Friday, May 3, 2019

Katibu Mkuu Wizara ya Madini, azindua Soko la Madini Chunya


Na Greyson Mwase, Chunya

Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila amezindua Soko la Madini Chunya ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa maagizo yaliyotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli ya kutaka Wilaya ya Chunya kuhakikisha imekamilisha na kuzindua soko la madini ndani ya kipindi cha siku saba. Rais Magufuli alitoa agizo hilo tarehe 27 Aprili, 2019 wilayani Chunya katika mkutano wake na wachimbaji na wachenjuaji wa madini.

Uzinduzi huo ulishirikisha Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula, Mkuu wa Wilaya ya Chunya, Mary-Prisca Mahundi,  Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu kutoka Wizara ya Madini, Issa Nchasi, Mhasibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Anthony Tarimo na Kamishna Msaidizi-Uendelezaji wa Migodi kutoka Wizara ya Madini, Ali Ali.

Wengine walioshiriki katika uzinduzi huo ni pamoja na Mkurugenzi wa Ukaguzi na Biashara ya Madini kutoka Tume ya Madini, Dk. Venance Mwase, wawakilishi wa wachimbaji na wafanyabiashara wa madini, viongozi wa dini pamoja na vyombo vya habari.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Profesa Msanjila alisema kuwa, tangu kuingia madarakani kwa Serikali ya Awamu ya Tano, imekuwa ikisisitiza dhamira yake ya kuhakikisha Sekta ya Madini inakua, inanufaisha watanzania pamoja na kuchangia ukuaji wa Pato la Taifa.

Akielezea mafanikio ya Serikali kupitia Wizara ya Madini kwenye usimamizi  wa rasilimali za madini, Profesa Msanjila alisema kuwa,  ili kuhakikisha kuwa wananchi wote wananufahika na rasilimali za madini, Serikali ilitunga Sheria ya Mamlaka ya Nchi  Kuhusiana na Umiliki wa Maliasili Namba 5 ya Mwaka 2017; Sheria ya Mapitio na Majadiliano Kuhusu Masharti Hasi katika Mikataba ya Maliasili za Nchi Namba 6 ya mwaka 2017 pamoja na kufanya marekebisho ya Sheria ya Madini Sura ya 123.

Aliendelea kueleza kuwa Serikali pia imefuta baadhi ya tozo ambazo zilikuwa kero kwa wafanyabiashara wa madini hususan wachimbaji wadogo na kufafanua kuwa tozo hizo kuwa ni pamoja na kodi ya ongezeko la thamani (VAT) asilimia 18 na kodi ya zuio ya asilimia tano kwa wachimbaji wadogo.

Alisema kuwa, kuwekwa kwa mazingira mazuri ya kibiashara kwenye sekta ya madini pamoja na kufuta kodi na tozo mbalimbali zinazofikia asilimia 23 kutaondoa utoroshwaji wa madini na kusaidia wachimbaji wadogo kutambuliwa kupitia uanzishwaji wa masoko ya madini.

Alieleza manufaa mengine kuwa ni pamoja na kupunguza gharama za uendeshaji wa shughuli za wachimbaji wadogo na kuongeza wigo wa mapato ya nchi.

Katika hatua nyingine, Profesa Msanjila aliwataka  wachimbaji wote wadogo na wafanyabiashara wa madini  kuendelea kushirikiana na mamlaka mbalimbali  za Serikali katika kutekeleza majukumu  yao kwa kufuata sheria, kanuni, taratibu na miongozo mbalimbali  inayotolewa na Serikali.

Akielezea manufaa ya soko jipya la madini Chunya, Profesa Msanjila alisema soko litaziba mianya ambayo imekuwa chanzo cha utoroshwaji wa madini, ukwepaji kodi na hivyo kusababisha biashara nzima ya madini kufanyika kiholela katika maeneo mengi ya nchi.

Aliongeza kuwa kuanzishwa kwa Soko la Madini Chunya kutawezesha na kurahisisha biashara nzima ya madini na kuwa kiungo muhimu cha kuwakutanisha wachimbaji na wafanyabiashara kwa lengo la kuuza na kununua madini.

Profesa Msanjila aliendelea kufafanua manufaa mengine ya soko kuwa ni pamoja na kuwa suluhisho la tatizo la kupunjwa na kudhulumiwa na kuondoa  vitendo vya dhuluma ambavyo vimekuwa  vikiwahusisha wafanyabiashara wa madini wasiokuwa waaminifu kwa baadhi ya wachimbaji wadogo.

“Soko hili litaondoa  uwezekano wa wanunuzi  wa madini kuibiwa na wajanja wachache wanaojifanya  kuwa na madini wakati hawana, nawasihi wanunuzi wa madini kulitumia soko kikamilifu ili kuepuka udanganyifu na matapeli tu” alisema Profesa Msanjila.

Katika hatua nyingine Profesa Msanjila aliupongeza uongozi wa Wilaya ya Chunya, wafanyabiashara wa madini kwa kuhakikisha Soko la Madini Chunya limezinduliwa ndani ya muda uliopangwa.

Wakati huo huo akizungumzia hali ya uanzishwaji wa masoko ya madini nchini, Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula alisema kuwa, hadi kufikia sasa masoko matano ya madini yameshafunguliwa katika mikoa ya Geita, Singida, Kahama, Arusha – Namanga na Chunya.

Aliongeza kuwa masoko mengine ya madini yanatarajiwa kufunguliwa kabla ya tarehe 05 Mei, 2019 ikiwa ni pamoja na Soko la Madini ya Dhahabu na Vito vya Thamani Ruvuma, Soko la Madini Shinyanga, Soko la Madini Dodoma na Soko la Madini Mbeya.

