran Manya leo tarehe 28 Juni, 2018, amepokea ripoti ya Ukaguzi Maalum wa Migodi ya Madini ya Vito na Madini ya Kinywe (Graphite) kutoka kwa Mwenyekiti wa Timu ya Ukaguzi Profesa Justinian Ikingura.

Ripoti hiyo imetokana na Tume Maalum ya Wataalam Sita iliyoundwa na Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini Prof. Manya tarehe 17 Juni, 2018 ikilenga kufanya ukaguzi maalum katika maeneo ya uchimbaji wa madini ya Vito na Kinywe katika wilaya ya Ulanga Mkoani Morogoro.

Aidha, ukaguzi huo ulilenga kutekeleza maelekezo ya Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko aliyoyatoa hivi karibuni wakati wa ziara yake mkoani Morogoro.

Katika ziara ya Naibu Waziri Biteko mkoani humo, alipokea malalamiko kutoka kwa wachimbaji wadogo wa madini ya vito ambao ni wanakijiji wa kijiji cha Epanko kilichopo katika eneo la mradi wa madini hayo.

 Aidha, kufuatia malalamiko hayo Naibu Waziri aliahidi kuunda timu ya watalaam wa madini itakayofanya kazi ya ukaguzi maalum kwa lengo la kutathmin uendeshwaji wa migodi ya madini ya vito na kinywe pamoja na biashara ya madini kulingana na Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 pamoja na marekebisho yake.

Katika ripoti hiyo, timu ya wataalam wa madini imetoa mapendekezo mbalimbali ikiwemo Serikali kupitia Wizara ya Madini na Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) kuweka mkakati wa kufanya Utafiti na tathmin ya madini adimu ya vito katika eneo la Mahenge na maeneo mengine nchini ili kuwepo na takwimu sahihi za kuvutia wawekezaji katika uchimbaji wa madini hayo.

Pendekezo jingine ni Mamlaka husika kuweka mpango wa kutoa huduma ya uthaminishaji wa madini ya vito katika maeneo ya wachimbaji wadogo ili kuwezesha wachimbaji hao kupata bei stahiki ya madini wanayozalisha na hivyo kuongeza kipato chao na kulipa tozo stahiki kwa Serikali.

Wajumbe wa timu hiyo walitoka katika Taasisi ya Jiolojia ya Utafiti wa Madini Tanzania (GST), Chuo cha Madini Dodoma, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi Ukaguzi wa Migodi na Afisa Madini Mkazi wa Dodoma.


Mwenyekiti wa Timu Maalumu ya Ukaguzi wa Migodi ya Vito na Madini ya Kinywe (Graphite) Profesa Justinian Ikingura akikabidhi Ripoti ya Ukaguzi huo kwa Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini Profesa Shukrani Manya, makabidhiano haya yamefanyika tarehe 28/6/2018 katika ukumbi wa mikutano wa GST. Wengine wanaoshuhudia tukio hilo ni Mwenyekiti wa Tume ya Madini Profesa Idris Kikula na Profesa Abdukarim Mruma pamoja na watalam wa timu hiyo. 

Mwenyekiti wa Timu Maalumu ya Ukaguzi wa Migodi ya Vito na Madini ya Kinywe (Graphite) Profesa Justinian Ikingura akikabidhi Ripoti ya Ukaguzi huo kwa Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini Profesa Shukrani Manya, makabidhiano haya yamefanyika tarehe 28/6/2018 katika ukumbi wa mikutano wa GST. Wengine wanaoshuhudia tukio hilo ni Mwenyekiti wa Tume ya Madini Profesa Idris Kikula na Profesa Abdukarim Mruma pamoja na watalam wa timu hiyo.
Mwenyekiti wa Timu ya Ukaguzi wa Migodi ya madini ya Vito na Kinywe Profesa Justinian Ikingura aliyekaa (katikati) akimsikiliza Mwenyekiti wa Tume ya Madini Profesa Idris Kikula mara baada ya kumaliza uwasilishaji wa mada nzima ya Ripoti ya Ukaguzi kwa Tume ya Madini.

Thursday, June 21, 2018

Naibu Waziri Nyongo awaongoza Wabunge wa Afrika Kusini kujifunza usimamiaji wachimbaji wadogo


Na Mwandishi wetu, Dodoma

Ziara ya Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini, ambao wapo nchini kujifunza na kupata uzoefu namna Tanzania inavyoendesha sekta ya madini, imeendelea kwa wabunge hao kuwatembelea wachimbaji wadogo wa dhahabu waliopo eneo la Nori, wilayani Bahi.

Wakiongozwa na Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo, Wabunge hao walifanya ziara hiyo Juni 20, 2018, ambapo walipata fursa ya kujionea shughuli za uchimbaji wa dhahabu unaofanywa na wachimbaji wadogo katika eneo hilo na kuzungumza nao kuhusu uzoefu wao katika kazi husika.

