Nuru Mwasampeta na
Greyson Mwase, Geita
Waziri Mkuu wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa ametoa muda wa miezi mitatu
kwa wakuu wa mikoa hususan mikoa yenye utajiri mwingi wa madini ya metali na
vito nchini kuhakikisha wanakamilisha na kufungua masoko ya madini ili kuwawezesha
wachimbaji na wafanyabiashara ya madini kuwa na soko la uhakika la madini hayo.
Majaliwa alitoa agizo hilo kwenye uzinduzi wa Soko la Madini
la Geita tarehe 17 Machi, 2019 uliofanyika katika viwanja vya Soko Kuu mkoani
Geita na kuhudhuriwa na viongozi wengine wa kiserikali ikiwa ni pamoja na
Waziri wa Madini, Doto Biteko, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon
Msanjila, Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula na Katibu Mtendaji
wa Tume ya Madini, Profesa Shukrani Manya.
Wengine ni pamoja na
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Dustan Kitandula,
watendaji kutoka Tume ya Madini, Wakuu wa Mikoa, wabunge, madiwani, viongozi wa
dini, waandishi wa habari pamoja na wananchi kutoka katika mkoa wa Geita pamoja
na mikoa ya jirani.
Alisema kuwa,
uanzishwaji wa masoko ya madini ni sehemu ya utekelezaji wa maagizo ya Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Magufuli aliyoyatoa tarehe 22
Januari, 2019 kwenye mkutano wake na wachimbaji wa madini nchini uliofanyika
jijini Dar Es Salaam.
“Ninawataka wakuu wa
mikoa kuhakikisha agizo hili linatekelezwa kabla ya mwaka wa fedha kumalizika
Juni 30, 2019,” alisema Majaliwa.
Alisema kuwa, katika
kuhakikisha Sekta ya Madini inakuwa na mchango mkubwa kwenye ukuaji wa uchumi
wa nchi na kuwanufaisha watanzania wote, Serikali kupitia Wizara ya Madini
ilianza kwa kuboresha Sheria ya Madini pamoja na kanuni zake na kuwataka
wananchi kuchangamkia fursa hiyo.
Aliongeza kuwa,
serikali imeamua kuondoa tozo mbalimbali zilizokuwa mzigo kwa wachimbaji wa
madini uli uchimbaji wao uwe na faida kubwa na kuwawezesha kulipa kodi
mbalimbali za Serikali.
Alisema kuwa, kufutwa
kwa kodi na tozo mbalimbali kutapunguza kwa kiwango kikubwa utoroshwaji wa
madini nje ya nchi na Serikali kujipatia pato kubwa linalotokana na shughuli za
madini nchini.
Akielezea umuhimu wa
masoko ya madini, Majaliwa alieleza kuwa mbali na kupunguza utoroshwaji wa
madini, hakutakuwepo na dhuluma kwa wachimbaji wadogo wa madini kwani watakuwa
na sehemu yenye uhakika ya kuuzia madini hayo kulingana na bei elekezi
iliyotolewa na Serikali.
Aliendelea kueleza
kuwa, soko la madini litarahisisha
huduma za uuzaji na ununuzi wa madini ambapo huduma zote zitatolewa ndani ya
jengo moja hivyo kuokoa muda wa wauzaji na wanunuzi wa madini.
Katika hatua
nyingine, Majaliwa alitoa tahadhari kwa wadau wote wa madini kuwa,
atakayekamatwa anatorosha madini atachukuliwa hatua za kisheria ikiwemo
utaifishaji wa madini atakayokuwa akiyatorosha.
Pia aliwataka
viongozi na watendaji wa Serikali kusimamia kwa weledi, uaminifu na uadilifu,
sheria, kanuni na miongozo mbalimbali
kuhusu sekta ya madini kwa lengo la kudhibiti utoroshwaji wa madini
hususan dhahabu kwenda nje ya nchi.
Aidha, aliitaka
Wizara ya Madini, Tume ya Madini, Serikali ya Mkoa, Idara na Taasisi nyingine
za Serikali zinazohusika na maendeleo ya
sekta ya madini kuheshimu mipaka ya majukumu yao ili waweze kulisimamia vizuri
soko hilo na kufanya kazi kama ilivyokusudiwa.
“Wizara ya Madini,
ishirikiane na vyama na mashirikisho ya wachimbaji na wafanyabiashara wa madini
kuandaa mpango kazi mahususi kwa ajili ya utekelezaji wa majukumu ya soko hilo
ili lisigeuke kuwa kikwazo kipya kwa wachimbaji na wafanyabiashara wa madini,”
alisisitiza Majaliwa.
Aliendelea kusisitiza
kuwa, Serikali imeamua kutoa mwelekeo mpya katika usimamizi na maendeleo
ya sekta ya madini ambapo
utekelezaji wa dhamira hiyo unakwenda
sambamba na kuweka mazingira mazuri na miundombinu itakayowezesha kuimarika kwa
sekta ya madini nchini.
Jiwe la Msingi kwenye
viwanja vya Soko la Madini Geita mara baada ya kuzinduliwa na Waziri Mkuu wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa tarehe 17 Machi, 2019.
Katibu Mtendaji wa
Tume ya Madini, Profesa Shukrani Manya (kushoto) akielezea namna Ofisi ya Afisa
Madini Mkazi wa Mkoa wa Geita ilivyojipanga kwenye usimamizi wa Soko la Madini Geita kwa Waziri Mkuu wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa kabla ya kuanza kwa shughuli
za uzinduzi wake tarehe 17 Machi, 2019.
Waziri Mkuu wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa (katikati) akisalimiana na
Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula kabla ya kuzindua Soko la
Madini Geita tarehe 17 Machi, 2019.
Mwenyekiti wa Tume ya
Madini, Profesa Idris Kikula (katikati) akizugumza na waandishi wa habari
(hawapo pichani) kabla ya uzinduzi wa Soko la Madini la Geita kufanywa na Waziri
Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa tarehe 17 Machi, 2019.
Soko la Madini Geita
kabla ya uzinduzi wake tarehe 17 Machi, 2019.
Waziri Mkuu wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa akitoa hotuba ya uzinduzi wa
Soko la Madini Geita kwa wananchi na watendaji waandamizi wa Serikali (hawapo
pichani) tarehe 17 Machi, 2019.
Waziri wa Madini,
Doto Biteko akifafanua jambo kwenye uzinduzi huo.
Katibu Mkuu wa Wizara
ya Madini, Simon Msanjila akitoa taarifa ya uzalishaji wa madini nchini kwenye
uzinduzi huo.
No comments:
Post a Comment