Monday, April 1, 2019

Naibu Waziri Nyongo abaini udanganyifu madini Kahama


Aelekeza soko la madini kuanzishwa mara moja………

Na Greyson Mwase, Kahama

Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo ameelekeza soko la madini katika mkoa wa kimadini wa Kahama ikiwa ni pamoja na maeneo mengine ya Chunya, Musoma, Singida kuanzishwa mara moja ili kudhibiti utoroshwaji wa madini unaopelekea Serikali kukosa mapato yake.

Naibu Waziri Nyongo ameyasema hayo leo tarehe 31 Machi, 2019 katika mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika mjini Kahama. Wengine waliokuwepo katika mkutano huo ni pamoja na Kamishna Msaidizi, Uendelezaji Migodi na Madini wa Wizara ya Madini,  Ali Saidi Ali, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Kimadini wa Kahama, Andrea Fabian pamoja na wataalam kutoka Tume ya Madini.

Alisema kuwa, mara baada ya kufanya ziara yake ya siku moja katika Wilaya ya Kahama, alibaini kumekuwepo na udanganyifu mkubwa katika shughuli za uchenjuaji wa madini huku akitolea mfano wa kampuni ya Busami inayojihusisha na uchenjuaji wa madini ya dhahabu.

Alisisitiza kuwa, alibaini kumekuwepo na udanganyifu kwenye uzito na kiwango halisi cha dhahabu kwenye madini yaliyopatikana hali inayopelekea Serikali kukosa mapato yake stahiki.

“Kwa mfano katika mtambo wa kuchenjua dhahabu unaomilikiwa na kampuni ya Busami tumebaini kuna udanganyifu kwenye uchenjuaji, jana baada ya kufika na kuona namna uchenjuaji wa madini unavyofanyika na kuelekeza wataalam wa madini kuchenjua upya mchanga uliokuwepo kwenye maji yaliyohifadhiwa, tulibaini kuna madini," alisema Nyongo

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri Nyongo alisimamisha shughuli za uchenjuaji katika kampuni ya Busami na kutaka hatua za kisheria kuchukuliwa dhidi ya mmiliki wake.

Wakati huo huo, Naibu Waziri Nyongo alielekeza wamiliki wote wa mitambo  ya kuchenjulia madini ya dhahabu nchini kuhakikisha wanakuwa na mizani na mashine maalum za kupimia madini ya dhahabu zilizoidhinishwa na Wakala wa Vipimo Tanzania, na biashara ya madini kufanyika katika masoko ya madini yaliyoanzishwa na kusisitiza kuwa lazima madini yajulikane yanapopelekwa na Ofisi za Madini Nchini kuhakikisha zinatuza kumbukumbu sahihi.

Wakati huo huo Naibu Waziri Nyongo aliagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila pamoja na Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Profesa Shukrani Manya kufuatilia iwapo hatua za kisheria zimechukuliwa dhidi ya kampuni inayojihusisha na uchenjuaji wa madini ya dhahabu Wilayani Kahama ya Jema baada ya kukamatwa ikifanya udanganyifu hivi karibuni.

Kufuatia ziara ya Naibu Waziri Nyongo soko la madini kufunguliwa Kahama


Na Greyson Mwase, Kahama

Ofisi ya Afisa Madini Mkazi, Mkoa wa Kimadini wa Kahama inatarajia kuanzisha soko la madini mapema ikiwa ni moja ya mikakati ya Serikali kupitia Wizara ya Madini katika kudhibiti utoroshwaji wa madini.

Hatua hiyo imekuja kufuatia ziara ya Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo aliyoifanya mapema leo tarehe 30 Machi, 2019 katika Wilaya ya Kahama lengo likiwa ni kukagua shughuli za uchimbaji na uchenjuaji wa madini ya dhahabu, kusikiliza na kutatua kero za wachimbaji wa madini.

Katika ziara hiyo, Naibu Waziri Nyongo aliambatana na Kamishna Msaidizi- Uendelezaji Migodi na Madini wa Wizara ya Madini, Ali Said Ali wataalam kutoka Tume ya Madini pamoja na wawakilishi wa vyombo vya ulinzi na usalama.

Mara baada ya kufanya ziara katika baadhi  ya mitambo ya kuchenjua dhahabu, Nyongo alifanya kikao na wamiliki wa mitambo hiyo na kusikiliza kero mbalimbali pamoja na kuzitatua.

Mara baada ya kusikiliza kero husika ikiwa ni pamoja na ya kutokuwepo kwa soko la madini katika Wilaya ya Kahama, Naibu Waziri Nyongo alimwelekeza Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Kimadini wa Kahama,  Adrea Fabian kuhakikisha sehemu ya ofisi yake inatumika kama soko la madini ya dhahabu ambapo wauzaji na wanunuzi watakuwa wanafanya biashara huku serikali ikipata mapato yake, kauli ambayo ilipokelewa kwa shangwe na wafanyabiashara wa madini ya dhahabu.

