Thursday, June 21, 2018

Naibu Waziri Nyongo awaongoza Wabunge wa Afrika Kusini kujifunza usimamiaji wachimbaji wadogo


Na Mwandishi wetu, Dodoma

Ziara ya Kamati ya Jamii na Masuala ya Usalama ya Bunge la Jimbo la Ghanteng, Afrika Kusini, ambao wapo nchini kujifunza na kupata uzoefu namna Tanzania inavyoendesha sekta ya madini, imeendelea kwa wabunge hao kuwatembelea wachimbaji wadogo wa dhahabu waliopo eneo la Nori, wilayani Bahi.

Wakiongozwa na Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo, Wabunge hao walifanya ziara hiyo Juni 20, 2018, ambapo walipata fursa ya kujionea shughuli za uchimbaji wa dhahabu unaofanywa na wachimbaji wadogo katika eneo hilo na kuzungumza nao kuhusu uzoefu wao katika kazi husika.

Akizungumza kwa niaba ya wenzake, Kiongozi wa Ujumbe huo, S. Khanyile alikiri kuwa, ziara husika imewawezesha kujifunza mambo mengi na kwamba watatumia uzoefu walioupata kuboresha na kuimarisha zaidi sekta ya madini nchini kwao.

Kwa upande wake, Naibu Waziri Nyongo aliwahakikishia Wabunge hao kuwa Tanzania itaendeleza ushirikiano kati yake na nchi ya Afrika Kusini, hususan katika sekta ya madini.

Alisema, ushirikiano wa nchi hizo mbili katika sekta ya madini, utasaidia kuimarisha na kuboresha zaidi sekta husika na hivyo kuziwezesha kuwa za mfano katika uchangiaji wa Pato la Taifa na kuimarisha uchumi wa nchi na wananchi wake kwa ujumla.

Juni 19, mwaka huu, Wabunge hao walifika Makao Makuu ya Wizara ya Madini jijini Dodoma, ambapo walipokelewa na Waziri mwenye dhamana, Angellah Kairuki. Katika siku hiyo ya kwanza ya ziara yao, walipata fursa ya kujifunza kuhusu sekta husika kupitia uwasilishwaji wa Mada mbalimbali uliofanywa na Kamishna wa Madini, Mhandisi David Mulabwa.

Pichani ni matukio mbalimbali wakati wa ziara hiyo.









No comments:

Post a Comment