Profesa Kikula alitaja masoko mengine ambayo yanatarajiwa kufunguliwa hivi karibuni kuwa ni pamoja na Soko la Madini ya Bati (tin) na Soko la Madini ya Dhahabu Handeni.

Alisisitiza kuwa mikoa mingine ipo katika  hatua za mwisho kukamilisha vigezo mbalimbali vikiwemo vya kiusalama na miundombinu.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila (kushoto) akisalimiana na Mkuu wa Wilaya ya Chunya, Mary-Prisca Mahundi (katikati) mara baada ya kuzindua Soko la Madini la Chunya lililopo Mjini Chunya  Mkoani Mbeya tarehe 02 Mei, 2019.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila akisoma hotuba ya uzinduzi kabla ya kuzindua Soko la Madini Chunya.

Watendaji kutoka Wizara ya Madini, Tume ya Madini na Idara nyingine za Serikali wakifuatilia hotuba  ya uzinduzi wa  Soko la Madini Chunya iliyokuwa inatolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila. (hayupo pichani).

Sehemu ya wananchi waliofika kushuhudia uzinduzi wa Soko la Madini Chunya wakifuatilia hotuba  ya uzinduzi iliyokuwa inatolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila. (hayupo pichani).

Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Soko la Madini Chunya. Kulia ni Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila, (katikati waliokaa mbele) Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula (wa pili kushoto waliokaa mbele) na   Mkuu wa Wilaya ya Chunya, Mary-Prisca Mahundi (wa nne kushoto waliokaa mbele) wakiwa katika picha ya pamoja na watendaji kutoka Wizara ya Madini, Tume ya Madini na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Chunya mara baada ya uzinduzi wa soko hilo

Biteko akutana na Viongozi Waandamizi wa Wizara na Tume ya Madini


Na Issa Mtuwa, Dodoma

Waziri wa madini Doto Biteko amewataka wafanyakazi wa wizara ya madini pamoja na taasisi zake kufanya kazi na kutekeleza majukumu yao kwa wakati ili kufikia malengo ya wizara hiyo.

Ameyasema hayo jijini Dodoma wakati wa kikao chake na viongozi waandamizi wa wizara ya madini na tume ya madini. Katika kikao hicho pamoja na mambo mengine amezungumzia juu utekelezaji wa maagizo anayoyatoa na usimamizi wa utekeleza wa maagizo yake. Ameongeza kuwa anawategemea sana viongozi hao na wafanyakazi wote katika kufanikisha kazi na malengo ya wizara hiyo.

Ametolea mfano wa maagizo aliyowahi kuyatoa ni pamoja na ufutwaji wa leseni zisizo hai ndani ya siku 7 na zingine siku 30 na lile linalo husu mgodi wa North Mara kuhusu utiririshaji wa maji yenye sumu kwenda kwenye makazi ya wananchi ambapo alitoa pia siku 30 kuhakikisha maji hayo yanadhibitiwa.

Amewaambia viongozi hao kuwa akishatoa maagizo, kazi ya kusimamia utekelezaji wa maagizo hayo ni kazi yao. Amemshukuru na kumpongeza Mwenyekiti wa Tume Prof. Idris Kikula na tume yake kwa kazi nzuri wanayoifanya na ziara zake mikoani zimekuwa na tija.

Biteko amesisitiza kuwa anatambua mchango wa watumishi wote wa wizara yake hivyo amewaomba kuongeza bidii  na kuongeza umakini katika utekelezaji wa majukumu yao huku wakizingatia weledi na uadilifu.

Kikao hicho kimehudhuriwa na Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo, Katibu Mkuu Wizara ya Madini Prof. Simon Msanjila na Makamishna. Kwa upande wa tume ya madini waliohudhuria ni pamoja na Mwenyekiti wa Tume Prof. Kikula, Mtendaji mkuu wa tume ya madini Prof. Shukrani Manya, Mkurugenzi wa Leseni Mhandisi Yahya Samamba, Mkurugenzi wa Biashara Dkt. Venance Bahati.


Waziri wa Madini Doto Biteko katikati akiongoza kikao cha kazi na viongo waandamizi wa wizara ya Madini na Tume ya Madini. Kushoto kwake ni Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo na kulia kwake Katibu Mkuu wizara ya Madini      Prof. Msanjila

Waziri wa Madini Doto Biteko katikati akisisitiza jambo wakati kikao cha kazi na viongo waandamizi wa wizara ya Madini na Tume ya Madini. Kushoto kwake ni Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo na kulia kwake Katibu Mkuu wizara ya Madini Prof. Msanjila. 

Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo akifafanua jambo wakati wa kikao kilichoitishwa na Waziri wa Madini Doto Biteko kilicho fanyika Ihumwa Jijini Dodoma.

Monday, April 29, 2019

Nyongo kupokea ujumbe wa watu kumi kutoka China


Nuru Mwasampeta na Tito Mselem

Naibu Waziri wa Madini, Stansilaus Nyongo jana tarehe 28 April, 2019 amepokea ujumbe ulioongozwa na Naibu Waziri wa Maliasili wa Jamhuri ya Watu wa China waliofika kwa ajili ya kujadili maeneo ya kushirikiana katika sekta ya madini baina ya nchi hizo mbili yaani Tanzania na China.

Akizungumza wakati akifungua kikao cha majadiliano baina ya nchi hizo mbili, Nyongo aliwahakikishia wageni hao kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imeweka mazingira mazuri ya kuwekeza nchini kupitia sekta ya Madini na kuwataka kutosita kutembelea maeneo mbalimbali ili kujionea fursa zilizopo na kuwekeza nchini Tanzania.
                     