Aliendelea kusema kuwa kutokuwepo kwa soko la madini katika Wilaya ya Kahama, kunachochea utoroshwaji wa madini ya dhahabu kwakuwa inakuwa vigumu kwa wauzaji wa madini hayo kusafiri umbali mrefu hadi Geita kwa ajili ya kwenda kuuza madini hayo.

“Hapa tunataka kuhakikisha biashara ya madini inafanyika hapa hapa ili kuwarahisishia wafanyabiashara wa madini ya dhahabu huku Serikali ikipata mapato yake,” alisisitiza Naibu Waziri Nyongo.

Katika hatua nyingine, Nyongo aliutaka uongozi wa Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Kimadini wa Kahama kushirikisha mamlaka nyingine za Serikali kama vile Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, Vyombo vya Ulinzi na Usalama, Mabenki na soko kuanza mara moja.

Aidha, Naibu Waziri Nyongo aliwataka wamiliki wa mitambo ya kuchenjua dhahabu kuunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Dkt. John Pombe Magufuli katika kulinda rasilimali za madini kwa kutoa ushirikiano kwa Wizara ya Madini.

Wakizungumza katika nyakati tofauti wamiliki wa mitambo ya kuchenjulia dhahabu walioshiriki katika kikao hicho mbali na kumpongeza Naibu Waziri Nyongo wamesema kuwa uwepo wa soko hilo utawarahisishia sana biashara ya madini kutokana na kuepukana na matapeli huku serikali ikipata mapato yake stahiki.

Walisema kabla ya uamuzi huo wamekuwa wakisafirisha madini hadi Geita kwa ajili ya kuuza hali inayopelekea baadhi yao kuuza kwa watu wasio waaminifu.


Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (wa pili kulia) akikagua mashine ya kupima dhahabu katika kampuni ya Busami iliyopo Wilayani Kahama Mkoani Shinyanga ikiwa ni sehemu ya ziara yake katika mkoa huo ya kukagua shughuli za uchimbaji na uchenjuaji wa madini, kusikiliza na kutatua kero za wachimbaji wa madini tarehe 30 Machi, 2019. 

Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (kushoto) akijadiliana jambo na Kamishna Msaidizi- Uendelezaji Migodi na Madini wa Wizara ya Madini, Ali Said Ali (katikati) katika kampuni ya Busami iliyopo Wilayani Kahama Mkoani Shinyanga. 

Kutoka kulia Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo na Kamishna Msaidizi- Uendelezaji Migodi na Madini wa Wizara ya Madini, Ali Said Ali wakisikiliza kero za wamiliki wa mitambo ya kuchenjulia dhahabu (hawapo pichani) kupitia mkutano maalum uliofanyika Wilayani Kahama Mkoani Shinyanga.

Hatukunufaika na madini, haikuwa ajenda ya Kitaifa–Spika Ndugai


Na Asteria Muhozya,

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Ndugani, amesema awali, Taifa halikunufaika na rasilimali madini kwa kuwa sekta hiyo haikuwa ajenda ya Kitaifa.

“Madini yaliachwa kwa wabunge ambao rasilimali hiyo inapatikana kwenye maeneo yao, haikuwa ajenda ya taifa, wengine walizungumzia zaidi masuala yanayowagusa kama korosho, pamba na mambo mengine, nashukuru tumefanya mabadiliko na sasa matokeo yameanza kuonekana,” amesema Spika Ndugai.

Amesema  kwa mwelekeo wa sasa, serikali imefika mahali ambapo manufaa ya rasilimali hiyo yameanza kuonekana kutokana na  mageuzi makubwa yaliyofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Magufuli na kumpongeza kutokana na namna anavyohakikisha rasilimali madini inalinufaisha taifa, na kuongeza, “kilio cha watanzania cha kutokunufaika na madini kimepata mwenyewe, Rais Magufuli amefanya uthubutu”.

Spika Ndugai ameyasema hayo Machi 30, 2019, wakati akifungua Semina kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini na baadhi ya Wenyeviti wa Kamati nyingine za bunge wanaohudhuria semina ya siku mbili jijini Dodoma, iliyoandaliwa na Wizara ya Madini kwa lengo la kutoa elimu ili kupata uelewa wa sekta ya madini.

Amesema, awali, ikijulikana kama Wizara ya Nishati na Madini ilikuwa ni kazi hata kwa bunge hilo kupitisha Bajeti ya wizara hiyo kutokana na kwamba, sekta zote mbili nishati na madini   hazikuwa zikilinufaisha taifa na kusema, “ kulikuwa na kutokuridhika na sekta zote na hususan madini, kama taifa tulikuwa hatupati haki yetu tuliyoistahili”.

Kufuatia hali hiyo, Spika Ndugai amewataka Wabunge  na wananchi kuunga mkono jitihada zinazofanywa na Rais Magufuli  kwa kuwa  mchango wa sekta ya madini katika uchumi wa taifa utasaidia kusogeza mbele maendeleo ya taifa na watu wake.

