Na Nuru Mwasampeta
Kufuatia ziara ya Mhe.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim
Majaliwa aliyoifanya hivi karibuni
katika eneo la Ihumwa ambako ujenzi wa Mji wa Serikali unaendelea na kubaini uhaba wa kokoto katika ujenzi huo, leo Disemba 30, Naibu Waziri wa Madini
Doto Biteko akifuatana na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi Ajira na
Vijana Anthony Mavunde wamefanya ziara ya kushtukiza kwenye maeneo yanayochimba
kokoto hizo na kubaini madudu.
Naibu Mawaziri hao wamebaini
machimbo ya kokoto yakiwa yamefungwa kwa madai kuwa wafanyakazi wako likizo, zikiwemo
mashine za kusagia mawe hayo zikiwa zimeharibika
kwa takribani miezi mitatu na hivyo kupelekea uzalishaji kusimama.
Akizungumza katika
eneo hilo la machimbo, Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko amesema anashangazwa
kuona kuwa watumishi katika mgodi wa kokoto wanakwenda likizo wakati mahitaji
ya kokoto ni makubwa na soko la uhakika.
“Mmechukua zabuni kwa ajili ya kusambaza kokoto kutoka kwa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), Shirika la
Nyumba la Taifa (NHC),na kampuni ya
MZINGA wenye uhitaji mkubwa kwa ajili ya ujenzi wa mji wa Serikali unaoendelea
halafu mnadai mko likizo,?” amehoji Biteko.
Akizungumza kwa njia ya simu na Mkurugenzi wa Kampuni ya
Laroy Aggregate Co. Ltd , Biteko amemtaka mkurugenzi huyo aliyefahamika kwa jina la Joel
Mchovu kuhakikisha kuwa, ifikapo Januari
2, 2019 kokoto ziwe zimezalishwa na kusambazwa kwa wahitaji kama
walivyokubaliana ili ujenzi uendelee kwa kasi iliyokusudiwa.
Aidha, amewataka
watendaji hao kufanya kazi kwa juhudi na weledi mkubwa ili kuzalisha kiasi
kinachotosheleza mahitaji vinginevyo oda zitahamishwa na kupewa kampuni za
zinazozalisha kokoto zilizopo Chalinze ambazo zinaonesha uwezo mkubwa katika uzalishaji wa kokoto.
“Mfahamu kwamba
endapo tutatoa oda kwa watu wa Chalinze maana halisi ya ujenzi wa mji wa
Serikali kwa watu wa Dodoma haitakuwepo kwani hamtanufaika na ujenzi huu,” amesisitiza
Biteko.
Biteko amewataka
wananchi wa Dodoma kutambua kuwa, ujenzi wa mji wa Dodoma ni fursa kwao ya kuweza
kujikwamua kiuchumi na kuboresha maisha yao binafsi hivyo, wanapaswa kuwajibika
ili kupata manufaa hayo. “Fursa kubwa imepatikana na soko la uhakika lipo
nitawashangaa kuona kuwa mnapoteza fursa hii,” amesisitiza.
Naye, Fundi wa Mitambo
ya kuchoronga mawe katika mgodi wa WADI, Gao Peng, amesema kuwa, kampuni hiyo
iko katika hatua za kutengeneza mashine iliyoharibika ili kuwawezesha kuendelea
na uzalishaji wa kokoto hizo na kueleza kwamba mashine hiyo imeharibika kwa
takribani kipindi cha miezi mitatu sasa
na hivyo kufanya uzalishaji wa kokoto hizo kusimama.
Kwa upande wake,
Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Vijana Anthony Mavunde,
amesema anajisikia vibaya kuona kazi katika maeneo ya machimbo hazifanyiki na
kuwataka wananchi wanaofanya shughuli hizo kuongeza nguvu, weledi na ufanisi
ili waweze kunufaika.
“Dodoma tumejaliwa
kuwa na mawe mengi ya kuzalisha kokoto na madini mengine ya ujenzi, mahitaji ni
makubwa kutokana na kasi ya ujenzi iliyopo lakini bado wana Dodoma mmelala,”
amesema Mavunde.
Kwa upande wake,
Afisa Madini wa Mkoa wa Dodoma, Mhandisi Jonas Mwano amekiri kuwepo kwa leseni
hai za uchimbaji wa madini ya kokoto 75 katika mji wa Chigongwe na leseni 66
zimekwisha tolewa kwa waliowasilisha maombi ya leseni hizo na hivyo kuwataka
wamiliki wa leseni hizo kuhakikisha wanazifanyia kazi leseni zao vinginevyo
zitagawiwa kwa watu wengine.
Aidha, Mwano amekiri
kuwa, awali wamiliki wengi wa leseni za madini ya kokoto walikuwa hawazalishi
vya kutosha kwa madai kuwa soko lilikuwa adimu lakini sasa soko ni la uhakika
na hivyo kuwataka wazalishe kokoto za kutosha ili kutoiangusha Serikali.