Na Asteria Muhozya
Ni takriban Miaka Mitatu sasa tangu
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aingie
madarakani kuliongoza Taifa la Tanzania katika Serikali ya Awamu ya Tano.
Tangu Rais Magufuli aingie madarakani mwaka 2015, Serikali
anayoiongoza imefanya mabadiliko makubwa kwenye Sekta ya Madini kwa ajili ya
kuhakikisha kuwa rasilimali madini zinawanufaisha zaidi Watanzania.
Katika hatua za awali za kutekeleza mabadiliko hayo,
Rais Magufuli Mwaka 2017, alianzisha Wizara mpya ya Madini baada ya kutenganishwa
kwa iliyokuwa Wizara ya Nishati na Madini kupitia Hati ya Majukumu (Instrument)
Na.144 ya tarehe 22 Aprili, 2016 na Marekebisho yake ya tarehe 7 Oktoba, 2017.
Wizara hii ya Madini inaongozwa na Waziri wa Madini
Angellah Kairuki na Naibu Mawaziri wawili, Stanslaus Nyongo na Doto Biteko
pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Profesa Simon Msanjila.
Mbali na uundwaji wa wizara hii mpya,
yamefanyika mabadiliko ya Sheria ya Madini ya Mwaka 2010,
utungwaji wa Sheria ya Mapitio na Majadiliano kuhusu Masharti Hasi katika
Mikataba ya Maliasili za nchi wa Mwaka 2017, na Sheria ya Mamlaka ya nchi
kuhusiana na Umiliki wa Maliasili za nchi wa Mwaka 2017.
Utungwaji wa Sheria hizo mpya na mabadiliko ya Sheria
ya Madini na Kanuni zake kumeboresha ulipaji wa mrabaha wa Serikali kutoka
asilimia nne (4) na kuwa asilimia
sita (6) ya bei ya madini ghafi kwa
madini ya metali na vito na kuanzishwa kwa ada ya ukaguzi wa madini ya kiasi
cha asilimia moja (1).
Mabadiliko haya pia yanaiwezesha Serikali kuwa na
umiliki wa asilimia zisizopungua 16 za
hisa huru kwenye Migodi mikubwa na ya kati, kodi ya zuio ya asilimia tano ya
thamani ghafi ya madini imeanzishwa kwa wachimbaji wadogo.
Akizungumza
katika kipindi Maalum cha TUNATEKELEZA,
Waziri wa Madini Angellah Kairuki anasema, Serikali imeweza kufanya majadiliano
na wamiliki wa migodi ya ACACIA na TANZANITE ONE ambapo majadiliano hayo
yameleta matokeo chanya kwa Acacia kukubali kuilipa Serikali kiasi cha Dola za
Marekani Milioni 300.
Katika maelezo yake, Waziri Kairuki
anaongeza kuwa, baada ya majadiliano na Kampuni ya Tanzanite One wamekubali
kulipa fidia pamoja na kodi watakayokubaliana kutokana na dosari zilizokuwepo
hapo awali. “Tume maalum iliyoundwa na Rais inaendelea na majadiliano na
makampuni yote makubwa yenye Mikataba na Serikali. Serikali ya Awamu ya Tano,
imedhamiria kuhakikisha rasilimali za madini zinasimimiwa ipasavyo ili ziweze
kuchangia kwa ufanisi katika uchumi wa Taifa na ustawi wa Watanzania,” anasema
Waziri Kairuki.
Aidha, Kairuki anaeleza kuwa, Mabadiliko ya Sheria
yamewezesha na kuzuia usafirishaji wa madini ghafi nje ya nchi ili madini
yaongezewe thamani hapa nchini. Aidha, Waziri Kairuki anasisitiza, mabadiliko
hayo yanaifanya migodi ilazimike kutumia bidhaa na huduma za ndani ya nchi na
kutoa uwezo wa usimamizi kisheria wa Sekta ya Madini kutakakoleta ufanisi
mkubwa.
Akisisitiza
suala hili katika moja ya mikutano yake na wadau wa sekta ya madini nchini, Waziri
Angellah Kairuki anasema Serikali imeweka ZUIO
la kusafirisha madini ghafi nje ya nchi ikiwa na lengo la kuyaongezea thamani kabla
ya kuyasafirisha. Katika kulisimamia hilo, anasema, Serikali kupitia Wizara ya Madini inaandaa Muswada wa
Sheria ya uongezaji Thamani Madini, ili kuwezesha shughuli za Uongezaji Thamani
madini kufanyika kwa kuzingatia Sheria na kusimamia vyema shughuli za uongezaji
thamani madini nchini.
“Dhamira ya Serikali ni kujenga na kuendeleza Viwanda
vya ndani, kuongeza Mapato ya Serikali kutoka Sekta ya Madini, na kurekebisha mapungufu yaliojitokeza
katika utekelezaji wa Sheria zilizopo katika shughuli za uongezaji thamani
madini hususani kwenye eneo la masonara,” anasisitiza Waziri Kairuki.