Aidha, amewaasa viongozi wote waliobeba dhamana ya kusimamia sekta husika kuhakikisha wanaichukulia dhamana waliyopewa kwa uzito wa kipekee  ili kuliwezesha taifa kufanana na nchi nyingine ambazo zimeendelea kutokana na rasilimali madini.

Pia, amepongeza mabadiliko yanayofanywa na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) na kueleza kwamba anafurahi kusikia STAMICO mpya tofauti na ilivyokuwa awali.

Akizungumzia Kamati mbili zilizoundwa na bunge kuchunguza biashara ya madini ya Tanzanite na Almasi, amesema kuwa, kamati hizo zilifanya kazi nzuri na kwamba  bunge litaendelea kuishauri serikali  ili kuhakikisha sekta  ya madini inazidi kuchangia zaidi katika uchumi wa taifa.

Ameongeza kuwa, ripoti hizo zilipokelewa vizuri na serikali na kwamba juhudi zilizochukuliwa zimewezesha uanzishwaji wa masoko ya madini huku STAMICO ikifanya mabadiliko makubwa.

Kwa upande wake, Waziri wa Madini Doto Biteko akizungumza katika semina hiyo, amesema  sekta ya madini ni muhimu kwa uchumi wa taifa la Tanzania na kueleza kuwa, mchango wa taifa umeendelea kuongezeka mwaka hadi mwaka na kueleza kuwa, mwaka 2017, sekta hiyo ilichangia asilimia 4.8 kwenye pato la taifa ikilinganishwa na asilimia 4.0 mwaka 2015.

Akizungumzia ukuaji wa sekta hiyo amesema umeongeza kwa kasi kutoka asilimia 9.0 mwaka 2015 kufikia 17.5 mwaka 2017, na kusema mafanikio hayo yametokana na juhudi za serikali kuhakikisha sekta hiyo inachangia zaidi  ili kufikia lengo la asilimia 10 ya mchango wake ifikapo mwaka 2025.

Akizungumzia marekebisho ya Sheria ya Madini yaliyofanywa mwaka 2017,  na usimamizi wa Rasilimali Madini, amesema umewezesha ongezeko la makusanyo ya maduhuli yatokanayo na shughuli za madini kutoka Shilingi bilioni 194 iliyotarajiwa kukusanywa mwaka 2017/18 hadi shilingi bilioni 301.29 sawa na asilimia 154.999 ya lengo la makusanyo kwa mwaka huo.

“Mhe. Spika, mwenendo wa ukusanyaji maduhuli kwenye sekta hii kwa mwaka 2018/19 ni wa kuridhisha ambapo hadi Februari kiasi cha shilingi 218,650,392 kimekusanywa hii ikiwa ni sawa na asilimia 105.6,” amesema Waziri Biteko.

Ameeleza kuwa, miongoni mwa sababu zilizopelekea mafanikio hayo ni pamoja na kuongezeka kwa mrabaha  kwa baadhi ya madini, kuanzisha kodi  mpya  ya ukaguzi ya asilimia 1; kuimarisha udhibiti wa utoroshaji wa madini; na kwa kushirikiana na wananchi  na vyombo vya ulinzi na usalama na kuzuia usafirishaji wa madini ghafi ya nje ya nchi ili  viwanda vya kusafishia na kuongeza ubora wa madini vijengwe  nchini.

Akizungumzia usimamizi wa shughuli za madini ya Tanzanite baada ya kukamilika kwa ukuta unaozunguka machimbo ya tanzanite Mirerani amesema udhibiti wa madini hayo umeimarika  na kusababisha kuongezeka kwa ukusanyaji wa maduhuli yatokanayo na madini hayo.

Ameongeza kuwa, kufuatia juhudi hizo, ukusanyaji wa maduhuli kutokana na uzalishaji wa tanzanite kwa wachimbaji wa Wadogo na Kati uliongezeka hadi kufikia shilingi 1,436, 427, 228.99 kwa mwaka  2018, ikilinganishwa na  shilingi 71,861,970 kwa mwaka 2016.

“Uzalishaji umeongezeka kutoka migodi midogo na ya kati hadi kufikia kilo 781.204 kwa mwaka 2018 ikilinganishwa na kilo 147.7  zilizoripotiwa  kwa mwaka 2017 na kilo 164.6 za mwaka 2016,” amesema Waziri Biteko.

Naye, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini Dustan Kitandula, ameishukuru Wizara kwa kuandaa semina hiyo kwa wabunge na kueleza kuwa, kamati hiyo itaendelea kupata uelewa kuhusu sekta ya madini.
Mbali na wabunge, wengine wanaoshiriki semina hiyo ni Wenyeviti wa Bodi za taasisi za zilizo chini ya wizara, Wataalam kutoka wizarani na taasisi zake.


Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Ndugai akieleza jambo wakati akifungua Semina kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini( hawapo pichani). 

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Ndugai (wa pili kulia) akiteta jambo na Waziri wa Madini Doto Biteko (wa pili kushoto)na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Dustan Kitandula (wa kwanza kulia). Wa kwanza kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Prof. Simon Msanjila. 

