Monday, April 29, 2019

Nyongo kupokea ujumbe wa watu kumi kutoka China


Nuru Mwasampeta na Tito Mselem

Naibu Waziri wa Madini, Stansilaus Nyongo jana tarehe 28 April, 2019 amepokea ujumbe ulioongozwa na Naibu Waziri wa Maliasili wa Jamhuri ya Watu wa China waliofika kwa ajili ya kujadili maeneo ya kushirikiana katika sekta ya madini baina ya nchi hizo mbili yaani Tanzania na China.

Akizungumza wakati akifungua kikao cha majadiliano baina ya nchi hizo mbili, Nyongo aliwahakikishia wageni hao kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imeweka mazingira mazuri ya kuwekeza nchini kupitia sekta ya Madini na kuwataka kutosita kutembelea maeneo mbalimbali ili kujionea fursa zilizopo na kuwekeza nchini Tanzania.
                     
Nyongo amewadhihirishia wageni hao uwepo wa sera na sheria  zisizokandamiza upande wowote baina ya wawekezaji, wananchi na Serikali na hivo kuzifanya pande zote kunufaika na rasilimali na uwekezaji unaofanyika katika sekta ya madini.

Aidha, Nyongo amebainisha kuwa ushirikiano baina ya Tanzania na China ni wa muda mrefu ikiwa ni takribani miaka 50 na kufika kwa ujumbe huo kunabainisha wazi kuwa  urafiki na ukaribu baina ya nchi hizo hauna mashaka.

Akizungumza na waandishi wa Habari mara baada ya mkutano huo, Nyongo alisema wataalamu kutoka China wamekuja kuunganisha nguvu ya pamoja na watanzania ili kuweza kusaidiana katika kufanya tafiti za kina katika kujua kiasi cha madini yaliyopo, namna nzuri ya kuvuna madini hayo pamoja na namna ya kuyaongezea thamani madini yaliyopo nchini kabla ya kuyasafirisha nje ya nchi.

Pia, Nyongo amebainisha kuwa China ipo tayari kuleta wataalamu katika masuala ya madini watakaojikita katika kufanya shughuli za uchimbaji wa madini.

Naibu Waziri Nyongo amebainisha kuwa ujio wa ujumbe kutoka China utasaidia kuweka makubaliano ya pamoja baina ya Taasisi ya Utafiti na Jiolojia Tanzania na Taasisi ya Jiolojia na utafiti ya nchini China katika kusimamia masuala ya utafiti wa madini katika maeneo ambayo hayajafikiwa.

Zaidi ya hayo Nyongo amewadhihirishia wageni hao uwepo wa mazingira mazuri na rafiki ya uwekezaji yanayotokana na uwepo wa sera na sheria zisizokandamiza upande wowote baina ya wawekezaji na Serikali na kuwataka kutosita kuja kuwekeza nchini.

Kwa upande wake Kaimu Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Utafiti na Jiolojia nchini Bi Yourghbert Myumbilwa amesema ushirikiano huo utaleta manufaa makubwa kwani uzoefu wa China katika masuala ya utafiti ni mkubwa hivyo itawawezesha watumishi wa taasisi hiyo kupata uelewa mkubwa katika kutekeleza majukumu yao.

Akizungumzia ujio wa ujumbe wake nchini, Naibu Waziri wa Maliasili wa China Dkt. Zhong Ziran amesema ni kuweza kujadili na kukubaliana juu ya maeneo ya kushirikiana baina ya Tanzania na China kupitia maliasili madini inayopatikana nchini.

Ushirikiano huu baina ya Taasisi ya Utafiti na Jiolojia nchini na Taasisi ya Utafiti wa Jiolojia nchini China ni matokeo ya kikao kilichofanyika mwezi Desemba, 2018 baina ya aliyekuwa Waziri wa Madini, Angellah Kairuki na Waziri wa Maliasili wa China kilichofanyika katika ofisi za Wizara ya Maliasili nchini China ambapo Mhe. Kairuki alishiriki kongamano la uwekezaji lililofanyika  nchini humo na kuibua fursa mbalimbali zilizopo katika sekta ya madini.


Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (Mbele Kushoto) akiwa na Naibu Waziri wa Maliasili wa China Dkt, Zhong Ziran (Kulia) pamoja na wajumbe walioambatana nao katika kikao kilichofanyika katika ukumbi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwl. JK Nyerere Jana. 

Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (Mbele Kushoto) akiwa na Naibu Waziri wa Maliasili wa China Dkt, Zhong Ziran (Kulia) pamoja na wajumbe walioambatana na Wajumbe alioambatana nao kutoka China wakifuatilia jambo katika kikao  kilichofanyika katika ukumbi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwl. JK Nyerere Jana.

Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo  (Kushoto-  waliokaa) akiwa na Naibu Waziri wa Maliasili wa China Dkt, Zhong Ziran (Kulia) pamoja na wajumbe walioambatana nao kutoka pande hizo mbili mara baada ya kumaliza kikao kilichofanyika mara baada ya ugeni kutoka China kuwasili.

Thursday, April 25, 2019

Wachimbaji watelekeza Madini na pikipiki kumbia msafara wa Mwenyekiti wa Tume ya Madini

Na Issa Mtuwa, Gairo

Wachimbaji wa Madini ya Rubi wilaya ya Gairo kata ya Iyombe kijiji cha Kirama, wamekimbia na kutelekeza Madini ya viwandani aina ya Rubi Nut, Pikipiki na vifaa mbalimbali vya kuchimbia baada ya kuona msafara wa Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Idris Kikula na Mwenyekiti wa ulinzi na usalama ambae pia ni Mkuu wa Wilaya (DC) ya Gairo Seriel Shaid Mchembe waliokuwa wanatembelea mgodi huo kuona shuguli za uchimbaji kwa lengo la kwenda kutatua kero zinazowakabili.

Msafara wa mwenyekiti wa Tume ya madini akiwa ameambatana na Kamishna wa Tume hiyo Dkt. Athanas Machiyeke na mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ulianza majira ya saa tatu asubuhi kuelekea  kwenye eneo la mgodi.

Wakiwa njiani msafara huo ulikubwa na changamoto baada ya gari ya Polisi iliyokuwa inaongoza msafara huo kukwama kwenye maji katikati ya mto kwa muda wa saa moja kitendo kilichopelekea kuchelewa kufika kwenye eneo la mgodi. 