Akizungumza kwa niaba ya wenzake, Kiongozi wa Ujumbe huo, S. Khanyile alikiri kuwa, ziara husika imewawezesha kujifunza mambo mengi na kwamba watatumia uzoefu walioupata kuboresha na kuimarisha zaidi sekta ya madini nchini kwao.

Kwa upande wake, Naibu Waziri Nyongo aliwahakikishia Wabunge hao kuwa Tanzania itaendeleza ushirikiano kati yake na nchi ya Afrika Kusini, hususan katika sekta ya madini.

Alisema, ushirikiano wa nchi hizo mbili katika sekta ya madini, utasaidia kuimarisha na kuboresha zaidi sekta husika na hivyo kuziwezesha kuwa za mfano katika uchangiaji wa Pato la Taifa na kuimarisha uchumi wa nchi na wananchi wake kwa ujumla.

Juni 19, mwaka huu, Wabunge hao walifika Makao Makuu ya Wizara ya Madini jijini Dodoma, ambapo walipokelewa na Waziri mwenye dhamana, Angellah Kairuki. Katika siku hiyo ya kwanza ya ziara yao, walipata fursa ya kujifunza kuhusu sekta husika kupitia uwasilishwaji wa Mada mbalimbali uliofanywa na Kamishna wa Madini, Mhandisi David Mulabwa.

Pichani ni matukio mbalimbali wakati wa ziara hiyo.









Wednesday, June 20, 2018

Wabunge wa Afrika Kusini wajifunza uzoefu sekta ya madini Tanzania


Veronica Simba na Samwel Mtuwa, Dodoma

Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini, wametembelea Wizara ya Madini kwa lengo la kujifunza na kupata uzoefu namna sekta husika inavyoendeshwa nchini.

Wawakilishi hao wa wananchi wa Afrika Kusini, walipokelewa na Waziri wa Madini Angellah Kairuki, Naibu Mawaziri Doto Biteko na Stanslaus Nyongo pamoja na Katibu Mkuu Prof Simon Msanjila, jana Juni 19, 2018, Makao Makuu ya Wizara Dodoma.

Akizungumzia nia ya ujio wao, Kiongozi wa Ujumbe huo ambaye ndiye pia Mwenyekiti wa Kamati husika, S. Khanyile alisema kuwa, walipenda kupata uzoefu wa Tanzania katika kusimamia uchimbaji mdogo wa madini pamoja na mbinu za udhibiti wa uchimbaji haramu wa madini.

Akiwasilisha Mada kwa Ujumbe huo kuhusu maeneo husika; Kamishna wa Madini Tanzania, Mhandisi David Mulabwa, alieleza kuwa, katika kusimamia uchimbaji mdogo, Serikali kupitia Wizara ya Madini inatekeleza mambo kadhaa muhimu ambayo ni pamoja na kuhakikisha wachimbaji wote wanarasimishwa kwa kupatiwa leseni.

Kamishna Mulabwa alieleza kuwa, pamoja na kuwarasimisha wachimbaji, Serikali pia inatoa mafunzo mbalimbali kwao kwa lengo la kuwajengea uelewa, inatenga maeneo ya uchimbaji kwa ajili yao pamoja na kujenga vituo vya mfano kama vile Mgodi wa Mfano wa Lwamgasa ambao pia utakuwa na Mtambo wa Uchenjuaji madini.

“Vilevile, tunasimamia pia suala la makusanyo ya kodi na tozo mbalimbali stahiki kutoka kwa sekta hii ya uchimbaji mdogo. Ili suala hili liwe na mafanikio, ni lazima kuhakikisha wachimbaji wanawezeshwa ipasavyo kupitia mafunzo na mambo mbalimbali kama nilivyoeleza awali,” alifafanua.

Aidha, aliongeza kuwa, Serikali imekuwa ikiwawezesha wachimbaji wadogo kwa kuwapatia ruzuku lakini akabainisha kuwa utaratibu huo umesitishwa kwa muda baada ya kujitokeza changamoto kadhaa, na utarejeshwa tena baada ya kuaandaa utaratibu mzuri zaidi na wenye tija katika kuendesha zoezi hilo.

Kuhusu suala la udhibiti wa uchimbaji haramu wa madini, Mhandisi Mulabwa alieleza kuwa, Tanzania imeweka mfumo mzuri wa kisheria ambao unamtaka yeyote anayejishughulisha na uchimbaji madini kuwa na leseni halali.

Alisema kuwa, Serikali pia imeweka utaratibu wa kusimamia kwa karibu shughuli zote za uchimbaji ikiwemo kufanya ukaguzi wa mara kwa mara.