Baadhi ya Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini wakifuatilia mada mbalimbali zilizowasilishwa na wataalam wa Wizara ya Madini. 

Baadhi ya Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini wakifuatilia mada mbalimbali zilizowasilishwa na wataalam wa Wizara ya Madini. 

Baadhi ya Watumishi wa Wizara ya Madini, Wenyeviti wa Bodi ya Taasisi  chini ya wizara na Wataalam kutoka wizarani na  taasisi zake wakifuatilia hotuba ya ufunguzi wa Semina iliyotolewa na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai kwa  Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini na baadhi ya wabunge wa kamati nyingine (hayupo pichani). 

Baadhi ya Watumishi wa Wizara ya Madini, Wenyeviti wa Bodi ya Taasisi  chini ya wizara na Wataalam kutoka wizarani na  taasisi zake wakifuatilia hotuba ya ufunguzi wa Semina iliyotolewa na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai kwa  Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini na baadhi ya wabunge wa kamati nyingine (hayupo pichani).

Friday, March 29, 2019

Waziri Biteko azindua Bodi ya GST


v AITAKA KUIWEZESHA GST KURAHISISHA MAISHA YA WACHIMBAJI

Asteria Muhozya na Samwel Mtuwa, Dodoma

Bodi ya Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST), imetakiwa kuiwezesha taasisi hiyo kurahisisha maisha ya Wachimbaji Wadogo, wa Kati na Wakubwa kwa kuhakikisha wanapata taarifa za tafiti zinazofanywa na taasisi hiyo.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Madini Doto Biteko wakati akizundua Bodi ya GST na kueleza kuwa, shughuli za utafiti ni moja ya maeneo muhimu katika sekta ya madini kutokana na kutoa uhakika kwa wachimbaji na hivyo kukidhi matarajio ya wadau.

Pia, ameitaka bodi kuiwezesha taasisi hiyo kutoa ubunifu mpya utakaowezesha taasisi hiyo kuongeza mapato kwa serikali kutokana na shughuli na huduma zinazotolewa na GST.

Katika hatua nyingine, Waziri Biteko ameitaka bodi hiyo kuhakikisha GST inapata Ithibati ya maabara yake ikiwemo kutangaza huduma zinazotolewa na maabara hiyo ili kuwawezesha wadau kuifahamu na kuitumia.

Aidha, ameitaka bodi husika kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia sera, sheria na taratibu zilizowekwa na kueleza kwamba, taasisi hiyo inao watendaji wazuri wa kuiwezesha kutekeleza majukumu yake kiamilifu na kutumia fursa hiyo kumpongeza Kaimu Mtendaji Mkuu wa GST Yokberth Myumbilwa, kwa kusimamia vema utendaji wa GST.

Naye, Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo amesema taasisi hiyo ni kitovu cha sekta ya madini nchini na kwamba ndiyo imeshikilia mstakabali wa wachimbaji wadogo, wa kati na wakubwa.

Ameongeza kuwa, bado yapo majukumu ya taasisi hiyo ambayo hayajafanikiwa na hivyo kuitaka bodi hiyo chini ya Prof. Ikungula kuhakikisha yanafanikiwa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi hiyo Prof. Justinian Ikingura amesema bodi hiyo inatambua umuhimu wa rasilimali madini katika kuchangia pato na kukuza uchumi wa taifa ikiwemo kutambua nia na lengo la Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Magufuli.

Amesema ili kufikia lengo hilo, ni muhimu GST ikawezeshwa ipasavyo kupitia wizara ili iongeze kasi na tija zaidi katika kutekeleza majukumu yake, hususan katika maeneo ya kufanya utafiti na kukusanya taarifa muhimu za kijiosayansi za kubaini maeneo yenye miamba yenye vishiria vyakuwepo madini ya kimkakati yanayohitajika zaidi katika matumizi ya teknolojia ya viwanda vya kielekitroniki, zana za utafiti wa mawasala ya anga na matumizi maalum katika viwanda vingine, ili kuvutia uwekezaji wa ndani na nje ya nchini katika maeneo hayo.

Kwa mfano madini lithium, cobalt na palladium yanazidi kupata umuhimu wa pekee katika matumizi ya viwanda vya kimkakati. Hivi majuzi takriba wiki moja iliyopita bei ya Palladium ilifikia kiasi cha dola za kimarekani 1,600 kwa wakia na kuzidi hata dhahabu ambayo ikiwa karibu dola 1,300 kwa wakia moja. Lakini si wengi wanatambua madini ya Palladium ambayo yako katika kundi la metali za Platinum, yaani Platinum Group Metals (PGM),” amesisitiza Prof. Ikingura.

Ameongeza kuwa, eneo jingine ni uboreshaji wa huduma za maabara za uchunguzi na upimaji wa miamba na madini yake ili zikidhi viwango vya kimataifa, na hivyo kuvutia wawekezaji katika sekta ya madini kutumia zaidi maabara za ndani ya nchini badala ya kupeleka sampuli katika maabara za nje ya nchi, na hivyo kupoteza fedha za kigeni.