Hata hivyo mara baada ya kufika kwenye nyumba ya mchimbaji mmoja alie tambuliwa kwa jina la Sadick Athuman maarufa kwa jina la (Saadam) alikutwa kijana mmoja aliejitambulisha kwa jina la Athumani mkazi wa Gairo mjini akilinda mahali apo ndipo mkuu wa Wilaya na vyombo vyake vya ulinzi na Mwenyekiti wa Tume na Kamishna waliingia ndani na kufanya msako na kukuta madini aina ya Rubi Nut yakiwa kwenye mifuko, Pikipiki moja na vifaa mbalimbali vya kuchimbia.

Alipo ulizwa bwana Athumani, nani anae miliki madini hayo, alisema ni madini ya bwana Saadam. Alipo ulizwa yeye anafanya nini alisema yeye ni kibarua tuu na mwenyewe Saadam yupo mgodini anaendelea na uchimbaji ndipo Mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama akamuamuru Athumani kwenda nae mpaka anakochimba bwana Saadam na mara baada ya kufika eneo la mgodi wachimbaji wote wakakimbia na kuelekea vichakani akiwemo bwa Saadam huku vifaa vya uchimbaji vikiwa vimetelekezwa sambamba na madini yale ya kwenye mfuko na pikipiki.

Kufuatia kitendo hicho mwenyekiti wa tume ya Madini Prof. Kikula amesikitishwa na kitendo hicho ambacho kinaashiria uchimbaji wa mgodi huo unafanyika bila kufuata sheria.

Kutokana na hali hiyoo, mwenyekiti wa tume amemuagiza afisa Madini Mkazi mkoa wa Morogoro Mhandisi Emmanuel Shija kufuatilia uhalali wa eneo hilo (Leseni na Codinates) na mwenendo mzima wa uchimbaji wake, endapo eneo hilo litakuwa na leseni mmiliki wake alipe maduhuli yote anayotakiwa kulipa tangu alipoanza na kama eneo hilo halijakatiwa leseni mgodi huo ufungwe mara moja na shuguli za uchimbaji zisitishwe mara moja.

Aidha, amesikitishwa na wachimbaji na wawekezaji katika eneo hilo kushindwa kusaidia shuguli za maendelo ya kijiji kinacho zunguka migodi hiyo ambapo ofisi yake haikumridhisha mwenyekiti wa tume.

Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Gairo amesikitishwa na wachimbaji hao kwa kukiuka sheria zinazo ongoza shuguli za uchimbaji madini, amesema amekuwa akiwahimizi mara kadhaa wachimbaji wote wilayani humo kuzingatia na kufuata taratibu kabla hawajanza kazi za uchimbaji ikiwemo kukata leseni na kulipa maduhuli ya serikali.

Kufuatia kwa tukio hilo Mchembe amepiga marufuku kwa mtu yeyote katika wilaya ya Gairo kufanya shuguli za madini bila kuwa na kibali kutoka tume ya madini.

Wakati huo huo Mchembe amemuagiza Kamanda wa Polisi wilaya ya Gairo Lugano Piter Mwakisunga kuhakikisha anamkamata Sadick Athumani ndani ya siku saba na kumfikisha kwenye vyombo vya sheria.

Wakiwa kwenye mgodi wa eneo la mwekezaji wa kampuni ya Mofar Holdings (T) Ltd Kamishna wa Tume ya Madini Dkt. Machiyeke amemsisitiza mwekezaji huyo kuzingatia taratibu na sheria katika hatua ya kuajiri wafanyakazi na vibarua na manunuzi ya bidhaa kama muongozo unavyo sema.

Dkt. Machiyeke amesema, sheria inasisitiza kutoa kipaumbele kwa wananchi waozunguka mgodi na taifa kwa nafasi kubwa kabla ya kufikiria nje ya eneo hilo na nje ya nchi.

Mwenyekiti wa Tume ya Madini na Kamishna walikuwa wanahitimisha ziara yao ya siku tano katika mkoa wa Morogoro baada ya kutembelea wilaya ya Morogoro mjini, Ulanga, Mvomero na Gairo ambapo ujumbe wake mkubwa kwa wafanyakazi wa tume na wachimbaji madini ulikuwa ni uadilifu katika kazi zaona kuepuka rushwa.

Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Kikula wa kwanza kushoto akiangalia madini ya Rubi Nut yaliyotelekezwa na mchimbaji wa madini hayo Sadick Athuman maarufu kwa jina la Saadam alie kimbia baada ya kuona msafara wa tume ya Madini na Mkuu wa Wilaya Gairo. Kulia ni Mkuu wa Wilaya Gairo Siriel Shaid Mchembe na Kamishna wa Tume ya Madini Dkt. Athanas Machiyeke.

 Msafara wa Tume ya Madini na wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama wakiwa kwenye eneo la mgodi Kijiji cha Kirama walipotembelea kukagua shuguli za uchimbaji katika eneo hilo wa mbele ni Athumani anae uongoza msafara kwenda kuonyesha anapochimba Sadick Athuan baada ya kukimbia

Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Kikula wa pili kulia akiwa na kamati ya ulinzi na usalama wilaya ya gairo ikiongozwa na mwenyekiti wake Siriel Shaid Mchembe wa tatu kushoto na wa kwanza kulia ni Kamishna wa Tume ya Madini Dkt. Athanas Machiyeke wakionyesha baadhi ya vifaa ikiwemo pikipiki iliyo telekezwa na  mchimbaji wa madini Sadick Athuman maarufu kwa jina la Saadam alie kimbia baada ya kuona msafara wa tume ya Madini. 

Tunataka kurahisisha mazingira biashara ya madini-Biteko


Ø Naibu Waziri Nyongo ataka Soko la Madini Arusha kuanzishwa haraka

Waziri wa Madini Doto Biteko amesema Serikali kupitia Wizara yake inalenga kurahisisha Mazingira ya Biashara ya Madini ikiwemo kuwalea wachimbaji na kuwataka wafanyabiashara na wachimbaji kuhakikisha wanajisimamia wenyewe kwa manufaa yao na Taifa.