 Vilevile, alisema kuwa kuimarisha mawasiliano kuanzia ngazi ya chini yaani Serikali ya Kijiji, Wilaya na hatimaye Ofisi za Madini ni muhimu sana katika udhibiti wa uchimbaji haramu.

“Kupitia mawasiliano hayo tunafanikiwa kupata taarifa zote mara moja na hivyo inatusaidia kuchukua hatua stahiki na kwa wakati stahiki.”
Kwa upande wake, Waziri Kairuki aliwashukuru wabunge hao kwa kufanya uamuzi wa kuja kujifunza Tanzania na kuomba ushirikiano baina yao uendelezwe. Wabunge hao pia walishukuru kwa ushirikiano waliopata na kusema kuwa wamefurahi kupata uzoefu wa Tanzania ambao utawasaidia katika uboreshaji wa sekta hiyo nchini kwao.


Waziri wa Madini, Angellah Kairuki (mwenye nguo ya kitenge) akiwapokea Wajumbe wa Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini, waliofika Makao Makuu ya Wizara – Dodoma, Juni 19, 2018 kujifunza na kupata uzoefu namna sekta husika inavyoendeshwa nchini. Kushoto ni Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko.


Kamishna wa Madini, Mhandisi David Mulabwa, akiwasilisha Mada kwa Wajumbe wa Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini, waliofika Makao Makuu ya Wizara – Dodoma, Juni 19, 2018 kujifunza na kupata uzoefu namna sekta husika inavyoendeshwa nchini.

Wajumbe wa Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini, waliofika Makao Makuu ya Wizara – Dodoma, Juni 19, 2018 kujifunza na kupata uzoefu namna sekta husika inavyoendeshwa nchini; wakifuatilia Mada zilizokuwa zikiwasilishwa na Kamishna wa Madini Tanzania, Mhandisi David Mulabwa (hayupo pichani).
Waziri wa Madini, Angellah Kairuki, akifafanua jambo, wakati wa kikao na Wajumbe wa Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini (hawapo pichani), waliofika Makao Makuu ya Wizara – Dodoma, Juni 19, 2018 kujifunza na kupata uzoefu namna sekta husika inavyoendeshwa nchini.
Kutoka Kulia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini, S. Khanyile, Waziri wa Madini Angellah Kairuki, Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo na Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko, wakifurahia jambo, wakati Kamati hiyo ilipotembelea Makao Makuu ya Wizara – Dodoma, Juni 19, 2018 kujifunza na kupata uzoefu namna sekta husika inavyoendeshwa nchini.

Waziri wa Madini, Angellah Kairuki (katikati) akiwapokea Wajumbe wa Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini, waliofika Makao Makuu ya Wizara – Dodoma, Juni 19, 2018 kujifunza na kupata uzoefu namna sekta husika inavyoendeshwa nchini.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila (kulia) na Makatibu wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, wakifuatilia Mada zilizokuwa zikiwasilishwa na Kamishna wa Madini Tanzania, Mhandisi David Mulabwa (hayupo pichani), wakati Wajumbe wa Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini, walipofika Makao Makuu ya Wizara – Dodoma, Juni 19, 2018 kujifunza na kupata uzoefu namna sekta husika inavyoendeshwa nchini.
Waziri wa Madini Angellah Kairuki (mwenye nguo ya kitenge), Naibu Mawaziri wa Madini Stanslaus Nyongo (kushoto kwa Waziri) na Doto Biteko (kulia kwa Waziri), wakibadilishana mawazo na Wajumbe wa Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini, waliofika Makao Makuu ya Wizara – Dodoma, Juni 19, 2018 kujifunza na kupata uzoefu namna sekta husika inavyoendeshwa nchini.

Tuesday, June 19, 2018

Tanzania yashiriki Mkutano wa Kimberley Process


Na Asteria Muhozya

Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini  Prof. Shukrani Manya na Afisa kutoka Wizara ya Madini Mhandisi Siri  Boga wanaiwakilisha Tanzania katika Mkutano wa Kimberley Process unaofanyika mjini Antwerp, nchini Ubeligiji, 

Mkutano huo huhudhuriwa na wanachama wa Umoja wa Kimberley Process ambao unahusisha  mataifa ya Kiraia, Serikali na kampuni zinazojishughulisha na  uzalishaji na watumiaji wa madini ya almasi.

Mkutano huo umefanyika kuanzia tarehe 18-22 Juni 2018.



Monday, June 18, 2018

Naibu Waziri wa madini Mhe. Biteko kuunda Tume maalumu kuchunguza migodi iliyopo Wilayani Ulanga

Na Fredy Mgunda, Morogoro

Naibu Waziri wa Madini Mhe Doto Mashaka Biteko amesema kuwa ataunda tume maalumu kwa ajili ya kuchunguza migodi yote nchini ikiwa ni pamoja na utambuzi wa aina ya madini yanayopatika katika migodi iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Ulanga Mkoani Morogoro kwa lengo la kuhakikisha kuwa Tanzania haiendelei kuibiwa na wawekezaji katika sekta ya madini.