Vilevile, amesema ipo haja ya kuboresha na kuongeza thamani taarifa za jiofikizia na jiokemia zilizo katika hifadhi au kanzidata ya GST ili ziweze kuwa na thamani kubwa zaidi  kwa taifa na kwa wawekezaji katika sekta ya madini, suala ambalo  litaiweesha GST kuongeza maduhuli ya serikali kupitia wizara.

Mbali ya Mwenyekiti, wajumbe wa bodi hiyo ni Abdulkarim Hamisi Mruma, Emanuel Mpawe Tutuba, Bibi Bertha Ricky Sambo, Shukrani Manya, David R. Mulabwa na Bibi Monica Otaru.

Bodi hiyo imezinduliwa Machi 27, 2019 Makao Makuu ya GST, jijini Dodoma.

Waziri wa Madini Doto Biteko,  akimkabidhi  kitendea kazi mmoja wa wajumbe wa Bodi ya GST , Kamishna wa Madini, David Mulabwa wakati wa uzinduzi wa bodi. Anayeshuhudia kulia ni Mwenyekiti wa Kamati  ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Dustan  Kitandula.

Baadhi ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Wajumbe wa  Bodi ya Taasisi ya Jiolojia na Utafiti  wa  Madini Tanzania (GST), Watendaji wa wizara  pamoja na watumishi  mbalimbali kutoka  GST wakifuatilia hotuba ya Waziri wa Madini Doto Biteko (hayupo pichani) wakati wa uzinduzi wa Bodi ya GST uliofanyika jijini Dodoma tarehe 27/3/2019.

Waliokaa kutoka kushoto ni  Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya  Bunge ya Nishati na Madini  Dustan  Kitandula, Waziri wa Madini Doto Biteko , Mwenyekiti wa Bodi ya GST Prof. Justinian Ikingula, na Naibu waziri wa Madini Stanslaus Nyongo. Wengine katika picha waliosimama ni Wajumbe wa Bodi ya GST na baadhi ya Wajumbe wa Menejimenti ya GST. 

Waziri wa Madini Doto Biteko akimkabidhi moja a kitendea kazi mjumbe wa Bodi ya GST Prof. Shukran Manya wakati wa Uzinduzi wa Bodi ya GST uliofanyika tarehe 27/3/2019 katika ukumbi wa mikutano wa wizara , pembeni anayeshuhudia makabidhiano hayo ni mwenyekiti wa Bodi hiyo Prof. Justinian Ikingula.

Waziri wa Madini Doto Biteko (kushoto) akizungumza na jambo wakati wa uzinduzi wa bodi ya GST . Kulia anayefuatilia hayo ni Mwenyekiti wa Bodi ya GST Prof. Justinian Ikingula.

Thursday, March 28, 2019

Waziri Mkuu atembelea Mji wa Serikali


Na Greyson Mwase,

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, amewapongeza wakandarasi kwa kukamilisha ujenzi wa majengo ya ofisi za Serikali katika eneo la Ihumwa jijini Dodoma.

Ametoa pongezi hizo leo tarehe 27 Machi, 2019 mara baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi huo na kuonesha kuridhishwa na hatua iliyofikiwa.

“Nimefurahishwa sana na wakandarasi waliochukua zabuni za kujenga majengo ya ofisi hizi, hivyo ninawaomba Wakala wa Ujenzi Tanzania (TBA) watoe vyeti kwenye majengo ambayo yamekamilika kwa asilimia mia ili waanze kutumia majengo hayo kama ilivyokusudiwa,” alisema Majaliwa.

Katika  hatua nyingine, Waziri Mkuu Majaliwa  hakuridhishwa  na ubora  wa milango iliyopachikwa kwenye jengo la Ofisi ya Makamu wa Rais pamoja na Jengo la Wizara ya Fedha na kuagiza milango hiyo kubadilishwa.

Pia, Majaliwa ameliagiza Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kupeleka umeme mkubwa katika eneo hilo kwa wakati ili majengo yakamilike kwa asilimia mia na kufikia azma ya Serikali ya kuhamia katika mji wa Serikali baada ya ofisi hizo kufunguliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Mgufuli.

Kwa upande wake Waziri wa Fedha, Philip Mpango, amesema mradi wa ujenzi wa nyumba hizo umezalisha ajira kubwa kwa vijana kutokana na kuajiri takribani watu 1141 walioshiriki katika ujenzi huo.

Akizungumzia hatua iliyofikiwa katika ujenzi wa Jengo la Wizara ya Madini,   Naibu Waziri wa  Madini, Stanslaus Nyongo, amesema jengo la Wizara limekamilika kwa asilimia 99, na kubainisha kuwa, mkandarasi yupo katika hatua za mwisho ili aweze kukabidhi jengo hilo.