Waziri Biteko ameyasema hayo alipokutana na viongozi wa Chama Cha Wafanyabiashara wa Madini Tanzania (TAMIDA), wakiongozwa na Mwenyekiti wa Chama hicho Sam Mollel ofisini kwake jijini Dodoma Aprili 10, kwa lengo la kujadili masuala mbalimbali yanayohusu biashara ya madini nchini.

Amekitaka chama hicho kuendelea kushirikiana na wizara kwa lengo la kusukuma mbele Sekta ya Madini ikiwemo kuhakikisha biashara ya madini inafanyika katika mazingira yenye kuzinufaisha pande zote na kuwasisitiza viongozi hao kuhakikisha wanachama wao wanafuata taratibu wanapofanya biashara ya madini.

Awali, kabla ya kujibu hoja zilizowasilishwa na chama hicho, Waziri Biteko amekipongeza  chama  hicho kwa kuwa kimekuwa kikitoa njia mbadala pindi kinapowasilisha changamoto na kero  zake badala ya kuishia kulalamika na kuongeza, “wizara inaona fahari kwa hilo na tunayachukulia kwa umuhimu maoni yenu,”.

Akizungumzia suala la kodi ya ongezeko la thamani na kodi ya zuio ambayo imeondolewa kwenye uchimbaji mdogo, Waziri Biteko amekitaka Chama hicho kutoa nafasi kwa serikali kufuatilia suala hilo. Waziri Biteko ameleeza hilo kufuatia hoja iliyowasilishwa na Mwenyekiti wa TAMIDA Sam Mollel ambaye ameeleza kuwa, katika mkoa wa Arusha, kodi hiyo bado inatozwa licha ya serikali kuiondoa.

Aidha, Waziri Biteko ametolea ufafanuzi wa changamoto kadhaa zilizowasilishwa na Mwenyekiti Sam Mollel kwa niaba ya chama hicho ikiwemo. Kuhusu bei elekezi, Waziri Biteko  amesema wizara itaendelea kushirikiana na wadau kuhakikisha suala hilo linakuwa shirikishi. Waziri Biteko amesema hilo baada ya TAMIDA kutoa pongezi kwa serikali kwa kutoa nafasi kwa wadau kukaa pamoja na serikali kujadili suala la bei elekezi ambapo Mwenyekiti huyo amemweleza Waziri Biteko kuwa, katika hilo, serikali na wadau wameanza vizuri.

Akitolea ufafanuzi kuhusu suala la kurejesha maonesho ya madini jijini Arusha, Waziri Biteko amesema suala la maonesho ya madini kufanyika arusha inawezekana lakini si kwa madini ya Tanzanite, na kuongeza kuwa, serikali imedhamiria kufanya shughuli zote zinazohusu madini hayo ndani ya ukuta unaozunguka machimbo ya mirerani lakini pia ikilenga kuubadilisha  mji wa  mirerani ufanane na madini hayo.

Aidha, Waziri Biteko amezungumzia suala la kuongeza wataalam wa kuthamini madini ya Tanzanite Mirerani na kueleza kuwa, kutokana na unyeti na umuhimu wa suala hilo, tayari serikali imeanza kulifanyia kazi ili kuhakikisha inaongeza idadi ya wataalam kuwezesha shughuli za uthamini Mirerani, kufanyika kwa wakati. Ufafanuzi huo umetolewa baada ya Mwenyekiti wa TAMIDA Sam Mollel kuwasilisha changamoto ya kuwepo na  upungufu wa wataalam hao.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo akizungumza katika kikao hicho, ametaka kuanzishwa haraka kwa soko la Madini jijini Arusha na kueleza kuwa, kwa upande wa wizara itahakikisha inashirikiana na serikali ya mkoa kuhakikisha soko hilo linaanzishwa haraka. Naibu Waziri Nyongo amesema hayo akijibu hoja ya Mwenyekiti wa TAMIDA Sam Mollel ambaye ameleeza katika kikao hicho kuwa, Chama hicho kinaunga mkono Serikali kuhusu uanzishwaji wa masoko ya madini na kuitaka serikali ione umuhimu wa kuanzisha soko La madini la madini mkoani arusha kuwezesha biashara ya madini ya vito kufanyika kwa urahisi.

Kuhusu vibali vya Wataalam wa masuala ya ukataji na unga’rishaji wa madini kutoka nje ya nchi, Naibu Waziri Nyongo amesema kuwa, ni kweli kwamba serikali inawahitaji wataalam hao kwa kuwa pia watawezesha kutoa ujuzi huo kwa wataalam wa ndani ili kuhamasisha viwanda vya ukataji madini na kuongeza, “ serikali inaangalia namna ya kulipatia ufumbuzi suala hilo kwa kushirikiana na mamlaka zinazohusika kwa sababu pia tunataka watu wetu wanufaike na utaalam huo”,.

Pia, ameongeza kuwa, kutokana na kulichukulia suala la uongezaji thamani madini kwa umuhimu, inakitegemea kituo cha Jemolojia Tanzania (TGC) kwa ajili ya kuzalisha wataalam na kukitaka chama hicho kusaidia kuongeza idadi ya wanafunzi wanaodahiliwa katika kituo hicho kwa kuwa hivi sasa idadi bado ni ndogo.

Kikao hicho cha Waziri na TAMIDA ni cha kwanza tangu kuteuliwa kwa Waziri wa Madini Doto Biteko kuiongoza wizara husika.

Wengine waliohudhuria kikao hicho ni Viongozi Waandamizi kutoka wizara ya Madini na Tume ya Madini.


Baadhi ya Viongozi wa Chama Cha Wafanyabiashara ya Madini Tanzania  (Tamida) wakifuatilia mkutano wao baina ya Waziri wa Madini Doto Biteko , Naibu Waziri na Viongozi wa Wizara. 

Waziri wa Madini Doto Biteko  (wa kwanza kulia) akizungumza jambo wakati wa kikao baina yake na Chama Cha Wafanyabiashara wa Madini Tanzania (TAMIDA). Wengine wanaofuatilia ni Kamishna wa Madini, Mhandisi David Mulabwa (kulia kwa Waziri) na   Ujumbe wa Chama hicho. 


Waziri wa Madini Doto Biteko katika picha ya pamoja na Viongozi wa (TAMIDA) pamoja na  Viongozi Waandamizi wa Wizara baada ya kikao.  

