Monday, February 11, 2019

Mlolongo wa kodi sekta ya madini kuondolewa-Biteko


Na Samwel Mtuwa, Mwanza

Mchakato wa kuondoa Mlolongo wa Kodi na Tozo kwa wachimbaji Wadogo wa Madini upo katika hatua za mwisho na ndani ya muda mfupi ujao, baadhi ya kodi na tozo hizo zitafutwa katika Sekta ya Madini.

Hayo yamesemwa Februari 11, 2019 na Waziri wa Madini Doto Biteko wakati akifungua Warsha kuhusu namna ya kuanzisha masoko ya madini nchini inayofanyika Jijini Mwanza.

Warsha hiyo inayolenga katika kutoa elimu ya namna ya kuanzisha masoko ya madini imeanza leo na itafanyika kwa siku mbili hadi Februari 12, 2019 ikiwashirikisha Wakuu wa Wilaya, Makatibu Tawala, Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa na Wawakilishi wa Wachimbaji Wadogo.

Waziri Doto ameeleza, warsha hiyo ni muhimu kwa wizara  nan  nchi kwa ujuml kutokana na  lengo ililojiwekea wizara hivi sasa ya kuhakikisha mchango wa sekta ya madini kwenye Uchumi na maisha ya wananchi unaongezeka.

Ameongeza kuwa, ana imani kwamba kwa kuondoa baadhi ya tozo na kodi kwa wachimbaji wadogo zitawezesha kuziba mianya ya utoroshaji wa madini na hivyo kuongeza mchango wa sekta ya madini kwenye pato la taifa.

Waziri Biteko amefafanua kuwa, Mchakato wa kuandaa Kanuni za Masoko ya madini umezingatia mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na kujifunza kutoka nchi zenye masoko ya madini.

Ameeleza kuwa, Halmashauri zinaowajibu wa kuendelea kuwajenga, kuwalea, na kuwawezesha wachimbaji wadogo kwa sababu mazao yao ndio yanayotegemewa kuuzwa katika masoko hayo.

Ametaka njia pekee ya kujibu na kutolea ufanunuzi wa taarifa potofu ni kutumia maelekezo yaliyopo katika sheria ya Madini ya 2010 na Marekebisho yake ya 2017.

“Pamoja na changamoto zilizopo kwenye usimamizi wa  sekta ya Madini nchini namshukuru Mungu kwani rasilimali hizi hazijageuka kuwa balaa,” amesema Biteko.

Katika hatua nyingne, amesema kuwa, Maafisa madini watakaokuwa kikwazo katika uanzishwaji wa masoko ya madini watachukuliwa hatua za kisheria.

Wadau katika warsha hiyo ni kutoka Mikoa ya Mwanza Dodoma, Arusha, Geita, Shinyanga, Mara, Manyara, Kagera, Tabora, Singida, Mbeya, Morogoro,na Ruvuma.

Warsha hiyo imeandaliwa na wizara ya Madini kwa ushirikiano na Taasisi ya Uongozi.


Waziri wa Madini Doto Biteko katika picha ya pamoja na wadau wanaoshiriki Warsha ya kuanzisha masoko ya Madini Nchini. 

Waziri wa Madini Doto Biteko akiteta jambo na baadhi ya Watendaji Waandamizi wa Wizara na Wadau wa warsha hiyo, mara baada ya kuifungua. 

Waziri wa Madini Doto Biteko katika picha ya pamoja na wadau wanaoshiriki Warsha ya kuanzisha masoko ya Madini Nchini.

No comments:

Post a Comment