Nyongo amewadhihirishia wageni hao uwepo wa sera na sheria  zisizokandamiza upande wowote baina ya wawekezaji, wananchi na Serikali na hivo kuzifanya pande zote kunufaika na rasilimali na uwekezaji unaofanyika katika sekta ya madini.

Aidha, Nyongo amebainisha kuwa ushirikiano baina ya Tanzania na China ni wa muda mrefu ikiwa ni takribani miaka 50 na kufika kwa ujumbe huo kunabainisha wazi kuwa  urafiki na ukaribu baina ya nchi hizo hauna mashaka.

Akizungumza na waandishi wa Habari mara baada ya mkutano huo, Nyongo alisema wataalamu kutoka China wamekuja kuunganisha nguvu ya pamoja na watanzania ili kuweza kusaidiana katika kufanya tafiti za kina katika kujua kiasi cha madini yaliyopo, namna nzuri ya kuvuna madini hayo pamoja na namna ya kuyaongezea thamani madini yaliyopo nchini kabla ya kuyasafirisha nje ya nchi.

Pia, Nyongo amebainisha kuwa China ipo tayari kuleta wataalamu katika masuala ya madini watakaojikita katika kufanya shughuli za uchimbaji wa madini.

Naibu Waziri Nyongo amebainisha kuwa ujio wa ujumbe kutoka China utasaidia kuweka makubaliano ya pamoja baina ya Taasisi ya Utafiti na Jiolojia Tanzania na Taasisi ya Jiolojia na utafiti ya nchini China katika kusimamia masuala ya utafiti wa madini katika maeneo ambayo hayajafikiwa.

Zaidi ya hayo Nyongo amewadhihirishia wageni hao uwepo wa mazingira mazuri na rafiki ya uwekezaji yanayotokana na uwepo wa sera na sheria zisizokandamiza upande wowote baina ya wawekezaji na Serikali na kuwataka kutosita kuja kuwekeza nchini.

Kwa upande wake Kaimu Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Utafiti na Jiolojia nchini Bi Yourghbert Myumbilwa amesema ushirikiano huo utaleta manufaa makubwa kwani uzoefu wa China katika masuala ya utafiti ni mkubwa hivyo itawawezesha watumishi wa taasisi hiyo kupata uelewa mkubwa katika kutekeleza majukumu yao.

Akizungumzia ujio wa ujumbe wake nchini, Naibu Waziri wa Maliasili wa China Dkt. Zhong Ziran amesema ni kuweza kujadili na kukubaliana juu ya maeneo ya kushirikiana baina ya Tanzania na China kupitia maliasili madini inayopatikana nchini.

Ushirikiano huu baina ya Taasisi ya Utafiti na Jiolojia nchini na Taasisi ya Utafiti wa Jiolojia nchini China ni matokeo ya kikao kilichofanyika mwezi Desemba, 2018 baina ya aliyekuwa Waziri wa Madini, Angellah Kairuki na Waziri wa Maliasili wa China kilichofanyika katika ofisi za Wizara ya Maliasili nchini China ambapo Mhe. Kairuki alishiriki kongamano la uwekezaji lililofanyika  nchini humo na kuibua fursa mbalimbali zilizopo katika sekta ya madini.


Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (Mbele Kushoto) akiwa na Naibu Waziri wa Maliasili wa China Dkt, Zhong Ziran (Kulia) pamoja na wajumbe walioambatana nao katika kikao kilichofanyika katika ukumbi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwl. JK Nyerere Jana. 

Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (Mbele Kushoto) akiwa na Naibu Waziri wa Maliasili wa China Dkt, Zhong Ziran (Kulia) pamoja na wajumbe walioambatana na Wajumbe alioambatana nao kutoka China wakifuatilia jambo katika kikao  kilichofanyika katika ukumbi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwl. JK Nyerere Jana.

Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo  (Kushoto-  waliokaa) akiwa na Naibu Waziri wa Maliasili wa China Dkt, Zhong Ziran (Kulia) pamoja na wajumbe walioambatana nao kutoka pande hizo mbili mara baada ya kumaliza kikao kilichofanyika mara baada ya ugeni kutoka China kuwasili.

Thursday, April 25, 2019

Wachimbaji watelekeza Madini na pikipiki kumbia msafara wa Mwenyekiti wa Tume ya Madini

Na Issa Mtuwa, Gairo

Wachimbaji wa Madini ya Rubi wilaya ya Gairo kata ya Iyombe kijiji cha Kirama, wamekimbia na kutelekeza Madini ya viwandani aina ya Rubi Nut, Pikipiki na vifaa mbalimbali vya kuchimbia baada ya kuona msafara wa Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Idris Kikula na Mwenyekiti wa ulinzi na usalama ambae pia ni Mkuu wa Wilaya (DC) ya Gairo Seriel Shaid Mchembe waliokuwa wanatembelea mgodi huo kuona shuguli za uchimbaji kwa lengo la kwenda kutatua kero zinazowakabili.

Msafara wa mwenyekiti wa Tume ya madini akiwa ameambatana na Kamishna wa Tume hiyo Dkt. Athanas Machiyeke na mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ulianza majira ya saa tatu asubuhi kuelekea  kwenye eneo la mgodi.

Wakiwa njiani msafara huo ulikubwa na changamoto baada ya gari ya Polisi iliyokuwa inaongoza msafara huo kukwama kwenye maji katikati ya mto kwa muda wa saa moja kitendo kilichopelekea kuchelewa kufika kwenye eneo la mgodi. 