Akizungumza wakati wa ziara ya siku mbili Mkoani Morogoro Mh Biteko alisema kuwa madini yote yaliyopo katika ardhi ya Tanzania ni mali ya watanzania hivyo yanapaswa kuwanufaisha watanzania kwanza ndipo watu wengine wafuate.

“Naombeni watanzania wote mjue kuwa madini haya ni mali ya watanzania wote hivyo tunapaswa kuyalinda na kutoa taarifa sahihi kwa serikali kama kuna mtu anaiibia serikali kwa namna moja au nyingine ili serikali iweze kuchukua hatua za kisheria dhidi yake, Na mimi nawaambieni watanzania tuache uoga tuseme ukweli kama Rais wetu Mhe Dkt John Pombe Magufuli anavyosisitiza utendaji wa uwazi na uwajibikaji katika serikali” Alikaririwa Mhe Biteko

Biteko amepiga marufuku wawekezaji kutumia fedha zao kuwanyanyasa wananchi waliopo kwenye maeneo ambayo kuna migodi kwa ajili ya kuwaibia watanzania ambao bado wana kipato cha chini katika maeneo yanapopatikana madini.

“Najua hawa wawekezaji wanapesa nyingi sana hivyo isiwe sababu ya kuwarubuni baadhi ya wananchi na kuwatesa wananchi wengi hususani waliopo kwenye maeneo ya madini na leo nataka niwaambie ukweli wawekezaji wote nchini najua ambavyo mnatumia pesa zenu kuwanyanyasa wananchi, sasa ndio mwisho wenu maana serikali ya awamu ya tano inataka haki kwa kila mwananchi” Alisisitiza Biteko

Naibu Waziri wa Madini Mhe Doto Mashaka Bitoke alifanya ziara ya kikazi katika kijiji cha Ipanko kilichopo katika wilaya ya Ulanga mkoani Morogoro na kugundua kuwa kuna wawekezaji wanaidanganya serikali na wananchi kwa kutoweka wazi kiasi gani ambacho wanakipata kwenye migodi iliyopo katika kijiji hicho.

“Jamani wana Ipanko nchi hii tumeibiwa sana sasa ifike mwisho tusema hapana haiwezekani tena kwenye serikali ya awamu ya tano chini ya Rais wetu Dkt John Pombe Magufuli tuendelee kuibiwa madini yetu na kuwanufaisha watanzania ambao wapo nje ya nchi yetu, Rais kashasema na sisi wasaidizi wake tunaungana naye kwamba iwe mwisho kuchezewa kwa rasilimali zetu”

“Chonde chonde nyie viongozi wetu wa ngazi za vijiji, kata, tarafa, wilaya na mkoa tunaomba msituangushe kwa kupokea rushwa kutoka kwa wawekezaji na kuisaliti nchi yako kuendelea kuibia kirahisi namna hii” alisema Biteko

Biteko alieleza kuwa serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dkt John Pombe Magufuli inawapenda sana kuwa na wawekezaji wengi wenye tija ambao sio wababaisha na ambao wamekuja nchi kuiba rasilimali za watanzania.

Aidha, Biteko alisema kuwa haiwekani muwekezaji akawekeza Bilioni 42 halafu akachangia madawati na mifuko ya saruji katika jamii kama ndio mchango wake, haiwezekani wanapaswa kuchangia kulingana na kiasi ambacho wamewekaza kwa faida na manufaa ya wananchi.

“Mimi binafsi hainiingi akilini kuona muwekezaji amewekeza pesa nyingi kama hizo halafu kwenye shughuli za kimendeleo amechangia kiasi kidogo namna hiyo kwangu nasema haiwezekani na nchi hii kwa sasa sio yakuchezewa tena” alisema Biteko

Lakini pia Naibu waziri huyo alimpongeza Mbunge wa Jimbo la Ulanga Mhe Goodluck Mlinga kwa kuwapigania wananchi wake kwa kuzifikisha kero mahali husika na kutafutiwa ufumbuzi.

Nao baadhi ya wananchi akiwemo Pangarasi Kanyali, Cyprian Kanyali, Micky Sengo, Doedatus Moholeli, Hilda Linoma na Fredrick Kazimoto  walimpongeza Naibu Waziri wa Madini Mhe Biteko kwa kufika kijiji hapo na kusiliza kero zao kwani wana amini zitatafutiwa ufumbuzi kwa kufuata sheria na katiba ya nchi.