Agizo la Waziri halijadiliwi, ni kutekeleza–Prof. Kikula


Na Issa Mtuwa, Ulanga Morogoro

Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Idris Kikula amewataka  Watumishi wa tume hiyo ofisi ya Morogoro na Ulanga kutambua kwamba agizo la Waziri linalowataka kufuta leseni zisizofuata utaratibu wa kisheria sio la kujadili bali ni kutekeleza.

Prof. Kikula ameyasema hayo Aprili 10, 2019 wilayani Ulanga wakati akizungumza na watumishi wa tume hiyo wakati wa ziara yake.

Taarifa iliyosomwa kwake na Afisa Migodi Mkazi ofisi ya Mahenge Ulanga, Tandu Jilabi inaonyesha kuwa wilaya ya Ulanga ina leseni za wachimbaji wadogo 221 kati ya hizo ni leseni 9 tu ndio zinazofanya kazi huku leseni za uchimbaji wa kati zikiwa 5 na leseni za utafiti wa madini 13.

Kufuatia hali hiyo, Afisa Migodi Mkazi ofisi ya Mahenge ameiomba tume ya madini kufuta leseni zisizofanya kazi ili wapewe wenye uhitaji ili waweze kuziendeleza. Kufuatia ombi hilo, Mwenyekiti wa tume amesema jukumu la kuzifuta leseni hizo ni la kwake pamoja na Afisa Madini Mkazi Morogoro na halina mjadala kwakuwa muongozo wa utekeleza wa suala hilo ulishatolewa na waziri wa Madini.

“Suala la leseni zisizofanya kazi sio la kujadili, hili ni agizo la Waziri na kazi yetu ni kutekeleza na wenye kuzifuta ni ninyi, fuateni taratibu uliowekwa kwa mujibu wa sheria katika kuzifuta na sio kuzifuta lazima wote waliozishikilia leseni hizo kwa muda wote walipe fidia na wasipo fanya hivyo taratibu za kisheria zifuatwe kwani katika kipindi hicho chote serikali imekosa mapato yake. Kuanzia leo pitieni leseni zote na ifikapo Juni 30 mwaka huu leseni zote zisizo hai ziwe zimefutwa”, amesema Prof. Kikula.

Wakati huo huo, mwenyekiti wa tume amekutana na kuzungumza mwakilishi wa mwekezaji wa kampuni ya TanzGraphite (T) Ltd ambae ni Meneja Uhusiano wa Jamii na kuzungumzia kuhusu mgogoro uliopo baina ya mwekezaji huyo na baadhi ya wananchi wanaotakiwa kufanyiwa tathimini ili kupisha shuguli za uchimbaji wa madini katika eneo hilo.

Prof. Kikula ameonyesha kusikitishwa na mgogoro huo ambao amesema ni wa muda mrefu sasa na unachelewesha maendeleo ya watu na kuikosesha serikali mapato.

Ameongeza kimsingi wananchi wanapaswa kuelewa kuwa “right surface” (haki ya kumiliki vitu vilivyo juu ya ardhi) inampa mwananchi haki  ya kulipwa fidia ya mali zilizo juu ya ardhi anayo miliki lakini watambue kuwa kuna “resource right” (haki ya kumiliki raslimali zilizo chini ya ardhi) ikiwemo madini ambayo mmiliki wake ni serikali, ndio maana inapohitaji raslimali hizo humuondoa na kumfidia mliliki wa mali za juu ya ardhi, hivyo wananchi wanapo ng’ang’ania wanatakiwa walitambue hilo.

Pia, amesema kuwa, kwa mpango ulioanishwa na mwekezaji huyo unaonyesha manufaa kwa wananchi kupitia miradi ya maendeleo (CSR) ambapo amebainisha kuwa mwekezaji ameahidi kuwalipa fidia, kuwajengea nyumba za kisasa wale wote walio ndani ya eneo.

Mambo mengine ni pamoja na kuwapatia chakula kwa muda wa miaka miwili wakiwa kwenye makazi mapya watakayo jengewa na kila kaya kusomesha mtoto mmoja kwenye vyuo vya veta na wakihitimu wataajiriwa na mgodi ili waweze kupata kipato cha kusaidia na kuendeleza kaya zao.

Pamoja na hayo, mwekezaji huyo amemweleza mwenyekiti wa tume kuwa tayari wameshakubaliana kujengaa kituo cha afya, matundu ya vyoo kwa baadhi ya shule, kujenga shule na ukarabati wa vyumba vya madarasa katika shule mbalimbali. Hata hivyo hakusita kuonyesha kusikitishwa kwake na watu wachache wanaogoma kuondoka kupisha shuguli za uchimbaji huku kila kitu ikiwemo mtaji wa shuguli hizo ukiwa tayari.

Katika mgogoro huo, kaya 347 zinatakiwa kuondoka kupisha mwekezaji huyo na kati ya hizo kaya 62 ndio zinazo goma kuondoka ili mwekezaji aanze kazi ya uchimbaji. Mwenyekiti amesikitishwa na hali hiyo na na kuuomba uongozi wa mkoa na wilaya kuzungumza na kaya hizo sambamba na Baba Askofu aliyeko ndani ya eneo hilo ili mradi huo uanze kwani ni wa muda mrefu na serikali inakosa mapato.

Amesema kwa sasa anaziachia juhudi za serikali ya mkoa na wilaya katika kuupatia ufumbuzi mgogoro huo.

Mapema mwenyekiti alikutana na kufanya mazungumzo na Mkuu wa Wilaya ya Ulanga Ngolo Malenya ambapo amemshukuru kwa ushirikiano anao utoa kwa viongozi na wafanyakazi wa tume ya madini wilaya ya Ulanga.

Amesisitiza suala la uadilifu kwa wafanyakazi wa tume na amesema hilo litakuwa jambo la kwanza kulisema kila aendapo sambamba na ukusanyaji wa maduhuli ya serikali.  Aidha, amesema kipimo kikubwa cha kila mkuu wa kituo cha tume ya madini kitakuwa ni ukusanyaji wa maduhuli ambapo katika Mwaka wa Fedha 2018/2019 tume ilipangiwa kukusanya Bilioni 310 na mwaka wa fedha ujao tume imepangiwa kukusanya Bilioni 467.

Upande wake, Kamishna wa tume hiyo Dkt. Athanas Macheyeki amewakumbusha na kuwasisitiza watumishi wa tume na wachimbaji wa madini kuhakikisha wanasimamia ukusanyaji na ulipaji wa tozo na stahiki zote za serikali kwa wakati.