Waziri Kairuki anaongeza kwamba, Wizara inaendelea kuhamasisha uwekezaji katika
shughuli za uongezaji thamani madini na kuendelea kutoa leseni za uchenjuaji na
uyeyushaji wa madini ya metali. Pia, anafafanua kuwa, jumla ya maombi 27 ya uwekezaji kwenye smelters
na refineries (ujenzi wa vinu (viwanda) vya uchenjuaji kwa ajili ya
kusafisha na kuongeza thamani madini ya metali) yaliwasilishwa na uchambuzi
unaendelea kufanyika ili kupata mwekezaji atakayekidhi vigezo.
Akizungumzia
ukuaji wa Sekta ya madini katika Awamu hii anasema, Sekta ya Madini ilikua kwa
asilimia 17.5 Mwaka 2017 ikilinganishwa na asilimia 9.1 Mwaka 2015. Mchango wa
Sekta ya Madini katika Pato la Taifa uliongezeka na kufikia asilimia 4.8 Mwaka
2017 ikilinganishwa na asilimia 4.0 Mwaka 2015.
Waziri
Kairuki anasisitiza kuwa, Wizara
imevuka malengo ya makusanyo ya maduhuli iliyopewa mwaka 2017/18
ya Shilingi bilioni 194.66 na kuweza
kukusanya Shilingi bilioni 298 sawa
na asilimia 153.09.
Pia anaongeza, kuongezeka kwa
kiwango cha ukuaji wa Sekta ya Madini kumetokana na kuimarishwa kwa udhibiti wa
biashara haramu na utoroshwaji wa madini; kuimarishwa kwa ukaguzi na usimamizi
katika sehemu za uzalishaji, biashara ya madini; na usafirishaji wa madini nje
ya nchi; kuongezeka kwa viwango vya mrabaha na kuanzishwa kwa ada ya ukaguzi wa
madini kufuatia marekebisho ya Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 yaliyofanyika
Mwaka 2017 na Kanuni zake.
Akizungumzia
uundwaji wa Tume ya Madini, ambayo ni zao la Mabadiliko ya Sheria ya Madini ya
Mwaka, 2010, baada ya kufutwa kwa Wakala wa Ukaguzi wa Madini Tanzania
(Tanzania Mineral Audit Agency–TMAA), Waziri Kairuki anasema kuundwa kwa Tume
ya Madini, kumepelekea usimamizi wa karibu zaidi wa maeneo yenye uchimbaji wa
madini. Aidha, uwepo wa ofisi za madini katika mikoa mbalimbali nchini unarahisisha
ushughulikiaji wa maombi ya leseni, kupunguza migogoro na kuongeza makusanyo ya
mrabaha.
“Pia, Tume imesimamia shughuli za uchimbaji ndani ya ukuta wa
Mererani ili kudhibiti utoroshwaji wa Madini ya Tanzanites na madini mengine ili kuimarisha ukusanywaji wa kodi za
Serikali,” anasema Waziri Kairuki.
Akizungumza katika Mkutano baina ya Waziri Kairuki na Wafanyabiashara
wa Madini ya Tanzanite jijini Arusha, Mwenyekiti wa Chama Cha Wafanyabiashara
wa Madini Tanzania (TAMIDA) Sam Mollel anasema ukuta uliojengwa kuzunguka
migodi ya Tanzanite Mirerani umeongeza Imani
kubwa kwa walaji wa madini hayo zikiwemo nchi za Marekani na Ulaya huku
akisisitiza kuwa, ukuta wa Mirerani umedhibiti ajira za watoto migodini na
kuondoa wizi wa vifaa migodini.
Haya ni baadhi tu ya mafanikio yaliyofanywa na Serikali ya Awamu ya
Tano katika Sekta ya Madini. Kwa hakika watanzania hawana budi kuunga mkono
jitihada hizi zinazofanywa na Serikali ambazo zinalenga kuhakikisha kwamba
rasilimali madini zinalinufaisha taifa na watanzania wote.
Aidha, katika kuhakikisha kwamba sekta ya madini inachangia zaidi
katika pato la Taifa na ukuaji wa uchumi, Waziri Kairuki anasema katika kipindi
cha miaka mitano ijayo, lengo la wizara ni kuhakikisha Sekta ya Madini inachangia
zaidi katika pato la Taifa ili hadi ifikapo mwaka 2025 sekta husika iweze
kuchangia hadi kufikia asilimia kumi (10%).
Waziri wa Madini Angellah Kairuki akimsikiliza mmoja wa Wachimbaji
wa Madini ya Bati katika moja ya ziara zake za kukagua shughuli za uchimbaji
madini, Kyerwa mkoani Kagera.
|
Waziri wa Madini Angellah Kairuki akiangalia bidhaa za mapambo
zilizotokana na madini yanayopatikana nchini baada ya kuongezwa thamani.
|
Wanafunzi wa Shule za Sekondari jijini Arusha wakiangalia Madini ya
Tanzanite wakati wa Maonesho ya 6 ya Kimataifa ya Madini ya Vito na Usonara ya
Arusha (AGF) yaliyofanyika Mwezi Mei,2017.
|
No comments:
Post a Comment