Thursday, June 14, 2018

Tanzania na Australia kuendeleza ushirikiano sekta ya madini


Na Veronica Simba, Dodoma

Balozi wa Australia nchini Tanzania, Alison Chartres, amemtembelea Waziri wa Madini Angellah Kairuki na kuzungumzia ushirikiano wa nchi hizo katika sekta ya madini.

Akiongoza Ujumbe wa Umoja wa Kampuni za Madini na Nishati za Australia, Juni 13, 2018 Makao Makuu ya Wizara Dodoma; Balozi Chartres alimweleza Waziri Kairuki kuwa nchi yake inapenda kuendelea kushirikiana na Tanzania katika sekta mbalimbali, ikiwemo sekta ya madini.

Kwa upande wake, Waziri Kairuki; pamoja na kumhakikishia Balozi huyo kuwa Tanzania itaendelea kutoa ushirikiano kadri inavyotakiwa kwa Australia, lakini pia alitumia fursa hiyo kuwakaribisha wawekezaji mbalimbali wa nchi hiyo, waendelee kuja kuwekeza katika sekta ya madini nchini na katika sekta nyingine pia.

“Ni matumaini yetu kuwa, nchi zetu zitaendeleza ushirikiano katika sekta ya madini na sekta nyingine mbalimbali kama ambavyo tumekuwa tukifanya,” alisisitiza Waziri.

Aidha, Waziri Kairuki aliuelekeza Ujumbe huo kutoka Australia, kuwasilisha mapendekezo rasmi kwa Serikali ikiwa kuna eneo lolote katika sekta ya madini, wanalodhani linahitaji kufanyiwa marekebisho ili wataalam wayapitie na kuona endapo yana tija kwa pande zote mbili, na kisha kufikia maamuzi.

“Niweke wazi kuwa, Serikali ya Tanzania imedhamiria kuhakikisha kuwa sekta ya madini inawanufaisha wananchi wake ipasavyo. Kwa hiyo, kila tutakapobaini kuwa liko eneo ambalo halituridhishi, hatutasita kufanya marekebisho kwa manufaa ya Watanzania wote.”

Kikao hicho pia kilihudhuriwa na Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo, Kamishna wa Madini Tanzania Mhandisi David Mulabwa pamoja na maafisa mbalimbali waandamizi kutoka Wizara ya Madini na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.


Waziri wa Madini Angellah Kairuki (katikati-waliokaa), Balozi wa Australia nchini Tanzania, Alison Chartres (kushoto-waliokaa) na Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo (kulia-waliokaa); wakiwa katika picha ya pamoja na Ujumbe wa Umoja wa Kampuni za Madini na Nishati za Australia na wataalam wa sekta ya madini Tanzania,  baada ya kikao baina ya pande hizo mbili kujadili ushirikiano katika sekta ya madini. Kikao kilifanyika Juni 13, 2018 Makao Makuu ya Wizara Dodoma.


Waziri wa Madini Angellah Kairuki (katikati), akizungumza na Balozi wa Australia nchini Tanzania, Alison Chartres (kushoto), wakati wa kikao kilichofanyika Juni 13, 2018 Makao Makuu ya Wizara Dodoma. Kikao hicho kilijadili ushirikiano wa Tanzania na Australia katika sekta ya madini. Kulia ni Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo. 


Waziri wa Madini Angellah Kairuki (katikati), akiongoza kikao baina ya wataalam wa sekta ya madini Tanzania (kulia) na Ujumbe wa Umoja wa Kampuni za Madini na Nishati za Australia, ulioongozwa na Balozi wake nchini, Alison Chartres (kushoto). Kikao hicho kilijadili ushirikiano wa Tanzania na Australia katika sekta ya madini na kilifanyika Juni 13, 2018 Makao Makuu ya Wizara jijini Dodoma.


Kutoka kushoto ni Kamishna wa Madini Tanzania, Mhandisi David Mulabwa, Afisa Sheria Mwandamizi Juliet Moshi na Mkaguzi wa Migodi kutoka Wizara ya Madini, Mhandisi Assa Mwakilembe, wakijadiliana jambo, muda mfupi baada ya kikao cha Waziri wa Madini Angellah Kairuki na Ujumbe wa Umoja wa Kampuni za Madini na Nishati za Australia, ulioongozwa na Balozi wake nchini, Alison Chartres (kushoto), Makao Makuu ya Wizara jijini Dodoma, Juni 13, 2018.

No comments:

Post a Comment