Amesema kwa kufanya hivyo raslimali za madini zitakuwa na tija kwa taifa kama anavyo sisitiza Rais John Pombe Magufuli kuwa anataka raslimali za madini ziwanufaishe watanzania wote na namna za kuwanufaisha ni kulipa stahiki za serikali zinazo tokana na madini ili zikatumike kujenga uchumi wa taifa.

Prof. Kikula na Dkt. Macheyeki wanaendelea na ziara yao mkoani Morogoro kukagua shuguli za Tume katika Wilaya mbalimbali ambapo leo walitembelea eneo la wachimbaaji wadogo ipanko wilayani ulanga.

Kamishna wa Tume ya Madini  Dkt. Athanas Macheyeki kushoto akizungumza jambo na Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Idris Kikula mara baada ya kuzunguka na kukagua eneo la wachimbaji lililopo Iponka eneo ambalo awali lilifungiwa kufanya shuguli za uchimbaji. 

Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Idris Kikula akionyesha jambo kwenye ramani ya mwekezaji wa Madini ya Graphite; TanzGraphite (T) Ltd. Wa tatu kushoto ni Meneja Uhusiano wa Jamii Bernad Mihayo, wa pili kushoto ni Kamishna wa Tume hiyo Dkt. Athanas Macheyeki.

Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Idris Kikula wa pili kushoto akiwa katika eneo la wachimbaji wadogo Ipanko wilayani Ulanga akipata maelezo kutoka kwa Kaimu Afisa Madini Mkazi Morogoro Mhandisi Emmanuel Shija alipotembelea kujionea namna shuguli za uchimbaji zinavyofanyika. Wa kwanza kushoto ni Kamishna wa Tume hiyo Dkt. Athanas Macheyeki.

Wednesday, April 10, 2019

Kufuatia ziara ya Naibu Waziri wa Madini, Mwakitolyo Wananchi watakiwa kumpisha mwekezaji kuchimba dhahabu


Na Greyson Mwase, Shinyanga

Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo amewataka wananchi wa kijiji cha Mwakitolyo kilichopo Wilayani Shinyanga Vijijini Mkoani Shinyanga kumpisha mwekezaji  ambaye ni  mgodi wa uchimbaji wa kati wa madini ya dhahabu wa kampuni ya  Hanan Afro Asia Geo Engineering (T) Limited kutoka China  kuendelea na maandalizi ya uchimbaji wa madini ya dhahabu, kwa kuwa ndiye aliyewekeza katika kijiji husika kwa kufuata sheria na kanuni zake.

Naibu Waziri Nyongo ametoa agizo hilo mapema leo tarehe 03 Aprili, 2019 katika mkutano wake wa hadhara na wananchi wa kijiji hicho ikiwa ni sehemu ya ziara yake katika mkoa wa Shinyanga yenye lengo la kukagua shughuli za uchimbaji na uchenjuaji wa madini, kusikiliza na kutatua kero za wachimbaji wa madini.

Katika ziara yake Naibu Waziri Nyongo aliambatana na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Jasinta Mboneko, Kaimu Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Shinyanga, Hamis Kamando, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, Hoja Mahiba, Mbunge wa Jimbo la Solwa, Ahmed Salum, wawakilishi wa vyombo vya ulinzi na usalama vya mkoa, wataalam kutoka Wizara ya Madini, Tume ya Madini pamoja na waandishi wa habari.

Alisema kuwa, kumekuwepo na mgogoro wa muda mrefu kati ya wananchi wa kijiji cha Mwakitolyo na mwekezaji kutoka nchini China ambaye ni  kampuni ya Henan Afro-Asia Geo Engineering Co. Limited ambapo malalamiko yaliwasilishwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Pombe Magufuli katika ziara yake aliyoifanya Wilayani Kahama Machi 10, 2018 ambapo alielezwa kuhusu unyanyasaji  uliofanywa wakati wa zoezi la uthamini na ulipaji wa fidia kwenye maeneo hayo kwa ajili ya kupisha uanzishwaji wa mgodi wa uchimbaji wa kati wa madini ya dhahabu.

Aliendelea kusema kuwa katika kutekeleza agizo la Rais Magufuli Machi 11, 2018 aliyekuwa Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko alitembelea eneo la Mwakitolyo linalolalamikiwa kwa lengo la kufanya mkutano na kusikiliza malalamiko ya wananchi ambapo baada ya kusikiliza malalamiko hayo aliahidi kwenda kufanyia kazi malalamiko yao na kuwapa mrejesho.

Aliendelea kueleza kuwa, iliundwa timu maalum kwa ajili ya kufanya uchunguzi kulingana na hadidu rejea iliyokuwa imepewa ambayo iliitaka timu kukutana na viongozi kuanzia ngazi ya mkoa hadi wilaya, kuainisha majina ya wananchi waliolipwa na ambao hawajalipwa fidia, vigezo vilivyotumika wakati wa uthaminishaji na ulipaji wa fidia pamoja na mapendekezo mbalimbali.

Nyongo aliendelea kufafanua kuwa, mara baada ya timu kumaliza kazi yake, ilibainika kuwa mwekezaji alilipa kiasi cha shilingi bilioni 1.63  kama fidia kwa wananchi waliokuwa katika eneo husika hivyo zoezi kukamilika kwa asilimia 99.6.

Alisisitiza kuwa pamoja na wananchi takribani 375 kulipwa fidia bado ilionekana kuwa wananchi wengi waliolipwa fidia sio wanakijiji wa Mwakitolyo na kuongeza kuwa wananchi 40 tu ndio walioonekana wamiliki halali wa mashamba pamoja na makazi.

Katika hatua nyingine Naibu Waziri Nyongo aliitaka Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga kuharakisha upatikanaji wa maeneo mapya kwa ajili ya wanananchi 40 ambao ni wamiliki halali wa makazi na mashamba katika kijiji cha Mwakitolyo ili mwekezaji aweze kuanza shughuli za uchimbaji mara moja.
Aidha, Naibu Waziri Nyongo alimtaka Mkurugenzi wa Kampuni ya Henan Afro-Asia Geo Engineering Co. Limited kuhakikisha anadumisha mahusiano na wananchi wa kijiji cha Mwakitolyo na kumtaka kuhakikisha anashiriki katika uboreshaji wa huduma za jamii kama vile afya, elimu, barabara kama Sheria ya Madini pamoja na kanuni zake inavyofafanua.