“Toka sisi tuzaliwe hatujawahi kutembelewa na waziri na kusikiliza kero zetu kama ambavyo wewe umefika kijijini kwetu leo hii tunajisikia wenye amani na furaha kwa kuwa tunajua kero zetu tunazifikisha moja kwa moja kwa kwa Rais wetu kupitia wewe waziri” Walisema wananchi hao

Awali Mbunge wa Jimbo la Ulanga Goodluck Mlinga alisema kuwa lengo la waziri kufika katika kijiji hapo ni kujionea kero wanazokumbana nazo wananchi kupitia wawekezaji wa sekta ya madini na kuzitafutia ufumbuzi.

“Huku ni mbali sana Mheshimiwa Naibu Waziri lakini kuna madini mengi ambayo ndio utajiri wa nchi hii hivyo tunapaswa kuwa makini na hawa wawekezaji maana wamekuwa wakiibia sana serikali yetu” Alisema Mlinga.

Naibu Waziri wa Madini Mhe Doto Mashaka Biteko akizungumza na wananchi kijijini Ipanko Wilaya ya Ulanga wakati wa ziara ya kikazi ya siku mbili mkoani Morogoro ya kukagua shughuli za uwekezaji wa migodi.
Baadhi ya wananchi kijijini Ipanko wakimsikiliza kwa makini Naibu Waziri wa Madini Mhe Doto Mashaka Biteko alipokuwa katika ziara ya kikazi katika Wilaya ya Ulanga mkoani Morogoro kukagua shughuli za utendaji wa wawekezaji wa migodi .
Naibu Waziri wa Madini Mhe Doto Mashaka Biteko akizungumza na wananchi kijijini Ipanko Wilaya ya Ulanga wakati wa ziara ya kikazi ya siku mbili mkoani Morogoro ya kukagua shughuli za uwekezaji wa migodi.

Thursday, June 14, 2018

Tanzania na Australia kuendeleza ushirikiano sekta ya madini


Na Veronica Simba, Dodoma

Balozi wa Australia nchini Tanzania, Alison Chartres, amemtembelea Waziri wa Madini Angellah Kairuki na kuzungumzia ushirikiano wa nchi hizo katika sekta ya madini.

Akiongoza Ujumbe wa Umoja wa Kampuni za Madini na Nishati za Australia, Juni 13, 2018 Makao Makuu ya Wizara Dodoma; Balozi Chartres alimweleza Waziri Kairuki kuwa nchi yake inapenda kuendelea kushirikiana na Tanzania katika sekta mbalimbali, ikiwemo sekta ya madini.

Kwa upande wake, Waziri Kairuki; pamoja na kumhakikishia Balozi huyo kuwa Tanzania itaendelea kutoa ushirikiano kadri inavyotakiwa kwa Australia, lakini pia alitumia fursa hiyo kuwakaribisha wawekezaji mbalimbali wa nchi hiyo, waendelee kuja kuwekeza katika sekta ya madini nchini na katika sekta nyingine pia.

“Ni matumaini yetu kuwa, nchi zetu zitaendeleza ushirikiano katika sekta ya madini na sekta nyingine mbalimbali kama ambavyo tumekuwa tukifanya,” alisisitiza Waziri.

Aidha, Waziri Kairuki aliuelekeza Ujumbe huo kutoka Australia, kuwasilisha mapendekezo rasmi kwa Serikali ikiwa kuna eneo lolote katika sekta ya madini, wanalodhani linahitaji kufanyiwa marekebisho ili wataalam wayapitie na kuona endapo yana tija kwa pande zote mbili, na kisha kufikia maamuzi.

“Niweke wazi kuwa, Serikali ya Tanzania imedhamiria kuhakikisha kuwa sekta ya madini inawanufaisha wananchi wake ipasavyo. Kwa hiyo, kila tutakapobaini kuwa liko eneo ambalo halituridhishi, hatutasita kufanya marekebisho kwa manufaa ya Watanzania wote.”

Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo, Kamishna wa Madini Tanzania Mhandisi David Mulabwa pamoja na maafisa mbalimbali waandamizi kutoka Wizara ya Madini na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.


Waziri wa Madini Angellah Kairuki (katikati-waliokaa), Balozi wa Australia nchini Tanzania, Alison Chartres (kushoto-waliokaa) na Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo (kulia-waliokaa); wakiwa katika picha ya pamoja na Ujumbe wa Umoja wa Kampuni za Madini na Nishati za Australia na wataalam wa sekta ya madini Tanzania,  baada ya kikao baina ya pande hizo mbili kujadili ushirikiano katika sekta ya madini. Kikao kilifanyika Juni 13, 2018 Makao Makuu ya Wizara Dodoma.


Waziri wa Madini Angellah Kairuki (katikati), akizungumza na Balozi wa Australia nchini Tanzania, Alison Chartres (kushoto), wakati wa kikao kilichofanyika Juni 13, 2018 Makao Makuu ya Wizara Dodoma. Kikao hicho kilijadili ushirikiano wa Tanzania na Australia katika sekta ya madini. Kulia ni Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo. 