Hata hivyo mara baada ya kufika kwenye nyumba ya mchimbaji mmoja alie tambuliwa kwa jina la Sadick Athuman maarufa kwa jina la (Saadam) alikutwa kijana mmoja aliejitambulisha kwa jina la Athumani mkazi wa Gairo mjini akilinda mahali apo ndipo mkuu wa Wilaya na vyombo vyake vya ulinzi na Mwenyekiti wa Tume na Kamishna waliingia ndani na kufanya msako na kukuta madini aina ya Rubi Nut yakiwa kwenye mifuko, Pikipiki moja na vifaa mbalimbali vya kuchimbia.

Alipo ulizwa bwana Athumani, nani anae miliki madini hayo, alisema ni madini ya bwana Saadam. Alipo ulizwa yeye anafanya nini alisema yeye ni kibarua tuu na mwenyewe Saadam yupo mgodini anaendelea na uchimbaji ndipo Mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama akamuamuru Athumani kwenda nae mpaka anakochimba bwana Saadam na mara baada ya kufika eneo la mgodi wachimbaji wote wakakimbia na kuelekea vichakani akiwemo bwa Saadam huku vifaa vya uchimbaji vikiwa vimetelekezwa sambamba na madini yale ya kwenye mfuko na pikipiki.

Kufuatia kitendo hicho mwenyekiti wa tume ya Madini Prof. Kikula amesikitishwa na kitendo hicho ambacho kinaashiria uchimbaji wa mgodi huo unafanyika bila kufuata sheria.

Kutokana na hali hiyoo, mwenyekiti wa tume amemuagiza afisa Madini Mkazi mkoa wa Morogoro Mhandisi Emmanuel Shija kufuatilia uhalali wa eneo hilo (Leseni na Codinates) na mwenendo mzima wa uchimbaji wake, endapo eneo hilo litakuwa na leseni mmiliki wake alipe maduhuli yote anayotakiwa kulipa tangu alipoanza na kama eneo hilo halijakatiwa leseni mgodi huo ufungwe mara moja na shuguli za uchimbaji zisitishwe mara moja.

Aidha, amesikitishwa na wachimbaji na wawekezaji katika eneo hilo kushindwa kusaidia shuguli za maendelo ya kijiji kinacho zunguka migodi hiyo ambapo ofisi yake haikumridhisha mwenyekiti wa tume.

Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Gairo amesikitishwa na wachimbaji hao kwa kukiuka sheria zinazo ongoza shuguli za uchimbaji madini, amesema amekuwa akiwahimizi mara kadhaa wachimbaji wote wilayani humo kuzingatia na kufuata taratibu kabla hawajanza kazi za uchimbaji ikiwemo kukata leseni na kulipa maduhuli ya serikali.

Kufuatia kwa tukio hilo Mchembe amepiga marufuku kwa mtu yeyote katika wilaya ya Gairo kufanya shuguli za madini bila kuwa na kibali kutoka tume ya madini.

Wakati huo huo Mchembe amemuagiza Kamanda wa Polisi wilaya ya Gairo Lugano Piter Mwakisunga kuhakikisha anamkamata Sadick Athumani ndani ya siku saba na kumfikisha kwenye vyombo vya sheria.

Wakiwa kwenye mgodi wa eneo la mwekezaji wa kampuni ya Mofar Holdings (T) Ltd Kamishna wa Tume ya Madini Dkt. Machiyeke amemsisitiza mwekezaji huyo kuzingatia taratibu na sheria katika hatua ya kuajiri wafanyakazi na vibarua na manunuzi ya bidhaa kama muongozo unavyo sema.

Dkt. Machiyeke amesema, sheria inasisitiza kutoa kipaumbele kwa wananchi waozunguka mgodi na taifa kwa nafasi kubwa kabla ya kufikiria nje ya eneo hilo na nje ya nchi.

Mwenyekiti wa Tume ya Madini na Kamishna walikuwa wanahitimisha ziara yao ya siku tano katika mkoa wa Morogoro baada ya kutembelea wilaya ya Morogoro mjini, Ulanga, Mvomero na Gairo ambapo ujumbe wake mkubwa kwa wafanyakazi wa tume na wachimbaji madini ulikuwa ni uadilifu katika kazi zaona kuepuka rushwa.

Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Kikula wa kwanza kushoto akiangalia madini ya Rubi Nut yaliyotelekezwa na mchimbaji wa madini hayo Sadick Athuman maarufu kwa jina la Saadam alie kimbia baada ya kuona msafara wa tume ya Madini na Mkuu wa Wilaya Gairo. Kulia ni Mkuu wa Wilaya Gairo Siriel Shaid Mchembe na Kamishna wa Tume ya Madini Dkt. Athanas Machiyeke.

 Msafara wa Tume ya Madini na wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama wakiwa kwenye eneo la mgodi Kijiji cha Kirama walipotembelea kukagua shuguli za uchimbaji katika eneo hilo wa mbele ni Athumani anae uongoza msafara kwenda kuonyesha anapochimba Sadick Athuan baada ya kukimbia

Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Kikula wa pili kulia akiwa na kamati ya ulinzi na usalama wilaya ya gairo ikiongozwa na mwenyekiti wake Siriel Shaid Mchembe wa tatu kushoto na wa kwanza kulia ni Kamishna wa Tume ya Madini Dkt. Athanas Machiyeke wakionyesha baadhi ya vifaa ikiwemo pikipiki iliyo telekezwa na  mchimbaji wa madini Sadick Athuman maarufu kwa jina la Saadam alie kimbia baada ya kuona msafara wa tume ya Madini. 