Wakati huo huo Nyongo aliwataka wananchi kumpa ushirikiano mwekezaji ili kufaidi matunda ya uwekezaji  kwenye kijiji chao ikiwa ni pamoja na ajira kwa wazawa, utoaji wa huduma za vyakula, biashara, huduma za jamii hivyo kupaisha uchumi wa kijiji hicho.

Aliendelea kusema kuwa, madini ni mali ya watanzania wote, hivyo baada ya uwekezaji kuanza kampuni hiyo italipa kodi mbalimbali kwenye halmashauri na Serikali kuu hivyo kuboresha sekta nyingine kama vile miundombinu, afya, elimu n.k.

Naye Mbunge wa Solwa, Ahmed Salum akizungumza katika mkutano huo mbali na kumpongeza Naibu Waziri Nyongo kwa kutatua mgogoro huo, aliwataka wananchi kufanya kazi kwa bidii huku wakilinda amani ya nchi.
Naye Mkurugenzi wa Kampuni ya Henan Afro-Asia Geo Engineering Co. Limited, Zhang Jiangho mbali na kuishukuru Serikali kupitia Wizara ya Madini kwa kutatua mgogoro huo  uliodumu kwa muda mrefu, aliahidi kushirikiana na wananchi wa kijiji cha Mwakitolyo kwa kuboresha  huduma za jamii na kulipa kodi na tozo mbalimbali za Serikali.


Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo akizungumza na wananchi wa kijiji cha Mwakitolyo kilichopo Wilayani Shinyanga Vijijini mkoani Shinyanga (hawapo pichani) kwenye mkutano wa hadhara uliolenga kutatua mgogoro kati yao na mwekezaji ambaye ni kampuni ya Henan Afro-Asia Geo Engineering Co. Limited tarehe 03 Aprili, 2019. 

Kutoka kushoto mbele, Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Jasinta Mboneko na Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo wakinukuu kero mbalimbali zilizokuwa zinawasilishwa na wananchi wa kijiji cha Mwakitolyo kilichopo Wilayani Shinyanga Vijijini mkoani Shinyanga (hawapo pichani) kwenye mkutano wa hadhara. 

Mmoja wa wananchi wa kijiji cha Mwakitolyo kilichopo Wilayani Shinyanga Vijijini mkoani Shinyanga  akiwasilisha kero yake kwa Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (hayupo pichani) kwenye mkutano wa hadhara. 

Sehemu ya wananchi wa kijiji cha Mwakitolyo kilichopo Wilayani Shinyanga Vijijini mkoani Shinyanga wakifuatilia ufafanuzi  uliokuwa unatolewa na Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (hayupo pichani) kwenye mkutano wa hadhara. 

Mbunge wa Solwa, Ahmed Salum akifafanua jambo kwa wananchi wa kijiji cha Mwakitolyo (hawapo pichani)

Thursday, April 4, 2019

Waziri Biteko akutana na kufanya mazungumzo na Wadau mbalimbali



Na Issa Mtuwa, Dodoma

Waziri wa Madini Doto Biteko amekutana na kufanya mazungumzo kwa nyakati tofauti na makundi mbalimbali ya wadau wa madini Aprili 3, 2019, Ofisini kwake Jijini Dodoma.

Miongoni mwa aliokutana nao ni pamoja na Kampuni ya MAGAL Security System inayojihusisha na ufungaji wa mitambo ya usalama (security system) katika maeneo mbalimbali yakiwemo ya migodini.

Mkurugenzi wa Biashara na Uendelezaji wa Masoko wa kampuni hiyo, Michael Gur Arie, amemweleza Waziri kuwa, kampuni yake inataka kufanya kazi na Wizara ya madini katika masuala ya ufungaji wa mitambo ya usalama kwenye migodi hususani Mirerani.

Amesema kuwa, kampuni hiyo ina uwezo wa kufunga mitambo Mirerani na wizara ikawa na uwezo wa kufuatilia kinacho fanyika kwenye eneo lote la mgodi huku shughuli nyingine za ofisi zikiendelea.
Akizungumza katika kikao hicho, Waziri Biteko ameishukuru kampuni ya MAGAL kwa kumtembelea na kuzungumza nae kuhusu suala la usalama hususani Mirerani. Amesema suala la usalama mirerani linapewa kipaumbele na uzito mkubwa katika kulinda raslimali hiyo ili iwanufaishe Watanzania wote.

Ameongeza kuwa, serikali imelipa kipaumbele suala la usalama katika eneo la Mirerani na Wizara imekuwa na mpango wa awamu mbili katika kutekeleza suala hilo. Amesema, Awamu ya kwanza ilikuwa ni kujenga ukuta kuzunguka eneo lote la migodi ya Mirerani na kufunga kamera na awamu ya pili inasubiri ushauri wa namna ya kutekeleza huku utekelezaaji wake ukitarajiwa kutafanyika baada ya kupitishwa kwa Bajeti ya Wizara kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.

Pia, waziri Biteko amekutana na Viongozi wa Shirikisho la Wachimbaji Wadogo Nchini (FEMATA) wakiongozwa na Rais wa Shirikisho hilo, John Bina.

Bina na ujumbe wake wamemtembelea Waziri Biteko kwa lengo la kukutana na kuzungumzia masuala mbalimbali yanayohusu shirikisho hilo ukizingatia kwamba, tangu ateuliwe kushika wadhifa huo hawajawahi kukutana na kufanya mazungumzo rasmi zaidi ya kukutana kwenye ziara mbalimbali.

Pamoja na mambo mengine, Bina amemweleza Waziri kuwa, Shirikisho lina laani vikali tukio la udanganyifu uliotokea hivi majuzi huko Chunya na kuongeza kwamba, FEMATA haikubaliana na udanganyifu unaofanywa na wachimbaji kwa kushirikiana na baadhi watendaji wa serikali waliopewa dhamana na kwamba halipo tayari kuwalinda wala kuwateteta.

Pia, Bina amezungumzia kuhusu Mgodi wa Buhemba uliofungwa na serikali akimuomba waziri kuufugua mgodi huo kwani  wanachi wengi walio katika eneo hilo wanategemea maisha yao  kutokana na uwepo wa mgodi huo.