Waziri wa Madini Angellah Kairuki (katikati), akiongoza kikao baina ya wataalam wa sekta ya madini Tanzania (kulia) na Ujumbe wa Umoja wa Kampuni za Madini na Nishati za Australia, ulioongozwa na Balozi wake nchini, Alison Chartres (kushoto). Kikao hicho kilijadili ushirikiano wa Tanzania na Australia katika sekta ya madini na kilifanyika Juni 13, 2018 Makao Makuu ya Wizara jijini Dodoma.


Kutoka kushoto ni Kamishna wa Madini Tanzania, Mhandisi David Mulabwa, Afisa Sheria Mwandamizi Juliet Moshi na Mkaguzi wa Migodi kutoka Wizara ya Madini, Mhandisi Assa Mwakilembe, wakijadiliana jambo, muda mfupi baada ya kikao cha Waziri wa Madini Angellah Kairuki na Ujumbe wa Umoja wa Kampuni za Madini na Nishati za Australia, ulioongozwa na Balozi wake nchini, Alison Chartres (kushoto), Makao Makuu ya Wizara jijini Dodoma, Juni 13, 2018.

Wednesday, June 13, 2018

Waziri Mkuu Kasimu Majaliwa amezindua Maabara kubwa na ya kisasa Afrika na ya pili Duniani kwa upimaji wa madini


Na Zuena Msuya, Dar es Salaam

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kasim Majaliwa amezindua Maabara ya kisasa ya utambuzi wa uasili wa madini iliyojengwa katika Kituo cha Madini na Jiosayansi Afrika kilichopo eneo la Kunduchi Mtongani, jijini Dar es salaam.

Akizungumza mara baada ya kuzindua maabara hiyo, Juni 8, 2018, Waziri Mkuu Majaliwa alisema maabara hiyo itakuwa na uwezo wa kutambua asili ya madini yote yanayochimbwa NA kupatikana duniani.

Vile vile italinda madini ya kila nchi husika hasa kwa nchi za Afrika na kumaliza kabisa tatizo la utoroshwaji wa madini ya aina yoyote kutoka nchi moja kwenda nyingine.

“Maabara hiyo itakuwa na uwezo wa kutambua mahali ambapo madini hayo yamechimbwa au yanapatikana, na haitakuwa  rahisi kwa mtu yeyote kufanya udanganyifu wa kutorosha madini hayo kutoka sehemu moja kwenda nyingine kwani kila nchi yatakapokuwa yatakapopelekwa madini hayo vipimo vitaonyesha asili yanapotoka madini hayo”, alisema Waziri Mkuu Majaliwa.

Alifafanua zaidi kuwa Maabara hiyo pia inauwezo mkubwa wa kupima na kutambua asili ya madini Bati( Tin),Tantalam na Tantalite, yanapochimbwa na yanapotoka, jambo ambapo litaondoka tatizo la kubaini kuwa madini hayo lilipo sasa kwa nchi za afrika zinazochimba madini hayo ikiwemo Burundi, Rwanda, Uganda na Jamhuri ya Kidemograsia ya Congo.

Hivyo amezishauri nchi za Afrika kutumia maadara hiyo ambayo kwa sasa inapatikana Tanzania pekee kwa nchi za afrika na niya pili kujengwa duniani, ili nchi hizo ziweze kufahamu madini yake halisi yanayopatikana katika nchi husika.

“ kwa mfano hapa Tanzania tunawachimbaji wadogo wengi sana wanachimba madini lakini wengi wao wanashindwa kutambua ni madini gani wanachimba, pia tunapokamata madini mipakani wengi husema madini hayo yanatoka nchi jirani na hivyo tunakosa uthibitisho, sasa maabara hii ni muarobaini wa kutatua changamoto zote hizi, na ni imani yangu kubwa italeta manufaa makubwa katika sekta ya madini”, alisisitiza Waziri Mkuu Majaliwa.

Aliweka wazi kuwa kuwepo kwa maabara hiyo Afrika kutamaliza kabisa tatizo la uotoshwaji wa madini kutoka sehemu moja kwenda nyinge na kuondoa udanganyifu na unaofanywa na baadhi ya watu wasio waaminifu kwa kusema ukweli kuhusu mahali yanapopatikana madini husika.

Maabara hiyo inauwezo mkubwa wa kupima madini na kutumia muda mfupi katika kutambua uhalisia wa madini.

Sambamba na hilo, Waziri Mkuu, Majaliwa alisema maabara hiyo ya kisasa itarahisisha biashara ya madini kwa kila nchi husika na kuleta manufaa zaidi kwa taifa na wake.


Waziri Mkuu Kasim Majaliwa (kushoto) akilakiwa na Waziri wa Madini, Angellah Kairuki mara baada ya kuwasili katika Viwanja vya Kituo cha Madini na Jiosayansi Afrika kuzindua Maabara ya kwanza ya kisasa Afrika na ya pili duniani ya kutambua uasili wa madini.