Tunataka kurahisisha mazingira biashara ya madini-Biteko


Ø Naibu Waziri Nyongo ataka Soko la Madini Arusha kuanzishwa haraka

Waziri wa Madini Doto Biteko amesema Serikali kupitia Wizara yake inalenga kurahisisha Mazingira ya Biashara ya Madini ikiwemo kuwalea wachimbaji na kuwataka wafanyabiashara na wachimbaji kuhakikisha wanajisimamia wenyewe kwa manufaa yao na Taifa.

Waziri Biteko ameyasema hayo alipokutana na viongozi wa Chama Cha Wafanyabiashara wa Madini Tanzania (TAMIDA), wakiongozwa na Mwenyekiti wa Chama hicho Sam Mollel ofisini kwake jijini Dodoma Aprili 10, kwa lengo la kujadili masuala mbalimbali yanayohusu biashara ya madini nchini.

Amekitaka chama hicho kuendelea kushirikiana na wizara kwa lengo la kusukuma mbele Sekta ya Madini ikiwemo kuhakikisha biashara ya madini inafanyika katika mazingira yenye kuzinufaisha pande zote na kuwasisitiza viongozi hao kuhakikisha wanachama wao wanafuata taratibu wanapofanya biashara ya madini.

Awali, kabla ya kujibu hoja zilizowasilishwa na chama hicho, Waziri Biteko amekipongeza  chama  hicho kwa kuwa kimekuwa kikitoa njia mbadala pindi kinapowasilisha changamoto na kero  zake badala ya kuishia kulalamika na kuongeza, “wizara inaona fahari kwa hilo na tunayachukulia kwa umuhimu maoni yenu,”.

Akizungumzia suala la kodi ya ongezeko la thamani na kodi ya zuio ambayo imeondolewa kwenye uchimbaji mdogo, Waziri Biteko amekitaka Chama hicho kutoa nafasi kwa serikali kufuatilia suala hilo. Waziri Biteko ameleeza hilo kufuatia hoja iliyowasilishwa na Mwenyekiti wa TAMIDA Sam Mollel ambaye ameeleza kuwa, katika mkoa wa Arusha, kodi hiyo bado inatozwa licha ya serikali kuiondoa.

Aidha, Waziri Biteko ametolea ufafanuzi wa changamoto kadhaa zilizowasilishwa na Mwenyekiti Sam Mollel kwa niaba ya chama hicho ikiwemo. Kuhusu bei elekezi, Waziri Biteko  amesema wizara itaendelea kushirikiana na wadau kuhakikisha suala hilo linakuwa shirikishi. Waziri Biteko amesema hilo baada ya TAMIDA kutoa pongezi kwa serikali kwa kutoa nafasi kwa wadau kukaa pamoja na serikali kujadili suala la bei elekezi ambapo Mwenyekiti huyo amemweleza Waziri Biteko kuwa, katika hilo, serikali na wadau wameanza vizuri.

Akitolea ufafanuzi kuhusu suala la kurejesha maonesho ya madini jijini Arusha, Waziri Biteko amesema suala la maonesho ya madini kufanyika arusha inawezekana lakini si kwa madini ya Tanzanite, na kuongeza kuwa, serikali imedhamiria kufanya shughuli zote zinazohusu madini hayo ndani ya ukuta unaozunguka machimbo ya mirerani lakini pia ikilenga kuubadilisha  mji wa  mirerani ufanane na madini hayo.

Aidha, Waziri Biteko amezungumzia suala la kuongeza wataalam wa kuthamini madini ya Tanzanite Mirerani na kueleza kuwa, kutokana na unyeti na umuhimu wa suala hilo, tayari serikali imeanza kulifanyia kazi ili kuhakikisha inaongeza idadi ya wataalam kuwezesha shughuli za uthamini Mirerani, kufanyika kwa wakati. Ufafanuzi huo umetolewa baada ya Mwenyekiti wa TAMIDA Sam Mollel kuwasilisha changamoto ya kuwepo na  upungufu wa wataalam hao.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo akizungumza katika kikao hicho, ametaka kuanzishwa haraka kwa soko la Madini jijini Arusha na kueleza kuwa, kwa upande wa wizara itahakikisha inashirikiana na serikali ya mkoa kuhakikisha soko hilo linaanzishwa haraka. Naibu Waziri Nyongo amesema hayo akijibu hoja ya Mwenyekiti wa TAMIDA Sam Mollel ambaye ameleeza katika kikao hicho kuwa, Chama hicho kinaunga mkono Serikali kuhusu uanzishwaji wa masoko ya madini na kuitaka serikali ione umuhimu wa kuanzisha soko La madini la madini mkoani arusha kuwezesha biashara ya madini ya vito kufanyika kwa urahisi.

Kuhusu vibali vya Wataalam wa masuala ya ukataji na unga’rishaji wa madini kutoka nje ya nchi, Naibu Waziri Nyongo amesema kuwa, ni kweli kwamba serikali inawahitaji wataalam hao kwa kuwa pia watawezesha kutoa ujuzi huo kwa wataalam wa ndani ili kuhamasisha viwanda vya ukataji madini na kuongeza, “ serikali inaangalia namna ya kulipatia ufumbuzi suala hilo kwa kushirikiana na mamlaka zinazohusika kwa sababu pia tunataka watu wetu wanufaike na utaalam huo”,.

Pia, ameongeza kuwa, kutokana na kulichukulia suala la uongezaji thamani madini kwa umuhimu, inakitegemea kituo cha Jemolojia Tanzania (TGC) kwa ajili ya kuzalisha wataalam na kukitaka chama hicho kusaidia kuongeza idadi ya wanafunzi wanaodahiliwa katika kituo hicho kwa kuwa hivi sasa idadi bado ni ndogo.

