Na Nuru Mwasampeta,
Waziri wa Madini,
Doto Biteko amewatoa hofu Wawekezaji wa Nje na kueleza kuwa, Mabadiliko yaliyofanywa
katika Sheria ya Madini ya Mwaka 2017, hayana lengo la kuwakandamiza isipokuwa
yamelenga katika kuifanya rasilimali madini kuwanufaisha wote, wawekezaji na
watanzania.
Aliyasema hayo Januari
4, 2019 katika kikao baina yake na Balozi wa Canada nchini Pamela O’Donnel, ambacho
pia kilihudhuriwa na Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo, Kamishna wa
Madini, Mhandisi David Mulabwa, Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Mipango,
Augustine Ollal.
Akielezea lengo la
kuonana na uongozi wa juu wa Wizara, Balozi O’Donnel alisema amefika ili kupata
uelewa wa mabadiliko mbalimbali yaliyotokea katika sekta ya madini pamoja na
maeneo mengine ili kuwatoa hofu wawekezaji kutoka katika taifa lake wanaopenda
kuwekeza nchini.
Pamoja na nia yake ya
kupata ufumbuzi kwa masuala ya Sheria ya Madini, Balozi O’Donnel alihoji kuhusu
masuala mengine ikiwemo utawala wa kisheria, mikataba ya madini, kodi na tozo mbalimbali
pamoja na upatikanaji wa vibali vya kufanya kazi nchini kwa wananchi kutoka
nchini Canada.
Akijibu hoja hizo,
Waziri Biteko aliwataka wawekezaji kutoka nchini Canada kutokuwa na wasiwasi kwa
mabadiliko hayo na kuwataka kutembelea ofisi ya madini ili kupata ufafanuzi wa
jambo lolote lenye utata katika kufanikisha nia njema ya kuwekeza nchini. “Tupo
kwa ajili yao, wasisite kupata ufafanuzi wa jambo lolote linalohusu sekta ya
madini,” alisisitiza.
Aliongeza kuwa,
mataifa mbalimbali duniani yanafanya mabadiliko katika masuala mbalimbali na
kueleza kuwa, si vibaya kwa Tanzania kufanya mabadiliko kwa jambo lolote ambalo
lina manufaa kwa taifa.
Waziri Biteko
alieleza kuwa, madini ni rasilimali inayokwisha, hivyo ni muhimu madini yanapochimbwa
yawaletee faida watanzania na pindi yatakapokwisha wajivunie rasilimali madini
iliyokuwepo kutokana na maendeleo yaliyoletwa na Madini hayo kama vile barabara
bora, shule, ujenzi wa vituo vya Afya na masuala mengine ya maendeleo.
“Sheria ya awali
ilikuwa hainufaishi taifa na watanzania ndio maana mabadiliko yanafanyika.Mabadiliko
ni kitu kizuri, tunahitaji rafiki atakayesababisha mabadiliko kutokea hivyo
hawana haja ya kuogopa, tunawakaribisha kuwekeza” alisisitiza Biteko.
Akifafanua zaidi, Biteko
alieleza kuwa, mabadiliko ya sheria ya madini yamekuwa yakifanyika kulingana na
sera inayoongoza. Alieleza kuwa tangu kutungwa kwa sheria ya madini mwaka 1998
mabadiliko yamefanyika kwa awamu mbili yaani mwaka 2010 na mwaka 2017 lengo
likiwa ni moja tu, rasilimali madini iweze kulinufaisha taifa na Watanzania.
Aidha, alibainisha
kuwa mabadiliko ya kisheria yanayotokea katika sekta ya madini yanapitia
mchakato wa kutosha kwa kuwashirikisha wadau mbalimbali wa sekta na hayatokei
kwa ghafla kama inavyozungumzwa.
Waziri Biteko alisema
serikali imekusudia kuziwezesha benki za ndani kukua na hivyo kuwataka
wawekezaji kutunza fedha zao katika benki za ndani na endapo wawekezaji
watataka kutunza fedha zao katika benki za nje watumie benki zenye usajili
nchini Tanzania.
Kuhusiana na suala la
upatikanaji wa vibali kwa wataalamu wa kigeni kufanya kazi nchini, Biteko alifafanua
kuwa, Serikali haizuii wataalamu kutoka
nje kufanya kazi nchini isipokuwa kuwepo uwazi na uwajibikaji na Serikali
ikijiridhisha na kubaini kuwa nchini
hakuna mtaalamu wa kufanya kazi fulani serikali haitasita kutoa kibali kwa watu
kutoka nje ya nchi kuja kufanya kazi nchini.