Waziri Mkuu Kasim Majaliwa (kushoto) akisalimiana na Naibu wa Waziri wa Madini, Stansilaus Nyongo mara baada ya kuwasili katika Viwanja vya Kituo cha Madini na Jiosayansi Afrika alipowasili kuzindua Maabara ya kisasa Afrika na ya pili duniani ya kutambua uasili wa madini.


Waziri Mkuu Kasim Majaliwa( kushoto) akisalimiana na Naibu wa Waziri wa Madini, Dotto Biteko mara baada ya kuwasili katika Viwanja vya Kituo cha Madini na Jiosayansi Afrika alipowasili kuzindua Maabara ya kisasa Afrika na ya pili duniani ya kutambua uasili wa madini.


Waziri Mkuu Kasim Majaliwa( kushoto) akisalimiana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila,(kulia) mara baada ya kuwasili katika Viwanja vya Kituo cha Madini na Jiosayansi Afrika alipowasili kuzindua Maabara ya kwanza ya kisasa Afrika na ya pili duniani ya kutambua uasili wa madini.


Waziri Mkuu Kasim Majaliwa (kulia) akipata maelezo  ya namna maabara hiyo inavyofanya kazi kutoka kwa mmoja wa wakufunzi   katika Kituo cha Madini na Jiosayansi Afrika kuzindua Maabara ya kwanza ya kisasa Afrika na ya pili duniani ya kutambua uasili wa madini,

Waziri Mkuu Kasim Majaliwa (kushoto) akipeana mkono na Waziri wa Madini, Angellah Kairuki mara baada ya kufungua kitambaa kuzindua  Maabara ya kwanza ya kisasa Afrika na ya pili duniani ya kutambua uasili wa madini.

Friday, June 8, 2018

Kampuni ya Auxin ya China yaonesha nia kuwekeza kwenye kiwanda cha Baruti


Na Asteria Muhozya, Dar es Salaam

Waziri wa Madini Angellah Kairuki amekutana na Wawakilishi wa Kampuni ya Auxin ya China ambao wameonesha nia ya Kujenga Kiwanda cha Baruti nchini.

Ujumbe wa kampuni hiyo umemweleza Waziri Kairuki lengo la kukutana naye kuwa ni kutaka kujua taratibu mbalimbali ikiwemo za Kisheria ili kujua namna ambavyo kinaweza kujenga kiwanda hicho nchini.

Akizungumza katika kikao hicho Waziri Kairuki amewaeleza wawakilishi hao kuwa, endapo kampuni husika itapata fursa ya kuwekeza nchini suala la ajira kwa watanzania linatakiwa kuchukuliwa kwa umuhimu wake ili kuhakikisha kwamba watanzania wanapata ajira.

Pia, amewataka watendaji hao kusoma na kuelewa kipengele cha uwezeshaji wazawa na maeneo ambayo shughuli zao zitafanyika ili kuelewa namna ambavyo watahakikisha watanzania wananufaika na uwekezaji wao katika maeneo ambayo shughuli zao zitafanyika.

kikao hicho kimehudhuriwa  pia na  Kaimu  Kamishna  Msaidizi wa  Madini anayeshughulikia masuala ya Baruti, Chiku  Juma, Wataalam wa Wizara ya Madini na  Afisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Kampuni hiyo inafanya shughuli kama hizo katika nchi za Congo DRC, Uganda, Namibia na Guinea.


Waziri wa Madini Angellah Kairuki akisisitiza jambo wakati wa kikao na Kampuni ya Auxin ya China ambayo imeonesha nia ya kuwekeza katika ujenzi wa Kiwanda cha Baruti nchini.


Kaimu Kamishna Msaidizi wa Madini anayeshughulikia masuala ya Baruti, Chiku Juma akiongea jambo katika kikao hicho. Wengine wanaofuatilia ni Wataalam kutoka Wizara ya Madini na Afisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na ushirikiano wa Afrika Mashariki.


Waziri wa Madini Angellah Kairuki (katikati) katika picha ya pamoja na Wawakilishi wa Kampuni ya Auxin ya nchini China.  Wa pili kulia ni Kaimu Kamishna Msaidizi wa Madini anayeshughulikia masuala ya Baruti, Chiku Juma. Wa pili kulia ni Afisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na ushirikiano wa Afrika Mashariki.


Waziri wa Madini Angellah Kairuki akiangalia mfano wa vifaa vinavyotengenezwa na kampuni Kampuni ya Auxin ya nchini China.


Waziri wa Madini Angellah Kairuki akiongoza kikao kati ya Wizara ya Madini na Wawakilishi wa Kampuni ya Auxin ya nchini China.


