Ø Naibu Waziri Nyongo ataka Soko la Madini Arusha
kuanzishwa haraka
Waziri wa
Madini Doto Biteko amesema Serikali kupitia Wizara yake inalenga kurahisisha
Mazingira ya Biashara ya Madini ikiwemo kuwalea wachimbaji na kuwataka
wafanyabiashara na wachimbaji kuhakikisha wanajisimamia wenyewe kwa manufaa yao
na Taifa.
Waziri Biteko
ameyasema hayo alipokutana na viongozi wa Chama Cha Wafanyabiashara wa Madini
Tanzania (TAMIDA), wakiongozwa na Mwenyekiti wa Chama hicho Sam Mollel ofisini
kwake jijini Dodoma Aprili 10, kwa lengo la kujadili masuala mbalimbali
yanayohusu biashara ya madini nchini.
Amekitaka
chama hicho kuendelea kushirikiana na wizara kwa lengo la kusukuma mbele Sekta
ya Madini ikiwemo kuhakikisha biashara ya madini inafanyika katika mazingira
yenye kuzinufaisha pande zote na kuwasisitiza viongozi hao kuhakikisha
wanachama wao wanafuata taratibu wanapofanya biashara ya madini.
Awali, kabla
ya kujibu hoja zilizowasilishwa na chama hicho, Waziri Biteko amekipongeza chama
hicho kwa kuwa kimekuwa kikitoa njia mbadala pindi kinapowasilisha
changamoto na kero zake badala ya
kuishia kulalamika na kuongeza, “wizara inaona fahari kwa hilo na
tunayachukulia kwa umuhimu maoni yenu,”.
Akizungumzia
suala la kodi ya ongezeko la thamani na kodi ya zuio ambayo imeondolewa kwenye
uchimbaji mdogo, Waziri Biteko amekitaka Chama hicho kutoa nafasi kwa serikali
kufuatilia suala hilo. Waziri Biteko ameleeza hilo kufuatia hoja
iliyowasilishwa na Mwenyekiti wa TAMIDA Sam Mollel ambaye ameeleza kuwa, katika
mkoa wa Arusha, kodi hiyo bado inatozwa licha ya serikali kuiondoa.
Aidha, Waziri
Biteko ametolea ufafanuzi wa changamoto kadhaa zilizowasilishwa na Mwenyekiti
Sam Mollel kwa niaba ya chama hicho ikiwemo. Kuhusu bei elekezi, Waziri
Biteko amesema wizara itaendelea
kushirikiana na wadau kuhakikisha suala hilo linakuwa shirikishi. Waziri Biteko
amesema hilo baada ya TAMIDA kutoa pongezi kwa serikali kwa kutoa nafasi kwa
wadau kukaa pamoja na serikali kujadili suala la bei elekezi ambapo Mwenyekiti
huyo amemweleza Waziri Biteko kuwa, katika hilo, serikali na wadau wameanza
vizuri.
Akitolea
ufafanuzi kuhusu suala la kurejesha maonesho ya madini jijini Arusha, Waziri
Biteko amesema suala la maonesho ya madini kufanyika arusha inawezekana lakini
si kwa madini ya Tanzanite, na kuongeza kuwa, serikali imedhamiria kufanya
shughuli zote zinazohusu madini hayo ndani ya ukuta unaozunguka machimbo ya
mirerani lakini pia ikilenga kuubadilisha
mji wa mirerani ufanane na madini
hayo.
Aidha, Waziri
Biteko amezungumzia suala la kuongeza wataalam wa kuthamini madini ya Tanzanite
Mirerani na kueleza kuwa, kutokana na unyeti na umuhimu wa suala hilo, tayari
serikali imeanza kulifanyia kazi ili kuhakikisha inaongeza idadi ya wataalam
kuwezesha shughuli za uthamini Mirerani, kufanyika kwa wakati. Ufafanuzi huo
umetolewa baada ya Mwenyekiti wa TAMIDA Sam Mollel kuwasilisha changamoto ya
kuwepo na upungufu wa wataalam hao.
Kwa upande
wake, Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo akizungumza katika kikao hicho,
ametaka kuanzishwa haraka kwa soko la Madini jijini Arusha na kueleza kuwa, kwa
upande wa wizara itahakikisha inashirikiana na serikali ya mkoa kuhakikisha
soko hilo linaanzishwa haraka. Naibu Waziri Nyongo amesema hayo akijibu hoja ya
Mwenyekiti wa TAMIDA Sam Mollel ambaye ameleeza katika kikao hicho kuwa, Chama
hicho kinaunga mkono Serikali kuhusu uanzishwaji wa masoko ya madini na kuitaka
serikali ione umuhimu wa kuanzisha soko La madini la madini mkoani arusha
kuwezesha biashara ya madini ya vito kufanyika kwa urahisi.
Kuhusu vibali
vya Wataalam wa masuala ya ukataji na unga’rishaji wa madini kutoka nje ya
nchi, Naibu Waziri Nyongo amesema kuwa, ni kweli kwamba serikali inawahitaji
wataalam hao kwa kuwa pia watawezesha kutoa ujuzi huo kwa wataalam wa ndani ili
kuhamasisha viwanda vya ukataji madini na kuongeza, “ serikali inaangalia namna
ya kulipatia ufumbuzi suala hilo kwa kushirikiana na mamlaka zinazohusika kwa
sababu pia tunataka watu wetu wanufaike na utaalam huo”,.
Pia, ameongeza
kuwa, kutokana na kulichukulia suala la uongezaji thamani madini kwa umuhimu, inakitegemea
kituo cha Jemolojia Tanzania (TGC) kwa ajili ya kuzalisha wataalam na kukitaka
chama hicho kusaidia kuongeza idadi ya wanafunzi wanaodahiliwa katika kituo
hicho kwa kuwa hivi sasa idadi bado ni ndogo.
Kikao hicho
cha Waziri na TAMIDA ni cha kwanza tangu kuteuliwa kwa Waziri wa Madini Doto
Biteko kuiongoza wizara husika.
Wengine
waliohudhuria kikao hicho ni Viongozi Waandamizi kutoka wizara ya Madini na
Tume ya Madini.
Baadhi ya Viongozi wa Chama Cha Wafanyabiashara ya
Madini Tanzania (Tamida) wakifuatilia
mkutano wao baina ya Waziri wa Madini Doto Biteko , Naibu Waziri na Viongozi wa
Wizara.
Waziri wa Madini Doto Biteko (wa kwanza kulia) akizungumza jambo wakati wa
kikao baina yake na Chama Cha Wafanyabiashara wa Madini Tanzania (TAMIDA).
Wengine wanaofuatilia ni Kamishna wa Madini, Mhandisi David Mulabwa (kulia kwa
Waziri) na Ujumbe wa Chama hicho.
Waziri wa Madini Doto Biteko katika picha ya
pamoja na Viongozi wa (TAMIDA) pamoja na
Viongozi Waandamizi wa Wizara baada ya kikao.
|
No comments:
Post a Comment