Wednesday, June 20, 2018

Wabunge wa Afrika Kusini wajifunza uzoefu sekta ya madini Tanzania


Veronica Simba na Samwel Mtuwa, Dodoma

Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini, wametembelea Wizara ya Madini kwa lengo la kujifunza na kupata uzoefu namna sekta husika inavyoendeshwa nchini.

Wawakilishi hao wa wananchi wa Afrika Kusini, walipokelewa na Waziri wa Madini Angellah Kairuki, Naibu Mawaziri Doto Biteko na Stanslaus Nyongo pamoja na Katibu Mkuu Prof Simon Msanjila, jana Juni 19, 2018, Makao Makuu ya Wizara Dodoma.

Akizungumzia nia ya ujio wao, Kiongozi wa Ujumbe huo ambaye ndiye pia Mwenyekiti wa Kamati husika, S. Khanyile alisema kuwa, walipenda kupata uzoefu wa Tanzania katika kusimamia uchimbaji mdogo wa madini pamoja na mbinu za udhibiti wa uchimbaji haramu wa madini.

Akiwasilisha Mada kwa Ujumbe huo kuhusu maeneo husika; Kamishna wa Madini Tanzania, Mhandisi David Mulabwa, alieleza kuwa, katika kusimamia uchimbaji mdogo, Serikali kupitia Wizara ya Madini inatekeleza mambo kadhaa muhimu ambayo ni pamoja na kuhakikisha wachimbaji wote wanarasimishwa kwa kupatiwa leseni.

Kamishna Mulabwa alieleza kuwa, pamoja na kuwarasimisha wachimbaji, Serikali pia inatoa mafunzo mbalimbali kwao kwa lengo la kuwajengea uelewa, inatenga maeneo ya uchimbaji kwa ajili yao pamoja na kujenga vituo vya mfano kama vile Mgodi wa Mfano wa Lwamgasa ambao pia utakuwa na Mtambo wa Uchenjuaji madini.

“Vilevile, tunasimamia pia suala la makusanyo ya kodi na tozo mbalimbali stahiki kutoka kwa sekta hii ya uchimbaji mdogo. Ili suala hili liwe na mafanikio, ni lazima kuhakikisha wachimbaji wanawezeshwa ipasavyo kupitia mafunzo na mambo mbalimbali kama nilivyoeleza awali,” alifafanua.

Aidha, aliongeza kuwa, Serikali imekuwa ikiwawezesha wachimbaji wadogo kwa kuwapatia ruzuku lakini akabainisha kuwa utaratibu huo umesitishwa kwa muda baada ya kujitokeza changamoto kadhaa, na utarejeshwa tena baada ya kuaandaa utaratibu mzuri zaidi na wenye tija katika kuendesha zoezi hilo.

Kuhusu suala la udhibiti wa uchimbaji haramu wa madini, Mhandisi Mulabwa alieleza kuwa, Tanzania imeweka mfumo mzuri wa kisheria ambao unamtaka yeyote anayejishughulisha na uchimbaji madini kuwa na leseni halali.

Alisema kuwa, Serikali pia imeweka utaratibu wa kusimamia kwa karibu shughuli zote za uchimbaji ikiwemo kufanya ukaguzi wa mara kwa mara.

 Vilevile, alisema kuwa kuimarisha mawasiliano kuanzia ngazi ya chini yaani Serikali ya Kijiji, Wilaya na hatimaye Ofisi za Madini ni muhimu sana katika udhibiti wa uchimbaji haramu.

“Kupitia mawasiliano hayo tunafanikiwa kupata taarifa zote mara moja na hivyo inatusaidia kuchukua hatua stahiki na kwa wakati stahiki.”
Kwa upande wake, Waziri Kairuki aliwashukuru wabunge hao kwa kufanya uamuzi wa kuja kujifunza Tanzania na kuomba ushirikiano baina yao uendelezwe. Wabunge hao pia walishukuru kwa ushirikiano waliopata na kusema kuwa wamefurahi kupata uzoefu wa Tanzania ambao utawasaidia katika uboreshaji wa sekta hiyo nchini kwao.


Waziri wa Madini, Angellah Kairuki (mwenye nguo ya kitenge) akiwapokea Wajumbe wa Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini, waliofika Makao Makuu ya Wizara – Dodoma, Juni 19, 2018 kujifunza na kupata uzoefu namna sekta husika inavyoendeshwa nchini. Kushoto ni Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko.


Kamishna wa Madini, Mhandisi David Mulabwa, akiwasilisha Mada kwa Wajumbe wa Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini, waliofika Makao Makuu ya Wizara – Dodoma, Juni 19, 2018 kujifunza na kupata uzoefu namna sekta husika inavyoendeshwa nchini.

Wajumbe wa Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini, waliofika Makao Makuu ya Wizara – Dodoma, Juni 19, 2018 kujifunza na kupata uzoefu namna sekta husika inavyoendeshwa nchini; wakifuatilia Mada zilizokuwa zikiwasilishwa na Kamishna wa Madini Tanzania, Mhandisi David Mulabwa (hayupo pichani).
Waziri wa Madini, Angellah Kairuki, akifafanua jambo, wakati wa kikao na Wajumbe wa Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini (hawapo pichani), waliofika Makao Makuu ya Wizara – Dodoma, Juni 19, 2018 kujifunza na kupata uzoefu namna sekta husika inavyoendeshwa nchini.
Kutoka Kulia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini, S. Khanyile, Waziri wa Madini Angellah Kairuki, Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo na Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko, wakifurahia jambo, wakati Kamati hiyo ilipotembelea Makao Makuu ya Wizara – Dodoma, Juni 19, 2018 kujifunza na kupata uzoefu namna sekta husika inavyoendeshwa nchini.

Waziri wa Madini, Angellah Kairuki (katikati) akiwapokea Wajumbe wa Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini, waliofika Makao Makuu ya Wizara – Dodoma, Juni 19, 2018 kujifunza na kupata uzoefu namna sekta husika inavyoendeshwa nchini.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila (kulia) na Makatibu wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, wakifuatilia Mada zilizokuwa zikiwasilishwa na Kamishna wa Madini Tanzania, Mhandisi David Mulabwa (hayupo pichani), wakati Wajumbe wa Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini, walipofika Makao Makuu ya Wizara – Dodoma, Juni 19, 2018 kujifunza na kupata uzoefu namna sekta husika inavyoendeshwa nchini.
Waziri wa Madini Angellah Kairuki (mwenye nguo ya kitenge), Naibu Mawaziri wa Madini Stanslaus Nyongo (kushoto kwa Waziri) na Doto Biteko (kulia kwa Waziri), wakibadilishana mawazo na Wajumbe wa Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini, waliofika Makao Makuu ya Wizara – Dodoma, Juni 19, 2018 kujifunza na kupata uzoefu namna sekta husika inavyoendeshwa nchini.

No comments:

Post a Comment