Kikao hicho cha Waziri na TAMIDA ni cha kwanza tangu kuteuliwa kwa Waziri wa Madini Doto Biteko kuiongoza wizara husika.

Wengine waliohudhuria kikao hicho ni Viongozi Waandamizi kutoka wizara ya Madini na Tume ya Madini.


Baadhi ya Viongozi wa Chama Cha Wafanyabiashara ya Madini Tanzania  (Tamida) wakifuatilia mkutano wao baina ya Waziri wa Madini Doto Biteko , Naibu Waziri na Viongozi wa Wizara. 

Waziri wa Madini Doto Biteko  (wa kwanza kulia) akizungumza jambo wakati wa kikao baina yake na Chama Cha Wafanyabiashara wa Madini Tanzania (TAMIDA). Wengine wanaofuatilia ni Kamishna wa Madini, Mhandisi David Mulabwa (kulia kwa Waziri) na   Ujumbe wa Chama hicho. 


Waziri wa Madini Doto Biteko katika picha ya pamoja na Viongozi wa (TAMIDA) pamoja na  Viongozi Waandamizi wa Wizara baada ya kikao.  

Agizo la Waziri halijadiliwi, ni kutekeleza–Prof. Kikula


Na Issa Mtuwa, Ulanga Morogoro

Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Idris Kikula amewataka  Watumishi wa tume hiyo ofisi ya Morogoro na Ulanga kutambua kwamba agizo la Waziri linalowataka kufuta leseni zisizofuata utaratibu wa kisheria sio la kujadili bali ni kutekeleza.

Prof. Kikula ameyasema hayo Aprili 10, 2019 wilayani Ulanga wakati akizungumza na watumishi wa tume hiyo wakati wa ziara yake.

Taarifa iliyosomwa kwake na Afisa Migodi Mkazi ofisi ya Mahenge Ulanga, Tandu Jilabi inaonyesha kuwa wilaya ya Ulanga ina leseni za wachimbaji wadogo 221 kati ya hizo ni leseni 9 tu ndio zinazofanya kazi huku leseni za uchimbaji wa kati zikiwa 5 na leseni za utafiti wa madini 13.

Kufuatia hali hiyo, Afisa Migodi Mkazi ofisi ya Mahenge ameiomba tume ya madini kufuta leseni zisizofanya kazi ili wapewe wenye uhitaji ili waweze kuziendeleza. Kufuatia ombi hilo, Mwenyekiti wa tume amesema jukumu la kuzifuta leseni hizo ni la kwake pamoja na Afisa Madini Mkazi Morogoro na halina mjadala kwakuwa muongozo wa utekeleza wa suala hilo ulishatolewa na waziri wa Madini.

“Suala la leseni zisizofanya kazi sio la kujadili, hili ni agizo la Waziri na kazi yetu ni kutekeleza na wenye kuzifuta ni ninyi, fuateni taratibu uliowekwa kwa mujibu wa sheria katika kuzifuta na sio kuzifuta lazima wote waliozishikilia leseni hizo kwa muda wote walipe fidia na wasipo fanya hivyo taratibu za kisheria zifuatwe kwani katika kipindi hicho chote serikali imekosa mapato yake. Kuanzia leo pitieni leseni zote na ifikapo Juni 30 mwaka huu leseni zote zisizo hai ziwe zimefutwa”, amesema Prof. Kikula.

Wakati huo huo, mwenyekiti wa tume amekutana na kuzungumza mwakilishi wa mwekezaji wa kampuni ya TanzGraphite (T) Ltd ambae ni Meneja Uhusiano wa Jamii na kuzungumzia kuhusu mgogoro uliopo baina ya mwekezaji huyo na baadhi ya wananchi wanaotakiwa kufanyiwa tathimini ili kupisha shuguli za uchimbaji wa madini katika eneo hilo.

Prof. Kikula ameonyesha kusikitishwa na mgogoro huo ambao amesema ni wa muda mrefu sasa na unachelewesha maendeleo ya watu na kuikosesha serikali mapato.

Ameongeza kimsingi wananchi wanapaswa kuelewa kuwa “right surface” (haki ya kumiliki vitu vilivyo juu ya ardhi) inampa mwananchi haki  ya kulipwa fidia ya mali zilizo juu ya ardhi anayo miliki lakini watambue kuwa kuna “resource right” (haki ya kumiliki raslimali zilizo chini ya ardhi) ikiwemo madini ambayo mmiliki wake ni serikali, ndio maana inapohitaji raslimali hizo humuondoa na kumfidia mliliki wa mali za juu ya ardhi, hivyo wananchi wanapo ng’ang’ania wanatakiwa walitambue hilo.

Pia, amesema kuwa, kwa mpango ulioanishwa na mwekezaji huyo unaonyesha manufaa kwa wananchi kupitia miradi ya maendeleo (CSR) ambapo amebainisha kuwa mwekezaji ameahidi kuwalipa fidia, kuwajengea nyumba za kisasa wale wote walio ndani ya eneo.

Mambo mengine ni pamoja na kuwapatia chakula kwa muda wa miaka miwili wakiwa kwenye makazi mapya watakayo jengewa na kila kaya kusomesha mtoto mmoja kwenye vyuo vya veta na wakihitimu wataajiriwa na mgodi ili waweze kupata kipato cha kusaidia na kuendeleza kaya zao.

Pamoja na hayo, mwekezaji huyo amemweleza mwenyekiti wa tume kuwa tayari wameshakubaliana kujengaa kituo cha afya, matundu ya vyoo kwa baadhi ya shule, kujenga shule na ukarabati wa vyumba vya madarasa katika shule mbalimbali. Hata hivyo hakusita kuonyesha kusikitishwa kwake na watu wachache wanaogoma kuondoka kupisha shuguli za uchimbaji huku kila kitu ikiwemo mtaji wa shuguli hizo ukiwa tayari.