Sehemu ya Jengo la Wizara ya Madini lililopo katika eneo la mji wa Serikali Ihumwa jijini Dodoma ambalo mpaka sasa limekamilika kwa asilimia 99.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa pamoja na Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (katikati mbele) wakipata maelezo ya hatua iliyofikiwa ya ujenzi wa Jengo la Wizara ya Madini kwenye mji wa Serikali, Ihumwa jijini Dodoma kutoka kwa msimamizi wa mradi wa ujenzi huo (kulia).


Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (wa tatu kutoka kushoto) akiwa pamoja na baadhi ya viongozi waandamizi wa Serikali wakati wakimsubiri  Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kwenye jengo la Wizara ya Madini  kabla ya kuanza kwa ukaguzi kwenye jengo hilo.

Wednesday, March 27, 2019

Waziri Biteko afanya mazungumzo na Kampuni ya PRNG Minerals


Na Issa Mtuwa,

Waziri wa Madini  Doto Biteko amekutana na kufanya mazungumzo na Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya PRNG Minerals Ltd, ya  Marekani, Rocky Smith na Mkurugenzi wa Maendeleo wa Kampuni hiyo Lucas Stanfield ofisini kwake Jijini Dodoma. 

Watendaji hao wapo nchini kwa ziara ya kawaida ya kikazi ya siku tano  ambapo waliomba kukutana na Waziri wa Madini.

Pamoja na mambo mengine, kampuni hiyo inakusudia kuwasilisha taarifa juu ya hali na Maendeleo ya soko la dunia kwa Madini ya Rare Earth Elements na kuzungumzia hatua iliyofikiwa kwa ombi la leseni ya  uchimbaji  Mkubwa wa madini hayo.

Akizungumza katika kikao hicho, Waziri Biteko  amesema wizara iko tayari kuipokea kampuni husika nchini baada ya kukamilika kwa taratibu kwa mujibu wa sheria.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu Rocky Smith, amesema kuwa, amefurahishwa na  ushirikiano unaooneshwa na wizara na kuahidi kuanza shughuli za uchimbaji mara baada ya kukamilika kwa taratibu.


Waziri wa Madini Doto Biteko akimsikiliza Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya PRNG Minerals Ltd kutoka Marekani Rocky Smith kushoto kwa Waziri. Smith alimtembelea Waziri ofisini kwake jijini Dodoma kwa mazungumzo akiwa ameambatana na Mkurungenzi wa Maendeleo wa Kampuni hiyo Lucas Stanfield wa kwanza kulia, na wa kwanza kushoto ni Mkurugenzi wa huduma za sheria Wizara ya Madini Edwin Igenge.
Waziri wa Madini Doto Biteko akimsikiliza Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya PRNG Minerals Ltd kutoka Marekani Rocky Smith kushoto kwa Waziri. Smith alimtembelea Waziri ofisini kwake jijini Dodoma kwa mazungumzo, wa kwanza kushoto ni Ali Ali, Kamishna Msaidizi Uendelezaji Migodi na Madini Wizara ya Madini, anaefuatia ni Mkurugenzi wa Huduma za Sheria Wizara ya Madini Edwin Igenge.

Kituo cha Madini na Jiosayansi Kunduchi, kinavyowanufaisha Watanzania


Na Nuru Mwasampeta,
TAARIFA za kijiolojia zinaonesha kuwa, Afrika ni bara lenye utajiri mkubwa wa rasilimali madini huku sehemu kubwa ya madini hayo yakiwa bado hayajaanza au yako kwenye hatua mbalimbali za uendelezaji.

Aidha, rasilimali za madini zilizopo barani Afrika hususani Tanzania, taarifa za kijiolojia zinadokeza kuwa yanaweza kuwa ni chanzo kikubwa cha kuharakisha maendeleo ya kiuchumi kwa Taifa na kijamii ikiwa kila mmoja aliyepewa jukumu la kuwajibika katika sekta ya madini atatumia utaalamu wake, weledi na ufanisi ili kupata matokeo chanya.

Ndiyo maana Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Dkt.John Magufuli kwa kutambua utajiri mkubwa wa madini tuliyonayo hapa nchini yakiwemo ya tanzanite, almasi,dhahabu, chuma au vito ameendelea kutoa hamasa kwa viongozi wenye mamlaka ya kuyasimamia madini kuongeza ubunifu na usimamizi wenye tija.

Kwa kutambua umuhimu wa madini katika kuharakisha maendeleo ya nchi, Wizara ya Madini kupitia viongozi wake kila kukicha wamekuwa wakifanya juhudi mbalimbali ili kutumia fursa zilizopo ndani na nje ya nchi kuleta tija kubwa kwenye sekta ya uchimbaji wa madini, uongezaji wa thamani na usimamizi wa sekta kwa matokeo makubwa.

WAZIRI NYONGO

Hivi karibuni, Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo, ameshiriki katika kikao cha 39 cha kutathmini utendaji wa Kituo cha Madini na Jiosayansi cha Afrika (AMGC)) katika kutekeleza maazimio ya nchi wanachama kilichofanyika nchini Sudani Februari 18, mwaka huu.

