Friday, February 8, 2019

Naibu Waziri Nyongo afungua warsha kujadili mpango ufungaji migodi


Na Nuru Mwasampeta, Dodoma

Kufuatia kutokuwepo kwa mwongozo wa ufungaji wa migodi pindi shughuli za uchimbaji zinapofikia kikomo, Wizara ya Madini kupitia Tume ya Madini imeandaa rasimu ya mwongozo ambayo inajadiliwa na wadau kutoka Taasisi za Kiserikali na wadau mbalimbali wa madini zikiwemo makampuni za uchimbaji kutoka Chamber of Mine.

Akifungua warsha ya kujadili rasimu hiyo, Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo, amewataka washiriki na waalikwa wote kufanya kazi hiyo kwa weledi mkubwa ili kuuboresha mwongozo huo.

Amesema, mwongozo huo utawasaidia wawekezaji watakaokuwa na nia ya kuwekeza nchini kujua taratibu na namna wanavyopaswa kufanya pindi wanapoandaa mpango wao wa kufunga mgodi ambao kwa mujibu wa taratibu, unapaswa kuwasilishwa serikalini kabla ya kuanza shughuli za uchimbaji nchini.

Kwa mujibu wa Kanuni ya 206 ya Sheria ya Madini ya 2010 kama ilivyorekebishwa mwaka 2107, kila mmiliki wa leseni ya uchimbaji wa madini wa kati na mkubwa anatakiwa kuandaa mpango wa ufungaji migodi na kuwasilisha kwa Mkaguzi Mkuu wa leseni ambaye ataandaa mkutano wa kamati ya kitaifa ya ufungaji migodi ambayo hupitia, kuujadili na kupitisha mpango huo.

Naibu Waziri Nyongo ameongeza kuwa, Mpango huo wa ufungaji wa migodi unaeleza kwa kina namna migodi itakavyofungwa na kurudisha eneo katika hali inayoweza kufaa kwa matumizi mengine.

Aidha, amesema kuwa, mipango hiyo huelezea namna wamiliki wa migodi watakavyowawezesha wafanyakazi pamoja na jamii inayozunguka eneo la migodi waliokuwa wakifanya kazi katika migodi hiyo pindi migodi hiyo inapofungwa.

Amesema mwongozo huo utaweka wazi namna bora ya kuandaa mpango wa kufunga mgodi pamoja na kuhifadhi mazingira kwa mujibu wa Sheria ya Madini na Sheria nyingine zinavyoelekeza.

Naibu Waziri, Nyongo amesema anatarajia mpango huo uendane na mazingira ya Tanzania na mwongozo ikiwemo kuhakikisha kuwa unajali vizazi na vizazi vitakavyofuata baada ya madini kuisha na kusema “Lazima tujue kwamba kuna vizazi vitakavyokuja baadaye, madini tunayo ni rasilimali yetu, lakini lazima tujue kuna vizazi vingine vinakuja,”

Ameongeza kuwa, uchimbaji unaendana na uharibifu wa mazingira, lakini ni lazima kuwaza namna ambavyo vizazi vinavyokuja vitakavyoishi.

Amebainisha kuwa, hatua hiyo ni muhimu ambayo kama taifa linategemea kikao hicho kiwe na manufaa kwa taifa la leo na vizazi vijavyo.

Akizungumza na washiriki wa warsha hiyo inayofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Chuo cha Ufundi (Veta) kwa siku mbili, Nyongo ameupongeza uongozi wa Tume ya Madini kwa hatua nzuri waliyoifikia katika kuandaa mwongozo huo.

Aidha, nyongo amesema Tume ya Madini kwa kushirikiana na Wizara ya Madini kupitia mradi wa Usimamizi Endelevu wa Rasilimali Madini (SMMRP), iliandaa rasimu ya kwanza ya mwongozo wa huo ambao unajadiliwa na wajumbe hao ili wamekutana ili kupata mwongozo unaokubalika kwa taifa.

Aidha, Nyongo ameeleza kuwa, maoni yaliyotolewa na wadau kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli wakati wa Mkutano wa kisekta uliofanyika mwezi Januari, yanafanyiwa kazi na hivyo kuahidi kuwa wadau wa madini na taifa watapata mrejesho wa kile kilichowasilishwa.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya ufunguzi wa warsha hiyo, Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Migodi na Mazingira kutoka Tume ya Madini, Dkt. Abdurahman Mwanga amesema katika nchi mbalimbali duniani suala la ufungaji wa migodi limekuwa ni gumu, hivyo, mwongozo unaoandaliwa utaonesha nini hasa kinapaswa kufanyika mara baada ya mgodi kufungwa.

Kwa upande wake, Meneja Mkuu wa Mgodi wa Neoroika, Honest Mrema, ulioko katika mkoa wa Songwe unaomilikiwa na Shanta mining, amesema rasimu hiyo ni nzuri na imetoa nafasi nzuri kwa wadau kukaa meza moja na watendaji wa serikali kujadili changamoto zinazowakabili kuhakikisha wanapochimba wanapata kile wanachotarajia.

Aidha, amebainisha kuwa, madini ni rasilimali, na pindi yanapochimbwa kuna uharibifu unatokea hivyo katika uharibifu kurudisha mazingira katika hali yake ya kawaida ni kuifanyia ardhi hivyo masuala muhimu.

Akielezea umuhimu wa maandalizi ya mwongozo huo, Mwenyekiti wa Chama cha Wanawake Wachimbaji Madini (TAWOMA), Eunice Negele, amesema rasimu inayojadiliwa itaisaidia jamii pamoja na vizazi vijavyo kwa kuwa, itawafanya wawekezaji kuhakikisha wanaiacha ardhi yenye kufaa kwa matumizi mengine tofauti na uchimbaji.


Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Migodi na Mazingira, Dr. Abdurahman Mwanga akiwasilisha rasimu ya ufungaji wa migodi kwa wadau waliojumuika kwa lengo la kuiboresha. 

Kamishna Msaidizi wa migodi na Maendeleo ya Madini Ali S. Ali akijitambulisha kabla ya ufunguzi wa warsha ya maandalizi ya mwongozo wa ufungaji wa migodi unaofanyika kwa siku mbili katika ukumbi wa VETA jijini Dodoma. 

Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (wa kwanza kushoto) akifuatana na Katibu Mtendaji wa Tume ya madini, Prof. Shukrani Manya na Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Migodi na Mazingira, Dr. Abdurahman Mwanga wakati wa ufunguzi wa warsha ya kuandaa mwongozo wa ufungaji wa migodi inayofanyika katika ukumbi wa VETA jijini Dodoma. 

Wadau mbalimbali wa madini walioshiriki katika warsha ya maandalizi ya mwongozo wa ufungaji wa migodi unaofanyika kwa siku mbili katika ukumbi wa VETA jijini Dodoma wakimsikiliza Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Migodi na Mazingira, Dr. Abdurahman Mwanga akiwasilisha rasimu hiyo tayari kwa majadiliano. 

Wadau mbalimbali wa madini walioshiriki katika warsha ya kujadili rasimu ya mwongozo wa ufungaji wa migodi inayofanyika kwa siku mbili katika ukumbi wa VETA jijini Dodoma.

No comments:

Post a Comment