Na Issa Mtuwa, Ulanga
Morogoro
Mwenyekiti wa Tume ya
Madini Prof. Idris Kikula amewataka Watumishi wa tume hiyo ofisi ya Morogoro na Ulanga
kutambua kwamba agizo la Waziri linalowataka kufuta leseni zisizofuata
utaratibu wa kisheria sio la kujadili bali ni kutekeleza.
Prof. Kikula ameyasema
hayo Aprili 10, 2019 wilayani Ulanga wakati akizungumza na watumishi wa tume
hiyo wakati wa ziara yake.
Taarifa iliyosomwa kwake
na Afisa Migodi Mkazi ofisi ya Mahenge Ulanga, Tandu Jilabi inaonyesha kuwa
wilaya ya Ulanga ina leseni za wachimbaji wadogo 221 kati ya hizo ni leseni 9
tu ndio zinazofanya kazi huku leseni za uchimbaji wa kati zikiwa 5 na leseni za
utafiti wa madini 13.
Kufuatia hali hiyo, Afisa Migodi Mkazi ofisi
ya Mahenge ameiomba tume ya madini kufuta leseni zisizofanya kazi ili wapewe
wenye uhitaji ili waweze kuziendeleza. Kufuatia ombi hilo, Mwenyekiti wa tume
amesema jukumu la kuzifuta leseni hizo ni la kwake pamoja na Afisa Madini Mkazi
Morogoro na halina mjadala kwakuwa muongozo wa utekeleza wa suala hilo
ulishatolewa na waziri wa Madini.
“Suala la leseni
zisizofanya kazi sio la kujadili, hili ni agizo la Waziri na kazi yetu ni
kutekeleza na wenye kuzifuta ni ninyi, fuateni taratibu uliowekwa kwa mujibu wa
sheria katika kuzifuta na sio kuzifuta lazima wote waliozishikilia leseni hizo
kwa muda wote walipe fidia na wasipo fanya hivyo taratibu za kisheria zifuatwe
kwani katika kipindi hicho chote serikali imekosa mapato yake. Kuanzia leo
pitieni leseni zote na ifikapo Juni 30 mwaka huu leseni zote zisizo hai ziwe
zimefutwa”, amesema Prof. Kikula.
Wakati huo huo,
mwenyekiti wa tume amekutana na kuzungumza mwakilishi wa mwekezaji wa kampuni
ya TanzGraphite (T) Ltd ambae ni Meneja Uhusiano wa Jamii na kuzungumzia kuhusu
mgogoro uliopo baina ya mwekezaji huyo na baadhi ya wananchi wanaotakiwa
kufanyiwa tathimini ili kupisha shuguli za uchimbaji wa madini katika eneo
hilo.
Prof. Kikula
ameonyesha kusikitishwa na mgogoro huo ambao amesema ni wa muda mrefu sasa na
unachelewesha maendeleo ya watu na kuikosesha serikali mapato.
Ameongeza kimsingi
wananchi wanapaswa kuelewa kuwa “right
surface” (haki ya kumiliki vitu vilivyo juu ya ardhi) inampa mwananchi haki
ya kulipwa fidia ya mali zilizo juu ya
ardhi anayo miliki lakini watambue kuwa kuna “resource right” (haki ya kumiliki raslimali zilizo chini ya ardhi)
ikiwemo madini ambayo mmiliki wake ni serikali, ndio maana inapohitaji
raslimali hizo humuondoa na kumfidia mliliki wa mali za juu ya ardhi, hivyo wananchi
wanapo ng’ang’ania wanatakiwa walitambue hilo.
Pia, amesema kuwa,
kwa mpango ulioanishwa na mwekezaji huyo unaonyesha manufaa kwa wananchi
kupitia miradi ya maendeleo (CSR) ambapo amebainisha kuwa mwekezaji ameahidi
kuwalipa fidia, kuwajengea nyumba za kisasa wale wote walio ndani ya eneo.
Mambo mengine ni
pamoja na kuwapatia chakula kwa muda wa miaka miwili wakiwa kwenye makazi mapya
watakayo jengewa na kila kaya kusomesha mtoto mmoja kwenye vyuo vya veta na
wakihitimu wataajiriwa na mgodi ili waweze kupata kipato cha kusaidia na
kuendeleza kaya zao.
Pamoja na hayo,
mwekezaji huyo amemweleza mwenyekiti wa tume kuwa tayari wameshakubaliana
kujengaa kituo cha afya, matundu ya vyoo kwa baadhi ya shule, kujenga shule na
ukarabati wa vyumba vya madarasa katika shule mbalimbali. Hata hivyo hakusita
kuonyesha kusikitishwa kwake na watu wachache wanaogoma kuondoka kupisha
shuguli za uchimbaji huku kila kitu ikiwemo mtaji wa shuguli hizo ukiwa tayari.
Katika mgogoro huo,
kaya 347 zinatakiwa kuondoka kupisha mwekezaji huyo na kati ya hizo kaya 62
ndio zinazo goma kuondoka ili mwekezaji aanze kazi ya uchimbaji. Mwenyekiti
amesikitishwa na hali hiyo na na kuuomba uongozi wa mkoa na wilaya kuzungumza
na kaya hizo sambamba na Baba Askofu aliyeko ndani ya eneo hilo ili mradi huo
uanze kwani ni wa muda mrefu na serikali inakosa mapato.
Amesema kwa sasa
anaziachia juhudi za serikali ya mkoa na wilaya katika kuupatia ufumbuzi
mgogoro huo.
Mapema mwenyekiti
alikutana na kufanya mazungumzo na Mkuu wa Wilaya ya Ulanga Ngolo Malenya ambapo
amemshukuru kwa ushirikiano anao utoa kwa viongozi na wafanyakazi wa tume ya
madini wilaya ya Ulanga.
Amesisitiza suala la
uadilifu kwa wafanyakazi wa tume na amesema hilo litakuwa jambo la kwanza
kulisema kila aendapo sambamba na ukusanyaji wa maduhuli ya serikali. Aidha, amesema kipimo kikubwa cha kila mkuu wa
kituo cha tume ya madini kitakuwa ni ukusanyaji wa maduhuli ambapo katika Mwaka
wa Fedha 2018/2019 tume ilipangiwa kukusanya Bilioni 310 na mwaka wa fedha ujao
tume imepangiwa kukusanya Bilioni 467.
Upande wake, Kamishna
wa tume hiyo Dkt. Athanas Macheyeki amewakumbusha na kuwasisitiza watumishi wa
tume na wachimbaji wa madini kuhakikisha wanasimamia ukusanyaji na ulipaji wa
tozo na stahiki zote za serikali kwa wakati.
Amesema kwa kufanya
hivyo raslimali za madini zitakuwa na tija kwa taifa kama anavyo sisitiza Rais
John Pombe Magufuli kuwa anataka raslimali za madini ziwanufaishe watanzania
wote na namna za kuwanufaisha ni kulipa stahiki za serikali zinazo tokana na
madini ili zikatumike kujenga uchumi wa taifa.
Prof. Kikula na Dkt. Macheyeki
wanaendelea na ziara yao mkoani Morogoro kukagua shuguli za Tume katika Wilaya
mbalimbali ambapo leo walitembelea eneo la wachimbaaji wadogo ipanko wilayani
ulanga.
No comments:
Post a Comment