Aidha, amemwomba Waziri maeneo mbalimbali yanayochukuliwa na serikali, afikirie kuwapatia wawekezaji wazawa ili wayaendeleze kwa  shughuli za uchimbaji. Bina ameongeza kuwa, FEMATA ina mpango wa kuanzisha Benki ya Wachimbaji (Miners Bank) kwa ajili ya kuwahudumia wachimbaji nchini.

Kwa upande wake, Waziri Biteko amemshukuru Rais wa FEMATA na ujumbe wake kwa kumtembelea. Amesema FEMATA na Wizara ya Madini huwezi kutenganisha kwa kupiga mstari kwa kuwa watu wa FEMATA ndio wadau wa wizara na kwamba hawajawahi kutofautiana na  kuomba ushirikiano huo uendelee.

Vilevile, Biteko amewashukuru FEMATA kwa kuunga mkono na kulaani kitendo cha udanganyifu uliofanywa na wachimbaji kwa kushirikiana na watendaji wa wizara huko Chunya kwa kutoa taarifa za uongo kuhusu uzalishaji wa madini.

Kuhusu kufunguliwa kwa mgodi wa Buhemba, Biteko amesema Wizara ina thamini maisha ya watu kuliko shuguli za uchimbaji na kuongeza kwamba hivi sasa kuna timu ya wataalamu ambao wamekwenda  Buhemba kufuatilia utekelezaji wa  waliyokubaliana katika kikao cha tarehe  6 Machi, 2019, na ripoti  hiyo inategemewa kuwa mwongozo wa iwapo mgodi huo ufunguliwe au ufungwe.

Akizungumzia kuhusu uanzishwaji wa Benki ya Wachimbaji amesema ni jambo zuri na kushauri kuanza na SACCOS ili kupima imani ya uaminifu wa wanchama wake katika kurejesha amana watakazo kuwa wanakopa.

Waziri Biteko amewahakikishia FEMATA kuwa wizara yake itaendelea kutoa ushirikiano mkubwa katika kutekeleza majukumu yake.


1   Waziri Doto Biteko akitoa ufafanuzi wa mambo mbalimbali kwa Michael Gur Arie, Mkurugenzi wa Biashara na Uendelezaji wa Masoko  wa Kampuni ya MAGUL Security System wa kwanza kushoto kwa Waziri alie ambatana na Idan   Segev wa kwanza kulia walipo mtembelea ofisini kwake Jijini Dodoma kwa mazungumzo


Waziri Doto Biteko katikati akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa Kampuni ya MAGUL Security System wa pili kushoto ni Omary Rajabu alie ambatana na wageni hao.

      Waziri Doto Biteko akimsikiliza Rais wa Shirikisho la Wachimbaji nchini (FEMATA), John Bina kulia wakati wa mazungumzo yao ofisini kwake Dodoma. Kushoto ni Mtendaji mkuu wa Shrikisho hilo amabe pia ni Kamishna wa Tume ya Madini Haroun Kinega. 

Waziri Doto Biteko akiongea na Viongozi wakuu wa Shirikisho la Wachimbaji nchini (FEMATA) wakati wa mazungumzo yao ofisini kwake Dodoma. Kulia  ni Rais wa Shirikisho hilo John Bina na kushoto ni Mtendaji mkuu wa Shrikisho amabe pia ni Kamishna wa Tume ya Madini Haroun Kinega

Waziri Doto Biteko katikati akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa Shirikisho la Wachimbaji nchini (FEMATA) walipo mtembelea ofisini kwake Jijini Dodoma kwa mazungumzo. Kulia  kwake ni Rais wa Shirikisho hilo John Bina na kushoto ni Mtendaji mkuu wa Shrikisho hilo amabe pia ni Kamishna wa Tume ya Madini Haroun Kinega

Wednesday, April 3, 2019

Waziri wa Madini Uganda afurahishwa na usimamizi wa sekta ya madini Nchini


Na Greyson Mwase, Geita

Waziri wa Madini Nchini Uganda, Peter Lokeris amesema kuwa amefurahishwa na usimamizi wa sekta ya madini nchini Tanzania na kusisitiza kuwa Uganda bado itaendelea kutuma wataalam wake pamoja na wachimbaji wadogo wa madini nchini Tanzania kwa ajili ya kujifunza namna bora ya uchimbaji na uchenjuaji wa madini.

Lokeris aliyasema hayo jana tarehe 02 Aprili, 2019 mara baada ya kutembelea migodi ya wachimbaji wadogo na wa kati ya madini iliyopo Wilayani Geita Mkoani Geita, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya siku nne nchini Tanzania yenye lengo la kujifunza namna Tanzania ilivyofanikiwa katika Sekta ya Madini kupitia Wizara ya Madini hususan katika kuwasaidia wachimbaji wadogo wa madini.

Akiwa ameongozana na  ujumbe wa maafisa waandamizi kutoka Serikali ya Uganda pamoja na wawakilishi wa wachimbaji wadogo aliwasili mkoani Geita na kupokelewa na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Geita ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Geita pamoja na Naibu Waziri wa Madini Nchini Tanzania, Stanslaus Nyongo.

Ziara hiyo pia ilihusisha wataalam kutoka Wizara ya Madini. Tume ya Madini, vyombo vya ulinzi na usalama vya mkoa pamoja na waandishi wa habari.

Akielezea hali iliyopelekea nchi ya Uganda kuichagua nchi ya Tanzania kama sehemu ya kujifunza kuhusu Sekta ya Madini, Lokeris alisema kuwa, baada ya kutanya  utafiti katika nchi za Aftika Mashariki, walibaini kuwa nchi ya Tanzania ni nchi iliyopiga hatua kubwa kwenye usimamizi wa sheria na kanuni za madini hali iliyopelekea wananchi wengi kunufaika nayo hususan wachimbaji wadogo wa madini.

Aliendelea kusema kuwa, Sekta ya Madini Nchini Uganda ndio inaanza kukua, hivyo wameona ni vyema kuja Tanzania  kwa ajili ya kujifunza na kwenda kuimarisha Sekta ya  Madini ili baada ya miaka kadhaa angalau iwe inakaribiana na nchi ya Tanzania.