Katika mgogoro huo, kaya 347 zinatakiwa kuondoka kupisha mwekezaji huyo na kati ya hizo kaya 62 ndio zinazo goma kuondoka ili mwekezaji aanze kazi ya uchimbaji. Mwenyekiti amesikitishwa na hali hiyo na na kuuomba uongozi wa mkoa na wilaya kuzungumza na kaya hizo sambamba na Baba Askofu aliyeko ndani ya eneo hilo ili mradi huo uanze kwani ni wa muda mrefu na serikali inakosa mapato.

Amesema kwa sasa anaziachia juhudi za serikali ya mkoa na wilaya katika kuupatia ufumbuzi mgogoro huo.

Mapema mwenyekiti alikutana na kufanya mazungumzo na Mkuu wa Wilaya ya Ulanga Ngolo Malenya ambapo amemshukuru kwa ushirikiano anao utoa kwa viongozi na wafanyakazi wa tume ya madini wilaya ya Ulanga.

Amesisitiza suala la uadilifu kwa wafanyakazi wa tume na amesema hilo litakuwa jambo la kwanza kulisema kila aendapo sambamba na ukusanyaji wa maduhuli ya serikali.  Aidha, amesema kipimo kikubwa cha kila mkuu wa kituo cha tume ya madini kitakuwa ni ukusanyaji wa maduhuli ambapo katika Mwaka wa Fedha 2018/2019 tume ilipangiwa kukusanya Bilioni 310 na mwaka wa fedha ujao tume imepangiwa kukusanya Bilioni 467.

Upande wake, Kamishna wa tume hiyo Dkt. Athanas Macheyeki amewakumbusha na kuwasisitiza watumishi wa tume na wachimbaji wa madini kuhakikisha wanasimamia ukusanyaji na ulipaji wa tozo na stahiki zote za serikali kwa wakati.

Amesema kwa kufanya hivyo raslimali za madini zitakuwa na tija kwa taifa kama anavyo sisitiza Rais John Pombe Magufuli kuwa anataka raslimali za madini ziwanufaishe watanzania wote na namna za kuwanufaisha ni kulipa stahiki za serikali zinazo tokana na madini ili zikatumike kujenga uchumi wa taifa.

Prof. Kikula na Dkt. Macheyeki wanaendelea na ziara yao mkoani Morogoro kukagua shuguli za Tume katika Wilaya mbalimbali ambapo leo walitembelea eneo la wachimbaaji wadogo ipanko wilayani ulanga.

Kamishna wa Tume ya Madini  Dkt. Athanas Macheyeki kushoto akizungumza jambo na Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Idris Kikula mara baada ya kuzunguka na kukagua eneo la wachimbaji lililopo Iponka eneo ambalo awali lilifungiwa kufanya shuguli za uchimbaji. 

Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Idris Kikula akionyesha jambo kwenye ramani ya mwekezaji wa Madini ya Graphite; TanzGraphite (T) Ltd. Wa tatu kushoto ni Meneja Uhusiano wa Jamii Bernad Mihayo, wa pili kushoto ni Kamishna wa Tume hiyo Dkt. Athanas Macheyeki.

Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Idris Kikula wa pili kushoto akiwa katika eneo la wachimbaji wadogo Ipanko wilayani Ulanga akipata maelezo kutoka kwa Kaimu Afisa Madini Mkazi Morogoro Mhandisi Emmanuel Shija alipotembelea kujionea namna shuguli za uchimbaji zinavyofanyika. Wa kwanza kushoto ni Kamishna wa Tume hiyo Dkt. Athanas Macheyeki.

Wednesday, April 10, 2019

Kufuatia ziara ya Naibu Waziri wa Madini, Mwakitolyo Wananchi watakiwa kumpisha mwekezaji kuchimba dhahabu


Na Greyson Mwase, Shinyanga

Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo amewataka wananchi wa kijiji cha Mwakitolyo kilichopo Wilayani Shinyanga Vijijini Mkoani Shinyanga kumpisha mwekezaji  ambaye ni  mgodi wa uchimbaji wa kati wa madini ya dhahabu wa kampuni ya  Hanan Afro Asia Geo Engineering (T) Limited kutoka China  kuendelea na maandalizi ya uchimbaji wa madini ya dhahabu, kwa kuwa ndiye aliyewekeza katika kijiji husika kwa kufuata sheria na kanuni zake.

Naibu Waziri Nyongo ametoa agizo hilo mapema leo tarehe 03 Aprili, 2019 katika mkutano wake wa hadhara na wananchi wa kijiji hicho ikiwa ni sehemu ya ziara yake katika mkoa wa Shinyanga yenye lengo la kukagua shughuli za uchimbaji na uchenjuaji wa madini, kusikiliza na kutatua kero za wachimbaji wa madini.

Katika ziara yake Naibu Waziri Nyongo aliambatana na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Jasinta Mboneko, Kaimu Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Shinyanga, Hamis Kamando, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, Hoja Mahiba, Mbunge wa Jimbo la Solwa, Ahmed Salum, wawakilishi wa vyombo vya ulinzi na usalama vya mkoa, wataalam kutoka Wizara ya Madini, Tume ya Madini pamoja na waandishi wa habari.