Neno jiosayansi linamaanisha sayansi inayohusu Dunia ikihusisha masuala yote yanayohusisha elimu ya miamba kama vile utafutaji wa madini, uchimbaji, uchenjuaji pamoja na biashara ya madini.

Hivyo, AMGC ni kituo kinachoratibu masuala hayo kwa nchi mwanachama wa umoja huo katika Bara la Afrika.

Kituo hicho kilichoanzishwa na Kamisheni inayohusu masuala ya Kiuchumi katika Umoja wa Afrika (UNECA) kwa lengo la kusimamia na kuratibu shughuli zote zinazohusu sekta ya madini chini ya Mwamvuli wa Dira ya Afrika kuhusu Madini (AMV) ili kupelekea maendeleo endelevu kwa nchi wanachama pasipo kuathiri mazingira. 

Umoja huo ulianzishwa kwa mara ya kwanza mwaka 1977 ukijulikana kama Southern and Eastern African Mineral Centre (SEAMIC) ambapo shughuli zake zilikuwa zikifanyika katika jengo la Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini (GST) jijini Dodoma, kabla ya kuhamia katika ofisi zilizopo Kunduchi jijini Dar es Salaam. 

Gharama za ujenzi wa ofisi za kituo hicho zilitokana na michango ya nchi wanachama.

Aidha, kituo hicho kinafanya shughuli mbalimbali za madini ikiwa ni pamoja na kutoa mafunzo ya namna ya kukata na kuchenjua madini, kukata madini na kutengeneza bidhaa mbalimbali zitokanazo na madini, uchambuzi na huduma za ushauri katika maeneo tofautitofauti ya kimadini, pamoja na tafiti juu ya madhara yatokanayo na kemikali za kuchenjulia madini kwa mazingira. 

Kabla ya mkutano uliowahusisha mawaziri wenye dhamana na sekta ya madini, kulitanguliwa na mikutano mingine miwili iliyohusisha Bodi ya Wakurugenzi wa kituo hiki ni kikao kidogo zaidi wakiwa ni wasimamizi wa karibu wa kituo kikao cha pili kinawahusisha watendaji wakuu katika wizara zenye dhamana ya madini, ambacho baada ya kikao waliwasilisha taarifa za kikao katika mkutano wa Baraza la Mawaziri la nchi wanachama kwa ajili ya kutolea maamuzi.

Kuhudhuria katika mkutano huo, Naibu Waziri wa Madini Nyongo amesema, amejifunza namna sekta ya madini nchini Sudan ulivyojipanga katika kuikwamua Sudan kiuchumi kutokana na rasilimani madini. 

Ameendelea kueleza kuwa, nchi ya Sudan inazalisha madini ya dhahabu kwa wingi kwa kiasi cha tani 107 ukilinganisha na Tanzania inayofikisha kiasi cha takriban tani 50 kwa mwaka.

Nyongo anaeleza kuwa, kiasi cha tani 107 cha dhahabu kilichozalishwa nchini Sudan mwaka uliopita kiliuzwa nje ya nchi ambapo asilimia 90 ya madini hayo yalichimbwa na kuuzwa kutoka kwa wachimbaji wadogo. 

Waziri Nyongo amekiri kuwa, sekta ya uchimbaji mdogo inao uwezo mkubwa wa kuchangia katika pato la Taifa tofauti na fikra za wengi zilivyo.

Kwa upande wake Kamishna Msaidizi wa Madini anayeshughulikia uwajibikaji wa migodi katika kutoa huduma na unufaikaji wa wazawa, Torence Ngole amesema uwepo wa kituo hicho kwa Watanzania una manufaa makubwa kwa Watanzania hususani wachimbaji wadogo katika kujipatia ujuzi.

Lakini pia kituo hicho kina maabara kubwa inayotumika katika kuchunguza madini na kuyabainisha ambapo wachimbaji wanaweza kupeleka madini yao na kuwa na uhakika zaidi wa mali waliyonayo. 

Katika kupunguza migogoro katika kanda ya maziwa makuu kama vile Sudan na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na nchi zenye migogoro na vita, Ngole amebainisha uwepo wa mashine maalumu inayoyafanya uchunguzi wa madini na kubaini madini hayo yanachimbwa nchi gani. 

Amesema, ikibainika kuwa madini husika yanapatikana katika nchi zenye vita basi hayapewi kibali cha kuweza kuyauza na hivyo kuyanyima sifa ya kuuzika. 

Hiyo ni moja kati ya mbinu ya kuleta amani na kupunguza kasi ya mauaji miongoni mwa nchi katika Bara la Afrika.

Pamoja na kuiwakilisha nchi katika kikao hicho cha mwaka, Ngole amesema alipata fursa ya kutembelea maonesho ya madini yanayoandaliwa na wizara yenye dhamana na madini nchini Sudan na kujifunza mambo muhimu ambayo nchi yetu ikiyafanya itasaidia katika kukuza sekta ya madini.