Akielezea mikakati ya matumizi ya uzoefu mkubwa ujumbe huo ilioupata kutoka kwa nchi ya Tanzania, Waziri Lokeris alisema hatua ya kwanza itakayofanywa na Serikali ya Uganda kupitia Wizara yake ya  Madini ni kuhamasisha wachimbaji wadogo wa madini kuunda vikundi na kuwapatia leseni.

Aliongeza kuwa, mara baada ya kuwapatia leseni hatua itakayofuata itakuwa ni kuwaleta Tanzania kwa ajili ya mafunzo ambapo watajifunza kupitia wachimbaji wadogo wa madini wa Tanzania waliofanikiwa kwenye shugfhuli za uchimbaji na uchenjuaji wa madini.

Aliendelea kueleza kuwa, nia ya Serikali ya Uganda kupitia Wizara yake ya Madini ni kuhakikisha sekta hiyo inakua kwa kasi na kuanza kuzalisha dhahabu na kuuza nyingine nje ya nchi na kujipatia mapato makubwa.

“Tumefurahishwa na usimamizi mzuri kwenye sekta ya madini hususan kwenye eneo la uwezeshaji wa wachimbaji wadogo, tumeona namna wanavyochenjua madini huku wakizingatia sheria na kanuni za mazingira,”alisisitiza Waziri Lokeris.

 Naye Naibu Waziri wa Madini Nchini Tanzania, Stanslaus Nyongo akielezea mafanikio ya sekta ya madini nchini alieleza kuwa, mafaniko yaliyopatikana ni pamoja na uboreshaji wa sheria mpya ya madini pamoja na kanuni zake inayotambua madini kama mali ya watanzania na kusisitiza kuwa wachimbaji wadogo wamekuwa wanufaika kwa kiasi kikubwa.

Aliongeza kuwa, Serikali kupitia Wizara ya Madini imeondoa tozo mbalimbali zisizo za lazima hali iliyopelekea wachimbaji wadogo kuzalisha madini kwa gharama nafuu na kulipa kodi na tozo mbalimbali serikalini.

Alieleza mafanikio mengine kuwa ni pamoja na uanzishwaji wa masoko nchini kama njia mojawapo ya kudhibiti utoroshwaji wa madini kwa kuhakikisha wachimbaji wa madini wanakuwa na soko la uhakika la kuuzia madini yao kwa bei yenye faida.

Naye mmiliki wa mgodi wa  dhahabu wa Blue Reef uliopo katika eneo la Rwamgaza Wilayani Geita mkoani Geita ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama Cha Wachimbaji wa Madini Mkoa wa Geita (GEREMA), Christopher Kadeo akizungumza na  ujumbe huo uliofanya ziara kwenye mgodi wake akielezea mchango  wa mgodi wake katika jamii iliyopo jirani alisema mgodi wake tangu ulipoanzishwa mwaka 1991 mpaka sasa umefanikiwa kuajiri watumishi  160 na vibarua takribani  200.

Alieleza mafanikio mengine kuwa ni pamoja na uboreshaji wa huduma za jamii kama vile afya, elimu, ulinzi kupitia ujenzi wa vituo vya polisi na kusisitiza kuwa mgodi umekuwa ukishirikiana kwa karibu zaidi na Tasisi nyingine za Serikali kama vile Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Chuo cha Madini Dodoma (MRI), Chuo Cha Ufundi Dar es Salaam (DIT), Wizara ya Madini, Tume ya Madini na mashirika mengine ya kimataifa.

Aidha, aliongeza kuwa mgodi wake umewahi kupewa tuzo ya utunzaji bora wa mazingira na Rais wa Awamu ya Tatu ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Benjamin Mkapa.

Akielezea mikakati ya mgodi wake kwenye shughuli za uchimbaji wa madini  alisema mgodi wake unatarajia kufanya utafiti zaidi ili kugundua madini zaidi na kuunganisha leseni zake tano unazomiliki na kutoka kwenye uchimbaji wa kati hadi mkubwa.


Waziri wa Madini Nchini Uganda, Peter Lokeris na Naibu Waziri wa Madini Nchini Tanzania, Stanslaus Nyongo (katikati) wakiangalia namna kifusi cha mchanga kinavyotolewa kwenye Mgodi wa Dhahabu wa Blue Creef  uliopo Wilayani Geita Mkoani Geita unaomilikiwa na Christopher Kadeo tarehe 02 Aprili, 2019 

Waziri wa Madini Nchini Uganda, Peter Lokeris (wa pili kulia) akifafanua jambo kwenye Mgodi wa Dhahabu wa Blue Reef  uliopo Wilayani Geita Mkoani Geita unaomilikiwa na Christopher Kadeo mara baada ya yeye pamoja na ujumbe wake kufanya ziara kwenye mgodi huo. Katikati ni Naibu Waziri wa Madini Nchini Tanzania, Stanslaus Nyongo. 

Mkurugenzi wa kampuni ya Tan-Discover Mineral Consultancy Co. Ltd, Peter Kaheshi (kushoto) akitoa ufafanuzi kwa Waziri wa Madini Nchini Uganda, Peter Lokeris (kulia) mara baada ya yeye pamoja na ujumbe wake kufanya ziara katika kituo cha mfano cha Rwamgaza kwa ajili ya kutoa mafunzo ya namna bora ya uchimbaji na uchenjuaji wa madini kilichopo katika eneo la Rwamgaza Wilayani Geita Mkoani Geita. 

Mtaalam kutoka Mgodi wa Dhahabu wa Busolwa uliopo Wilayani Geita Mkoani Geita, Felix Adolf Ishebabi  (katikati) akielezea shughuli za uchimbaji wa madini ya dhahabu zinavyofanywa na mgodi huo kwa Waziri wa Madini Nchini Uganda, Peter Lokeris, Naibu Waziri wa Madini Nchini Tanzania, Stanslaus Nyongo pamoja na wajumbe kutoka Uganda na Tanzania kwenye ziara hiyo. 

Afisa Migodi Mkazi wa Mkoa wa Geita, Ernest Maganga (kulia) akielezea namna biashara ya madini inavyofanyika kwenye Soko la Madini la Geita kwa Waziri wa Madini Nchini Uganda, Peter Lokeris (kushoto) na Waziri wa Madini Nchini Tanzania, Stanslaus Nyongo (katikati) pamoja na wajumbe kutoka Uganda na Tanzania kwenye ziara hiyo