Waziri wa Madini Angellah Kairuki akiangalia mfano wa vifaa vinavyotengenezwa na kampuni Kampuni ya Auxin ya nchini China.

Thursday, June 7, 2018

Kikao cha 21 cha Makatibu Wakuu wa Kituo cha AMGC chafanyika Tanzania


Na Rhoda James, Dar es Salaam

Makatibu Wakuu kutoka nchi Wanachama wa Kituo cha Madini na Jiosayansi cha Afrika (AMGC) wameshiriki katika kikao cha 21 cha Kituo hicho kilichopo Kunduchi, jijini Dar es Salaam.

Akifungua rasmi kikao hicho kilichofanyika tarehe 6-7 Juni, 2018, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini Tanzania, Prof. Simon Msanjila ambaye anashiriki kwa mara ya kwanza, alisema kuwa, kituo hicho hakina budi kuweka jitihada katika kuhamasisha nchi  nyingine za Afrika ambazo bado hazijajiunga ili ziweze  kujiunga  na kituo hicho.

Pia, alieleza kuhusu umuhimu wa kituo kuendelea kuweka msisito kwa nchi wanachama kulipa ada za uanachama kwa wakati na kuhakikisha kuwa kinatekeleza majukumu yake kwa ubora uliokusudiwa.

Akichangi mada, Prof. Msajila alizungumzia kuhusu suala la upatikanaji wa eneo la ujenzi wa vinu vya kuchenjua na kuongeza thamani madini na kushauri kuhusu kuzingatia suala ya uhifadhi wa mazingira.

Pia, Profesa Msajila alikitaarifu kikao hicho kuhusu ushiriki wa Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Dkt. Tito Mwinuka na Kaimu Mkurugenzi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Mhandisi Amon Maganga pamoja na Wataalam mbalimbali kutoka taasisi hizo  katika Mkutano wa 38 wa Wakuu wa nchi wanachama utakaofanyika tarehe 8 Juni, 2018.

“Nimeeleza kuhusu ushiriki wa Watendaji hao kwa lengo la kujadili suala la kufanya biashara na kituo cha AMGC kwa kuwa vipo vifaa ambavyo kituo chetu kinaweza kuvizalisha kwa matumizi ya taasisi za REA na TANESCO,” alisema Prof. Msanjila.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kikao hicho Dkt. Kojo Busia alisema kuwa, asilimia 75 ya madini ya Coltan hupita katika Bandari ya Dar es Salaam Tanzania kuelekea nchi jirani ukilinganisha na asilimia 25 ambayo hupita Mombasa nchini Kenya na kueleza umuhimu kituo hicho kuboreshwa ili kutoa huduma bora zaidi.

Pia, Dkt. Busia alisisitiza suala la kituo cha AMGC kuona namna bora ya kuungana na Taasisi ya African Minerals Development (AMDC) ili kuwa chombo kimoja ambalo litapelekea kuongeza ufanisi wa kituo hicho.

Nchi wanachama wa kituo cha AMGC ni Tanzania, Angola, Msumbiji, Sudani Kaskazini, Ethiopia, Uganda, Kenya, Comoro na Burundi.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msajila akichangia mada katika kikao cha 21 cha Makatibu wakuu kilichofanyika katika Kituo cha Madini na Jiosayansi cha Afrika (AMGC) Kunduchi, jijini Dar es Salaam. 


Wajumbe mbalimbali waliohudhuria kikao cha 21 cha Makatibu wakuu kilichofanyika katika Kituo cha Madini na Jiosayansi cha Afrika (AMGC) Kunduchi, jijini Dar es Salaam.


Mwenyekiti wa Bodi wa Kituo cha Madini na Jiosayansi cha Afrika (AMGC), Assa Mwakilembe akichangia mada katika kikao hicho. Kulia kulia kwake Mjumbe kutoka nchi ya Uganda.


Mtendaji Mkuu wa Tume ya Madini, Profesa Shukrani Manya akichangia mada katika kikao cha 21 cha Makatibu Wakuu kilichofanyika katika Kituo cha Madini na Jiosayansi cha Afrika (AMGC) Kuduchi, jijini Dar es Salaam.


Mwenyekiti wa Kikao cha 21 cha Makatibu Wakuu Dkt. Kojo Busia akichangia mada katika kikao cha 21 cha Makatibu Wakuu kilichofanyika katika Kituo cha Madini na Jiosayansi cha Afrika (AMGC) Kuduchi, jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Katibu Mkuu wa Madini, Profesa Simon Msajila na Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Madini na Jiosayansi cha Afrika (AMGC) Ibrahim Shadard.


Wajumbe mbalimbali waliohudhuria kikao cha 21 cha Makatibu wakuu kilichofanyika katika Kituo cha Madini na Jiosayansi cha Afrika (AMGC) Kunduchi, jijini Dar es Salaam.