Amesema, kuwepo kwa maonesho ya madini kunafungua ukurasa kwa wachimbaji na wauzaji wa madini kukutana na kushirikishana uzoefu katika masuala yanayohusiana na sekta ya madini. 

Swali unaweza kujiuliza je? Umoja wa kusimamia sekta ya madini Afrika una umuhimu gani?. 

Akifafanua swali hilo, Ngole anasema, wakati wa uumbaji wa nchi/dunia mipaka ya kikanda na kijiografia havikuwepo, kutokana na hilo mipaka hiyo haizuii miamba ya madini iliyopo Tanzania inapofika baina ya mpaka wa nchi na nchi kukoma na kutokuendelea, kutokana na ukweli huo ushirikiano huo utazifanya nchi mwanachama kufanya shughuli za uchimbaji kwa namna zinazofanana na kutumia uzoefu wa nchi jirani kutambua uwepo wa madini katika nchi nyingine. 

Ameongeza kuwa, katika kufanya tafiti za madini kuna ramani za madini zinatengenezwa, endapo kutakuwa na ushirikiano ramani hizo zitaandaliwa kwa vigezo vinavyofanana hivyo utangazaji wa sekta ya madini kufanana kwa nchi zote mwanachama.

Ameendelea kueleza kuwa, tafiti za pamoja zinasaidia sana katika kugundua aina mbalimbali za madini yaliyopo kwenye nchi wanachama kutokana na kufanya tafiti kwa pamoja na kubainisha kuwa mipaka ya kijiolojia iko tofauti na mipaka ya kijografia.

Pia ushirikiano unasaidia kupunguza changamoto ya utoroshwaji wa madini na kubainisha kuwa kutokuwepo na ushirikiano na mbinu za kuwafanya watoroshaji wa madini kukaguliwa katika mipaka ya nchi, nchi mwanachama hazitanufaika na madini yanayochimbwa kwani hayatalipiwa tozo zinazotakiwa na Serikali.

Katika hatua nyingine, inabainishwa kuwa, ushirikino ukiwepo baina ya nchi wanachama nchi hizo zitakuwa na sera zinazofanana kusimamia sekta ya madini. 

Hii itatokana na mijadala wanayoifanya ya kubaini na kuchangia uzoefu katika kuendesha sekta, wawekezaji watashindwa kukimbia kimbilia, kwani sera zinafanana za nchi hizo zinafanana na kuamua kuwekeza mahali walipoanzia.

 UMOJA UNAVYOJIENDESHA

Uendeshwaji wa kituo hicho unategemea michango ya nchi wanachama kwa asilimnia 60 ambapo kila nchi mwanachama anatakiwa kuchangia kiasi cha sh.milioni 150 (zaidi ya dola za Kimarekani 62,000) kwa mwaka na asilimia 40 zinatokana na kipato kitokanacho na ada za huduma zinazotolewa na kituo hicho.

KILICHOJADILIWA

Aidha, katika kikao hicho, kilijadili tathmini ya utekelezaji wa maelekezo yaliyotolewa na kikao cha maamuzi cha mwaka uliotangulia ili kujiridhisha na mwenendo wa kituo hicho na kubaini changamoto zinazopelekea maagizo hayo kutokutekelezwa.

UMUHIMU WA KITUO

Kwanza kabisa kituo cha umoja huo kipo nchini Tanzania katika Jiji la Dar es Salaam. Uwepo wa kituo hicho ni heshima kubwa taifa limepewa na kuaminiwa na nchi wanachama.

Umuhimu wa kwanza unaotokana na kituo ni elimu inayotolewa katika kituo hicho kwa wachimbaji wadogo wa madini, hivyo Watanzania wengi kunufaika. 

Wachimbaji wanafundishwa namna ya kukata madini, kuyaongezea thamani kwa kutengeneza bidhaa mbalimbali zitokanazo na madini pamoja na njia bora za uchenjuaji wa madini.

Pili kituo kinatoa huduma za kimaabara, hivyo mtu yeyote mwenye madini na anataka kutambua madini yake anaweza kupata huduma hiyo katika kituo hicho.

Vikao vya utendaji wa kituo vinakaliwa kila mwaka sawasawa na utaratibu uliowekwa na nchi wanachama.

Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (wa pili kutoka kulia)  akifuatilia mada wakati wa kikao kilichowahusisha Mawaziri wenye Dhamana na madini kwa nchi wanachama wa Kituo cha Madini na Jiosayansi Afrika kilichofanyika mwezi Februari nchini Sudan, kushoto kwake ni Kamishna Msaidizi wa Madini anayeshughulikia uwajibikaji wa migodi katika kutoa huduma na unufaikaji wa wazawa, Torence Ngole. 

Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (wa kwanza kulia) akiwa pamoja na wawakilishi wengine kutoka mataifa wanachama wa Kituo cha Madini na Jiosayansi Afrika kilichofanyika mwezi Februari nchini Sudan, wakifuatilia mada.