Thursday, March 28, 2019

Waziri Mkuu atembelea Mji wa Serikali


Na Greyson Mwase,

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, amewapongeza wakandarasi kwa kukamilisha ujenzi wa majengo ya ofisi za Serikali katika eneo la Ihumwa jijini Dodoma.

Ametoa pongezi hizo leo tarehe 27 Machi, 2019 mara baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi huo na kuonesha kuridhishwa na hatua iliyofikiwa.

“Nimefurahishwa sana na wakandarasi waliochukua zabuni za kujenga majengo ya ofisi hizi, hivyo ninawaomba Wakala wa Ujenzi Tanzania (TBA) watoe vyeti kwenye majengo ambayo yamekamilika kwa asilimia mia ili waanze kutumia majengo hayo kama ilivyokusudiwa,” alisema Majaliwa.

Katika  hatua nyingine, Waziri Mkuu Majaliwa  hakuridhishwa  na ubora  wa milango iliyopachikwa kwenye jengo la Ofisi ya Makamu wa Rais pamoja na Jengo la Wizara ya Fedha na kuagiza milango hiyo kubadilishwa.

Pia, Majaliwa ameliagiza Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kupeleka umeme mkubwa katika eneo hilo kwa wakati ili majengo yakamilike kwa asilimia mia na kufikia azma ya Serikali ya kuhamia katika mji wa Serikali baada ya ofisi hizo kufunguliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Mgufuli.

Kwa upande wake Waziri wa Fedha, Philip Mpango, amesema mradi wa ujenzi wa nyumba hizo umezalisha ajira kubwa kwa vijana kutokana na kuajiri takribani watu 1141 walioshiriki katika ujenzi huo.

Akizungumzia hatua iliyofikiwa katika ujenzi wa Jengo la Wizara ya Madini,   Naibu Waziri wa  Madini, Stanslaus Nyongo, amesema jengo la Wizara limekamilika kwa asilimia 99, na kubainisha kuwa, mkandarasi yupo katika hatua za mwisho ili aweze kukabidhi jengo hilo.


Sehemu ya Jengo la Wizara ya Madini lililopo katika eneo la mji wa Serikali Ihumwa jijini Dodoma ambalo mpaka sasa limekamilika kwa asilimia 99.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa pamoja na Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (katikati mbele) wakipata maelezo ya hatua iliyofikiwa ya ujenzi wa Jengo la Wizara ya Madini kwenye mji wa Serikali, Ihumwa jijini Dodoma kutoka kwa msimamizi wa mradi wa ujenzi huo (kulia).


Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (wa tatu kutoka kushoto) akiwa pamoja na baadhi ya viongozi waandamizi wa Serikali wakati wakimsubiri  Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kwenye jengo la Wizara ya Madini  kabla ya kuanza kwa ukaguzi kwenye jengo hilo.

No comments:

Post a Comment