Wednesday, February 27, 2019

Leseni za migodi mikubwa kutolewa karibuni


Na Asteria Muhozya, Dodoma

Serikali kupitia Wizara ya Madini inakamilisha taratibu za utoaji wa Leseni kwa Migodi Mikubwa ambazo hazijawahi kutolewa nchini, huku migodi hiyo ikitarajiwa kuanzishwa hivi karibuni.

Hayo yamebainishwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini Prof. Simon Msanjila alipokutana na viongozi wa Jumuiya ya Watendaji Wakuu wa Taasisi Binafsi ofisini kwake, jijini Dodoma.

Viongozi hao walikutana na Prof. Msanjila Februari 26, kwa lengo la kujitambulisha, kuelewa shughuli za serikali upande wa sekta ya madini, kupata uelewa kuhusu mabadiliko ya Sheria ya Madini na namna pande hizo mbili zinavyoweza kushirikiana katika kuendeleza sekta husika.

Prof. Msanjila aliwakaribisha viongozi hao kwenye sekta ya madini huku akiwataka kuzishawishi kampuni mbalimbali kuwekeza nchini hususani katika shughuli za uongezaji thamani madini na kueleza kuwa, suala hilo ni miongoni mwa maeneo ambayo serikali inayapa kipaumbele ikiwemo ujenzi wa vinu vya kusafisha na kuyeyusha madini.

Akizungumzia Sheria Mpya ya Madini ya Mwaka 2017, Prof. Msanjila amesema hakuna tatizo lolote katika utekelezaji wa sheria na kueleza kuwa, serikali kupitia wizara ya madini inapokea wawekezaji wengi wenye utayari na nia ya kuwekeza nchini huku utekelezaji wa sheria hiyo ukiwa si kikwazo na kuongeza kwamba, “hakuna mahali ambapo serikali inatengeneza sheria kwa ajili ya kumkandamiza mfanya biashara”.

“Hakuna tatizo lolote kwenye sheria ya madini. Hata wageni huwa tunakaa nao tunawaelimisha na wanatuelewa vizuri.  Kama kuna dosari ni vitu ambavyo tunaweza kuvirekebisha na tayari tumekwishakufanya hivyo kwa baadhi ya maeneo,” alisema Prof. Msanjila.

Aidha, katika kikao hicho Prof. Msanjila alitoa ushauri kwa viongozi hao kujitangaza zaidi kuhusu kazi zao huku akiwataka kutafuta wasaa kwa ajili ya pande hizo mbili kukutana ili wizara iweze kutoa elimu zaidi kwa Jumuiya hiyo kuhusu sekta ya madini ikiwemo fursa za uwekezaji zilizopo.

Pia, Prof. Msanjila alisema kuwa suala la kuaminiana linaweza kujengwa huku akiwataka watanzania kuwa wazalendo na namna wanavyotumia fedha za umma. Prof. Msanjila alizungumzia jambo hilo baada ya mmoja wa viongozi hao kueleza kuwa, bado kuna hali ya kutokuaminiana baina ya serikali na taasisi binafsi.

Kwa upande wake, mmoja wa viongozi wa jumuiya hiyo, Francis Nanai ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mwananchi Communications Limited amemweleza Prof. Msanjila kuwa, kama viongozi wa umoja huo, wamezipokea changamoto zilizotolewa kwao na Prof. Msanjila ikiwemo ushauri wa kukutana na wizara kwa lengo la kupata ufafanuzi na elimu  zaidi  kuhusu sekta ya madini.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini Prof. Simon Msanjila (kulia) akizungumza jambo wakati wa kikao baina yake na Viongozi wa Jumuiya ya Watendaji Wakuu wa Taasisi Binafsi. Kushoto ni mmoja wa viongozi hao. 

Mmoja wa Viongozi wa Jumuiya ya Watendaji Wakuu wa Taasisi Binafsi akizungumza jambo katika kikao hicho. Kulia ni Kamishna Msaidizi wa Wizara ya Madini, Godfrey Nyamrunda. 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini Prof. Simon Msanjila  wakijadiliana jambo na baadhi Viongozi wa Jumuiya ya Watendaji Wakuu wa Taasisi Binafsi. 

Mmoja wa viongozi wa jumuiya Jumuiya ya Watendaji Wakuu wa Taasisi Binafsi, Francis Nanai ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mwananchi Communications Limited, akizungumza jambo. 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini Prof. Simon Msanjila katika picha ya pamoja na Viongozi wa Jumuiya ya Watendaji Wakuu wa Taasisi Binafsi.

No comments:

Post a Comment