Thursday, April 25, 2019

Wachimbaji watelekeza Madini na pikipiki kumbia msafara wa Mwenyekiti wa Tume ya Madini

Na Issa Mtuwa, Gairo

Wachimbaji wa Madini ya Rubi wilaya ya Gairo kata ya Iyombe kijiji cha Kirama, wamekimbia na kutelekeza Madini ya viwandani aina ya Rubi Nut, Pikipiki na vifaa mbalimbali vya kuchimbia baada ya kuona msafara wa Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Idris Kikula na Mwenyekiti wa ulinzi na usalama ambae pia ni Mkuu wa Wilaya (DC) ya Gairo Seriel Shaid Mchembe waliokuwa wanatembelea mgodi huo kuona shuguli za uchimbaji kwa lengo la kwenda kutatua kero zinazowakabili.

Msafara wa mwenyekiti wa Tume ya madini akiwa ameambatana na Kamishna wa Tume hiyo Dkt. Athanas Machiyeke na mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ulianza majira ya saa tatu asubuhi kuelekea  kwenye eneo la mgodi.

Wakiwa njiani msafara huo ulikubwa na changamoto baada ya gari ya Polisi iliyokuwa inaongoza msafara huo kukwama kwenye maji katikati ya mto kwa muda wa saa moja kitendo kilichopelekea kuchelewa kufika kwenye eneo la mgodi. 

Hata hivyo mara baada ya kufika kwenye nyumba ya mchimbaji mmoja alie tambuliwa kwa jina la Sadick Athuman maarufa kwa jina la (Saadam) alikutwa kijana mmoja aliejitambulisha kwa jina la Athumani mkazi wa Gairo mjini akilinda mahali apo ndipo mkuu wa Wilaya na vyombo vyake vya ulinzi na Mwenyekiti wa Tume na Kamishna waliingia ndani na kufanya msako na kukuta madini aina ya Rubi Nut yakiwa kwenye mifuko, Pikipiki moja na vifaa mbalimbali vya kuchimbia.

Alipo ulizwa bwana Athumani, nani anae miliki madini hayo, alisema ni madini ya bwana Saadam. Alipo ulizwa yeye anafanya nini alisema yeye ni kibarua tuu na mwenyewe Saadam yupo mgodini anaendelea na uchimbaji ndipo Mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama akamuamuru Athumani kwenda nae mpaka anakochimba bwana Saadam na mara baada ya kufika eneo la mgodi wachimbaji wote wakakimbia na kuelekea vichakani akiwemo bwa Saadam huku vifaa vya uchimbaji vikiwa vimetelekezwa sambamba na madini yale ya kwenye mfuko na pikipiki.

Kufuatia kitendo hicho mwenyekiti wa tume ya Madini Prof. Kikula amesikitishwa na kitendo hicho ambacho kinaashiria uchimbaji wa mgodi huo unafanyika bila kufuata sheria.

Kutokana na hali hiyoo, mwenyekiti wa tume amemuagiza afisa Madini Mkazi mkoa wa Morogoro Mhandisi Emmanuel Shija kufuatilia uhalali wa eneo hilo (Leseni na Codinates) na mwenendo mzima wa uchimbaji wake, endapo eneo hilo litakuwa na leseni mmiliki wake alipe maduhuli yote anayotakiwa kulipa tangu alipoanza na kama eneo hilo halijakatiwa leseni mgodi huo ufungwe mara moja na shuguli za uchimbaji zisitishwe mara moja.

Aidha, amesikitishwa na wachimbaji na wawekezaji katika eneo hilo kushindwa kusaidia shuguli za maendelo ya kijiji kinacho zunguka migodi hiyo ambapo ofisi yake haikumridhisha mwenyekiti wa tume.

Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Gairo amesikitishwa na wachimbaji hao kwa kukiuka sheria zinazo ongoza shuguli za uchimbaji madini, amesema amekuwa akiwahimizi mara kadhaa wachimbaji wote wilayani humo kuzingatia na kufuata taratibu kabla hawajanza kazi za uchimbaji ikiwemo kukata leseni na kulipa maduhuli ya serikali.

Kufuatia kwa tukio hilo Mchembe amepiga marufuku kwa mtu yeyote katika wilaya ya Gairo kufanya shuguli za madini bila kuwa na kibali kutoka tume ya madini.

Wakati huo huo Mchembe amemuagiza Kamanda wa Polisi wilaya ya Gairo Lugano Piter Mwakisunga kuhakikisha anamkamata Sadick Athumani ndani ya siku saba na kumfikisha kwenye vyombo vya sheria.

Wakiwa kwenye mgodi wa eneo la mwekezaji wa kampuni ya Mofar Holdings (T) Ltd Kamishna wa Tume ya Madini Dkt. Machiyeke amemsisitiza mwekezaji huyo kuzingatia taratibu na sheria katika hatua ya kuajiri wafanyakazi na vibarua na manunuzi ya bidhaa kama muongozo unavyo sema.

Dkt. Machiyeke amesema, sheria inasisitiza kutoa kipaumbele kwa wananchi waozunguka mgodi na taifa kwa nafasi kubwa kabla ya kufikiria nje ya eneo hilo na nje ya nchi.

Mwenyekiti wa Tume ya Madini na Kamishna walikuwa wanahitimisha ziara yao ya siku tano katika mkoa wa Morogoro baada ya kutembelea wilaya ya Morogoro mjini, Ulanga, Mvomero na Gairo ambapo ujumbe wake mkubwa kwa wafanyakazi wa tume na wachimbaji madini ulikuwa ni uadilifu katika kazi zaona kuepuka rushwa.

Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Kikula wa kwanza kushoto akiangalia madini ya Rubi Nut yaliyotelekezwa na mchimbaji wa madini hayo Sadick Athuman maarufu kwa jina la Saadam alie kimbia baada ya kuona msafara wa tume ya Madini na Mkuu wa Wilaya Gairo. Kulia ni Mkuu wa Wilaya Gairo Siriel Shaid Mchembe na Kamishna wa Tume ya Madini Dkt. Athanas Machiyeke.

 Msafara wa Tume ya Madini na wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama wakiwa kwenye eneo la mgodi Kijiji cha Kirama walipotembelea kukagua shuguli za uchimbaji katika eneo hilo wa mbele ni Athumani anae uongoza msafara kwenda kuonyesha anapochimba Sadick Athuan baada ya kukimbia

Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Kikula wa pili kulia akiwa na kamati ya ulinzi na usalama wilaya ya gairo ikiongozwa na mwenyekiti wake Siriel Shaid Mchembe wa tatu kushoto na wa kwanza kulia ni Kamishna wa Tume ya Madini Dkt. Athanas Machiyeke wakionyesha baadhi ya vifaa ikiwemo pikipiki iliyo telekezwa na  mchimbaji wa madini Sadick Athuman maarufu kwa jina la Saadam alie kimbia baada ya kuona msafara wa tume ya Madini. 

No comments:

Post a Comment