Alisema kuwa, kumekuwepo na mgogoro wa muda mrefu kati ya wananchi wa kijiji cha Mwakitolyo na mwekezaji kutoka nchini China ambaye ni  kampuni ya Henan Afro-Asia Geo Engineering Co. Limited ambapo malalamiko yaliwasilishwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Pombe Magufuli katika ziara yake aliyoifanya Wilayani Kahama Machi 10, 2018 ambapo alielezwa kuhusu unyanyasaji  uliofanywa wakati wa zoezi la uthamini na ulipaji wa fidia kwenye maeneo hayo kwa ajili ya kupisha uanzishwaji wa mgodi wa uchimbaji wa kati wa madini ya dhahabu.

Aliendelea kusema kuwa katika kutekeleza agizo la Rais Magufuli Machi 11, 2018 aliyekuwa Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko alitembelea eneo la Mwakitolyo linalolalamikiwa kwa lengo la kufanya mkutano na kusikiliza malalamiko ya wananchi ambapo baada ya kusikiliza malalamiko hayo aliahidi kwenda kufanyia kazi malalamiko yao na kuwapa mrejesho.

Aliendelea kueleza kuwa, iliundwa timu maalum kwa ajili ya kufanya uchunguzi kulingana na hadidu rejea iliyokuwa imepewa ambayo iliitaka timu kukutana na viongozi kuanzia ngazi ya mkoa hadi wilaya, kuainisha majina ya wananchi waliolipwa na ambao hawajalipwa fidia, vigezo vilivyotumika wakati wa uthaminishaji na ulipaji wa fidia pamoja na mapendekezo mbalimbali.

Nyongo aliendelea kufafanua kuwa, mara baada ya timu kumaliza kazi yake, ilibainika kuwa mwekezaji alilipa kiasi cha shilingi bilioni 1.63  kama fidia kwa wananchi waliokuwa katika eneo husika hivyo zoezi kukamilika kwa asilimia 99.6.

Alisisitiza kuwa pamoja na wananchi takribani 375 kulipwa fidia bado ilionekana kuwa wananchi wengi waliolipwa fidia sio wanakijiji wa Mwakitolyo na kuongeza kuwa wananchi 40 tu ndio walioonekana wamiliki halali wa mashamba pamoja na makazi.

Katika hatua nyingine Naibu Waziri Nyongo aliitaka Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga kuharakisha upatikanaji wa maeneo mapya kwa ajili ya wanananchi 40 ambao ni wamiliki halali wa makazi na mashamba katika kijiji cha Mwakitolyo ili mwekezaji aweze kuanza shughuli za uchimbaji mara moja.
Aidha, Naibu Waziri Nyongo alimtaka Mkurugenzi wa Kampuni ya Henan Afro-Asia Geo Engineering Co. Limited kuhakikisha anadumisha mahusiano na wananchi wa kijiji cha Mwakitolyo na kumtaka kuhakikisha anashiriki katika uboreshaji wa huduma za jamii kama vile afya, elimu, barabara kama Sheria ya Madini pamoja na kanuni zake inavyofafanua.

Wakati huo huo Nyongo aliwataka wananchi kumpa ushirikiano mwekezaji ili kufaidi matunda ya uwekezaji  kwenye kijiji chao ikiwa ni pamoja na ajira kwa wazawa, utoaji wa huduma za vyakula, biashara, huduma za jamii hivyo kupaisha uchumi wa kijiji hicho.

Aliendelea kusema kuwa, madini ni mali ya watanzania wote, hivyo baada ya uwekezaji kuanza kampuni hiyo italipa kodi mbalimbali kwenye halmashauri na Serikali kuu hivyo kuboresha sekta nyingine kama vile miundombinu, afya, elimu n.k.

Naye Mbunge wa Solwa, Ahmed Salum akizungumza katika mkutano huo mbali na kumpongeza Naibu Waziri Nyongo kwa kutatua mgogoro huo, aliwataka wananchi kufanya kazi kwa bidii huku wakilinda amani ya nchi.
Naye Mkurugenzi wa Kampuni ya Henan Afro-Asia Geo Engineering Co. Limited, Zhang Jiangho mbali na kuishukuru Serikali kupitia Wizara ya Madini kwa kutatua mgogoro huo  uliodumu kwa muda mrefu, aliahidi kushirikiana na wananchi wa kijiji cha Mwakitolyo kwa kuboresha  huduma za jamii na kulipa kodi na tozo mbalimbali za Serikali.


Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo akizungumza na wananchi wa kijiji cha Mwakitolyo kilichopo Wilayani Shinyanga Vijijini mkoani Shinyanga (hawapo pichani) kwenye mkutano wa hadhara uliolenga kutatua mgogoro kati yao na mwekezaji ambaye ni kampuni ya Henan Afro-Asia Geo Engineering Co. Limited tarehe 03 Aprili, 2019. 

Kutoka kushoto mbele, Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Jasinta Mboneko na Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo wakinukuu kero mbalimbali zilizokuwa zinawasilishwa na wananchi wa kijiji cha Mwakitolyo kilichopo Wilayani Shinyanga Vijijini mkoani Shinyanga (hawapo pichani) kwenye mkutano wa hadhara. 

Mmoja wa wananchi wa kijiji cha Mwakitolyo kilichopo Wilayani Shinyanga Vijijini mkoani Shinyanga  akiwasilisha kero yake kwa Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (hayupo pichani) kwenye mkutano wa hadhara. 

Sehemu ya wananchi wa kijiji cha Mwakitolyo kilichopo Wilayani Shinyanga Vijijini mkoani Shinyanga wakifuatilia ufafanuzi  uliokuwa unatolewa na Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (hayupo pichani) kwenye mkutano wa hadhara. 

Mbunge wa Solwa, Ahmed Salum akifafanua jambo kwa wananchi wa kijiji cha Mwakitolyo (hawapo pichani)