Na Asteria Muhozya,
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Ndugani, amesema awali,
Taifa halikunufaika na rasilimali madini kwa kuwa sekta hiyo haikuwa ajenda ya Kitaifa.
“Madini yaliachwa kwa wabunge ambao rasilimali hiyo inapatikana kwenye
maeneo yao, haikuwa ajenda ya taifa, wengine walizungumzia zaidi masuala yanayowagusa
kama korosho, pamba na mambo mengine, nashukuru tumefanya mabadiliko na sasa
matokeo yameanza kuonekana,” amesema Spika Ndugai.
Amesema kwa mwelekeo wa sasa,
serikali imefika mahali ambapo manufaa ya rasilimali hiyo yameanza kuonekana
kutokana na mageuzi makubwa yaliyofanywa
na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Magufuli na kumpongeza kutokana
na namna anavyohakikisha rasilimali madini inalinufaisha taifa, na kuongeza,
“kilio cha watanzania cha kutokunufaika na madini kimepata mwenyewe, Rais
Magufuli amefanya uthubutu”.
Spika Ndugai ameyasema hayo Machi 30, 2019, wakati akifungua Semina kwa
Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini na baadhi ya
Wenyeviti wa Kamati nyingine za bunge wanaohudhuria semina ya siku mbili jijini
Dodoma, iliyoandaliwa na Wizara ya Madini kwa lengo la kutoa elimu ili kupata
uelewa wa sekta ya madini.
Amesema, awali, ikijulikana kama Wizara ya Nishati na Madini ilikuwa ni
kazi hata kwa bunge hilo kupitisha Bajeti ya wizara hiyo kutokana na kwamba,
sekta zote mbili nishati na madini hazikuwa
zikilinufaisha taifa na kusema, “ kulikuwa na kutokuridhika na sekta zote na
hususan madini, kama taifa tulikuwa hatupati haki yetu tuliyoistahili”.
Kufuatia hali hiyo, Spika Ndugai amewataka Wabunge na wananchi kuunga mkono jitihada
zinazofanywa na Rais Magufuli kwa
kuwa mchango wa sekta ya madini katika
uchumi wa taifa utasaidia kusogeza mbele maendeleo ya taifa na watu wake.
Aidha, amewaasa viongozi wote waliobeba dhamana ya kusimamia sekta
husika kuhakikisha wanaichukulia dhamana waliyopewa kwa uzito wa kipekee ili kuliwezesha taifa kufanana na nchi
nyingine ambazo zimeendelea kutokana na rasilimali madini.
Pia, amepongeza mabadiliko yanayofanywa na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO)
na kueleza kwamba anafurahi kusikia STAMICO mpya tofauti na ilivyokuwa awali.
Ameongeza kuwa, ripoti hizo zilipokelewa vizuri na serikali na kwamba
juhudi zilizochukuliwa zimewezesha uanzishwaji wa masoko ya madini huku STAMICO
ikifanya mabadiliko makubwa.
Kwa upande wake, Waziri wa Madini Doto Biteko akizungumza katika semina
hiyo, amesema sekta ya madini ni muhimu
kwa uchumi wa taifa la Tanzania na kueleza kuwa, mchango wa taifa umeendelea
kuongezeka mwaka hadi mwaka na kueleza kuwa, mwaka 2017, sekta hiyo ilichangia
asilimia 4.8 kwenye pato la taifa ikilinganishwa na asilimia 4.0 mwaka 2015.
Akizungumzia ukuaji wa sekta hiyo amesema umeongeza kwa kasi kutoka
asilimia 9.0 mwaka 2015 kufikia 17.5 mwaka 2017, na kusema mafanikio hayo
yametokana na juhudi za serikali kuhakikisha sekta hiyo inachangia zaidi ili kufikia lengo la asilimia 10 ya mchango
wake ifikapo mwaka 2025.
Akizungumzia marekebisho ya Sheria ya Madini yaliyofanywa mwaka
2017, na usimamizi wa Rasilimali Madini,
amesema umewezesha ongezeko la makusanyo ya maduhuli yatokanayo na shughuli za
madini kutoka Shilingi bilioni 194 iliyotarajiwa kukusanywa mwaka 2017/18 hadi
shilingi bilioni 301.29 sawa na asilimia 154.999 ya lengo la makusanyo kwa
mwaka huo.
