Monday, April 1, 2019

Naibu Waziri Nyongo abaini udanganyifu madini Kahama


Aelekeza soko la madini kuanzishwa mara moja………

Na Greyson Mwase, Kahama

Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo ameelekeza soko la madini katika mkoa wa kimadini wa Kahama ikiwa ni pamoja na maeneo mengine ya Chunya, Musoma, Singida kuanzishwa mara moja ili kudhibiti utoroshwaji wa madini unaopelekea Serikali kukosa mapato yake.

Naibu Waziri Nyongo ameyasema hayo leo tarehe 31 Machi, 2019 katika mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika mjini Kahama. Wengine waliokuwepo katika mkutano huo ni pamoja na Kamishna Msaidizi, Uendelezaji Migodi na Madini wa Wizara ya Madini,  Ali Saidi Ali, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Kimadini wa Kahama, Andrea Fabian pamoja na wataalam kutoka Tume ya Madini.

Alisema kuwa, mara baada ya kufanya ziara yake ya siku moja katika Wilaya ya Kahama, alibaini kumekuwepo na udanganyifu mkubwa katika shughuli za uchenjuaji wa madini huku akitolea mfano wa kampuni ya Busami inayojihusisha na uchenjuaji wa madini ya dhahabu.

Alisisitiza kuwa, alibaini kumekuwepo na udanganyifu kwenye uzito na kiwango halisi cha dhahabu kwenye madini yaliyopatikana hali inayopelekea Serikali kukosa mapato yake stahiki.

“Kwa mfano katika mtambo wa kuchenjua dhahabu unaomilikiwa na kampuni ya Busami tumebaini kuna udanganyifu kwenye uchenjuaji, jana baada ya kufika na kuona namna uchenjuaji wa madini unavyofanyika na kuelekeza wataalam wa madini kuchenjua upya mchanga uliokuwepo kwenye maji yaliyohifadhiwa, tulibaini kuna madini," alisema Nyongo

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri Nyongo alisimamisha shughuli za uchenjuaji katika kampuni ya Busami na kutaka hatua za kisheria kuchukuliwa dhidi ya mmiliki wake.

Wakati huo huo, Naibu Waziri Nyongo alielekeza wamiliki wote wa mitambo  ya kuchenjulia madini ya dhahabu nchini kuhakikisha wanakuwa na mizani na mashine maalum za kupimia madini ya dhahabu zilizoidhinishwa na Wakala wa Vipimo Tanzania, na biashara ya madini kufanyika katika masoko ya madini yaliyoanzishwa na kusisitiza kuwa lazima madini yajulikane yanapopelekwa na Ofisi za Madini Nchini kuhakikisha zinatuza kumbukumbu sahihi.

Wakati huo huo Naibu Waziri Nyongo aliagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila pamoja na Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Profesa Shukrani Manya kufuatilia iwapo hatua za kisheria zimechukuliwa dhidi ya kampuni inayojihusisha na uchenjuaji wa madini ya dhahabu Wilayani Kahama ya Jema baada ya kukamatwa ikifanya udanganyifu hivi karibuni.

No comments:

Post a Comment