Kwa upande wa utawala
wa kisheria, Biteko alikiri kuwa Serikali ya Awamu ya Tano inaongoza nchi kwa
Sheria na taratibu bila kuchagua wala kubagua.
Biteko alitanabaisha
kuwa kutokana na ukweli kwamba wapo watu ambao wamejikita katika kuamini
mitazamo hasi na hawataki ukweli ni suala gumu kubadili mitazamo yao, na
kueleza kuwa, itakuwa rahisi kwa wale watakaokubali ukweli na kubadili mitazamo
hasi waliyonayo juu ya serikali ili kwenda sambamba.
Kwa upande wake,
Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo alisema, wawekezaji ni wadau muhimu wa
maendeleo na hakuna taifa lolote lililo tayari kuwakatisha tamaa wadau wa
maendeleo.
Aidha, alibainisha mambo
manne yaliyopelekea Sheria ya Madini kufanyiwa marekebisho ili kukidhi matakwa
ya taifa na watu wake kwa ujumla na kusema kuwa mambo hayo ni pamoja na kuongeza
mapato kwa taifa kwa kuongeza mrabaha wa madini ya vito na almasi kutoka
asilimia 5 mpaka asilimia 6.
Alisema, suala
lingine ni uongezaji thamani wa rasilimali madini inayopatikana nchini ili inaposafirishwa
nje ya nchi iwe ya viwango vyenye ubora mkubwa na hivyo kusaidia kuongeza
mapato kwa taifa. Aidha, amebainsha kuwa kuna baadhi ya madini kama ya graphite
yanayoongezwa thamani kwa asilimia 90 na kusafirishwa nje ya nchi kuongezewa
ubora zaidi.
Akifafanua hilo,
Nyongo alisema ili kulipelekea taifa kuwa na viwanda vya kutosha, serikali
imefanya mabadiliko hayo ili kupata wawekezaji watakaojenga viwanda vya
kuchakata madini nchini ili yasafirishwe yakiwa katika viwango bora na
kupelekea ongezeko la fedha za kigeni nchini.
Pia, Naibu Waziri
Nyongo alizungumzia suala la uwajibikaji wa wawekezaji kwa jamii ya kitanzania na
kusema kuwa, ili kuwafanya wawekezaji kuwatumia wazawa katika kufanikisha
shughuli za uchimbaji na biashara ya madini, Sheria mpya imeweka wazi masuala
mbalimbali yanayopaswa kufanywa na wazawa na manunuzi ya baadhi ya mahitaji
kufanyika ndani ya nchi na si vinginevyo ikiwa ni pamoja na kuajili wazawa.
Mwisho Naibu Waziri
Nyongo alizungumzia suala la kuzuia wawekezaji kumiliki leseni wasizozifanyia
kazi. Alisema kuwa, wapo baadhi ya wawekezaji wamekuwa wakitumia leseni
za madini kuombea mikopo katika taasisi
za kifedha nje ya nchi na baada ya kupata mikopo hiyo wamekuwa wakiendesha shughuli zao nje ya Tanzania.
Alibainisha kuwa, ili
kuwabana wawekezaji hao sheria imekuja ikiweka wazi muda maalum wa mmiliki wa
leseni kumiliki leseni hiyo vinginevyo maeneo yanarudishwa serikalini ili kutoa
fursa kwa watu wenye nia ya kufanya kazi kuendelea na kazi.
Waziri wa Madini,
Doto Biteko (kulia) akifuatiwa na Naibu Waziri Stanslaus Nyongo wakiwa katika
kikao kifupi na Balozi wa Canada nchini Pamela O’Donnel. Kushoto ni Kamishna wa
Madini nchini Mhandisi David Mulabwa.
Waziri wa Madini,
Doto Biteko (kulia) akiagana na Balozi wa Canada nchini mara baada ya kumaliza
kikao baina yao. Katikati ni Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo.
|
Waziri wa Madini,
Doto Biteko (kushoto), akizungumza jambo wakati wa kikao na Balozi wa Canada
nchini Pamela O’Donnel (wa pili kutoka kushoto).
|
Waziri wa Madini,
Doto Biteko (kushoto), Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Mipango (Kulia), katikati
ni Katibu wa Waziri Kungulu Masakala wakifuatilia hoja kutoka kwa Balozi wa
Canada nchini Pamela O’Donnel (Hayupo pichani)
|
No comments:
Post a Comment