“Mhe. Spika, mwenendo wa ukusanyaji maduhuli kwenye sekta hii kwa mwaka
2018/19 ni wa kuridhisha ambapo hadi Februari kiasi cha shilingi 218,650,392
kimekusanywa hii ikiwa ni sawa na asilimia 105.6,” amesema Waziri Biteko.
Ameeleza kuwa, miongoni mwa sababu zilizopelekea mafanikio hayo ni
pamoja na kuongezeka kwa mrabaha kwa
baadhi ya madini, kuanzisha kodi
mpya ya ukaguzi ya asilimia 1;
kuimarisha udhibiti wa utoroshaji wa madini; na kwa kushirikiana na
wananchi na vyombo vya ulinzi na usalama
na kuzuia usafirishaji wa madini ghafi ya nje ya nchi ili viwanda vya kusafishia na kuongeza ubora wa
madini vijengwe nchini.
Akizungumzia usimamizi wa shughuli za madini ya Tanzanite baada ya
kukamilika kwa ukuta unaozunguka machimbo ya tanzanite Mirerani amesema
udhibiti wa madini hayo umeimarika na
kusababisha kuongezeka kwa ukusanyaji wa maduhuli yatokanayo na madini hayo.
Ameongeza kuwa, kufuatia juhudi hizo, ukusanyaji wa maduhuli kutokana na
uzalishaji wa tanzanite kwa wachimbaji wa Wadogo na Kati uliongezeka hadi
kufikia shilingi 1,436, 427, 228.99 kwa mwaka
2018, ikilinganishwa na shilingi
71,861,970 kwa mwaka 2016.
“Uzalishaji umeongezeka kutoka migodi midogo na ya kati hadi kufikia
kilo 781.204 kwa mwaka 2018 ikilinganishwa na kilo 147.7 zilizoripotiwa kwa mwaka 2017 na kilo 164.6 za mwaka 2016,”
amesema Waziri Biteko.
Naye, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini Dustan
Kitandula, ameishukuru Wizara kwa kuandaa semina hiyo kwa wabunge na kueleza kuwa,
kamati hiyo itaendelea kupata uelewa kuhusu sekta ya madini.
Mbali na wabunge,
wengine wanaoshiriki semina hiyo ni Wenyeviti wa Bodi za taasisi za zilizo
chini ya wizara, Wataalam kutoka wizarani na taasisi zake.
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Job Ndugai akieleza jambo wakati akifungua Semina kwa Wajumbe wa Kamati ya
Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini( hawapo pichani).
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Job Ndugai (wa pili kulia) akiteta jambo na Waziri wa Madini Doto Biteko (wa
pili kushoto)na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini,
Dustan Kitandula (wa kwanza kulia). Wa kwanza kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara
ya Madini, Prof. Simon Msanjila.
Baadhi ya Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya
Nishati na Madini wakifuatilia mada mbalimbali zilizowasilishwa na wataalam wa
Wizara ya Madini.
Baadhi ya Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya
Nishati na Madini wakifuatilia mada mbalimbali zilizowasilishwa na wataalam wa
Wizara ya Madini.
Baadhi ya Watumishi wa Wizara ya Madini, Wenyeviti wa Bodi ya
Taasisi chini ya wizara na Wataalam
kutoka wizarani na taasisi zake
wakifuatilia hotuba ya ufunguzi wa Semina iliyotolewa na Spika wa Bunge la
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai kwa
Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini na baadhi ya
wabunge wa kamati nyingine (hayupo pichani).
Baadhi ya Watumishi wa Wizara ya Madini, Wenyeviti wa Bodi ya
Taasisi chini ya wizara na Wataalam
kutoka wizarani na taasisi zake
wakifuatilia hotuba ya ufunguzi wa Semina iliyotolewa na Spika wa Bunge la
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai kwa
Wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini na baadhi ya
wabunge wa kamati nyingine (hayupo pichani).
No comments:
Post a Comment