Monday, January 21, 2019

Madini kufanya mazungumzo barabara mgodi wa Makaa, Ngaka


Na Asteria Muhozya, Mbinga

Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo amesema Wizara yake itafanya mazungumzo na  Mamlaka zinazohusika na masuala  ya barabara ili kuweka mazingira bora ya miundombinu hiyo  kwa lengo la  kuwezesha biashara ya makaa ya mawe na shughuli za uzalishaji makaa hayo kufanyika kwa ufanisi zaidi katika mgodi wa makaa ya mawe  Ngaka, uliopo wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma.  

Alisema mgodi huo wa Ngaka chini ya kampuni ya TANCOAL ndiyo taswira ya uzalishaji makaa ya mawe nchini hivyo, serikali haina budi kuweka mazingira bora yatakayowezesha kupunguza gharama za uendeshaji jambo ambalo litapunguza gharama kwa walaji wa nje na ndani ikizingatiwa kuwa, ni kampuni ya Kimataifa kutokana na kuhudumia wateja kutoka nchi mbalimbali zikiwemo Rwanda, Burundi, Uganda nchi na nyingine.

Kauli ya Naibu Waziri Nyongo inafuatia changamoto ya barabara iliyowasilishwa kwake na Meneja Mgodi wa TANCOAL Mhandisi David Kamenya, ambaye alimweleza Naibu Waziri kuwa, ukosefu wa miundombinu imara ikiwemo madaraja imechangia shughuli za upakiaji makaa hayo kutokuzidi tani 20 kwa kila gari jambo ambalo linapelekea kuwepo na foleni kubwa  kutokana na uhitaji wa makaa hayo.

Naibu Waziri Nyongo alifanya ziara mgodini hapo Januari 17 ikilenga kukagua shughuli za madini mkoani Ruvuma pamoja na kuangalia changamoto mbalimbali ambazo mgodi huo unakabiliana nazo katika utekelezaji wa shughuli zake.

Pamoja na kuridhia ombi hilo, Naibu Waziri aliitaka kampuni hiyo kuongeza kasi ya uzalishaji kutokana na mahitaji makubwa ya bidhaa hiyo katika soko la nje na ndani na kuitaka kutobweteka huku ikitakiwa kuboresha huduma inazotoa ikiwemo kuongeza vifaa vya kazi.

“Nimeona changamoto ya barabara. Kama serikali ni lazima tuifanyie kazi changamoto hii ili kuwezesha uzalishaji zaidi wa makaa. Sisi tutaendelea kutoa leseni kwa wazalishaji wengine ili kuweka ushindani, hivyo msibeweteke, tunahitaji sana makaa haya kwa uchumi wa taifa letu kwa kuwa tunayo hazina ya kutosha ya rasilimali hii,” alisema Nyongo.

Aliongeza kuwa, kufuatia serikali kuweka zuio la uingizaji makaa kutoka nje, ni lazima kuweka mazingira bora ya uzalishaji wa madini hayo ikiwemo kuwezesha biashara hiyo   na kuutaja mgodi wa makaa ya mawe wa Kabulo unaomilikiwa na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) kuwa ni eneo jingine ambalo miundombinu ya barabara ni lazima iboreshwe kuwezesha  ufanisi zaidi wa shughuli za uzalishaji madini hayo.

Alisema kuwa, ili serikali iendelee kupata mrabaha zaidi kutokana na rasilimali hiyo suala hilo lazima lichukuliwe kwa uzito ili kuongeza mapato zaidi.

Aidha, akijibu ombi la kampuni hiyo kutaka kurudishiwa eneo ambalo lilitolewa kwa ajili ya Kiwanda cha Dangote na Rais John Magufuli, kwa kuwa bado haijanza kuchimba mpaka sasa, Naibu Waziri Nyongo alizitaka pande zote ikiwemo wizara na kampuni hizo kukutana Januari 22 mara baada ya kikao cha wadau wa sekta ya madini ili kujadili suala hilo ili hatimaye shughuli za uzalishaji zianze katika eneo hilo.

Mbali na hilo, kampuni hiyo ilimwomba Naibu Waziri kuwezesha upatikanaji  wa leseni mbili zilizoombwa na kampuni hiyo ikilenga kutumia makaa hayo kuzalisha umeme  kwa ajili ya matumizi ya mgodi. Naibu Waziri aliahidi kuwa, kupitia Tume ya Madini, suala hilo litakuwa limekamilika ndani ya kipindi cha wiki mbili.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri Nyongo aliitaka Halmashauri ya Mbinga kubuni miradi kwa ajili ya vijana na wanawake yenye lengo la kuhamasisha matumizi ya makaa ya mawe kwa ajili ya matumizi ya majumbani na kuachana na matumizi ya mkaa kwa kuwa umekuwa ukisababisha uharibifu wa mazingira.

Wakati huo huo, akizungumzia suala la Mrabaha wa serikali  wa asilimia 3, alisema usilipwe kwa bei ya maeneo ya uchimbaji   bali ulipwe kwa bei ya sokoni. Hivyo, aliwataka wazalishaji wote na Maafisa wa Tume ya Madini kuhakikisha wanatoza bei ya sokoni na siyo ya uzalishaji.

Kwa upande wake, Meneja wa  mgodi  Mhandisi  David  Kamenya akizungumzia ubora wa makaa hayo, alisema kuwa, Makaa ya Ngaka yana ubora wa kimataifa  na ndiyo sababu imepelekea kupata wateja wengi kutoka nchi mbalimbali na kuongeza kwamba makaa hayo yana uwezo wa kufanya matumizi mbalimbali na kuongeza kuwa, kwa siku kampuni hiyo inapakia idadi ya magari yapatayo 100.

AKizungumzia malengo ya baaaye, alisema kuwa, idadi ya mashine ndani ya siku chache zinatarajiwa kuongezwa na kwamba kampuni imelenga kuzalisha hadi tani 5,000 kwa siku kutoka 3,000 za sasa.

Akizungumzia uwezeshaji kwa vijana na akina mama, alisema kuwa, tayari kipo kikundi cha wakina Mama cha Mbarawala ambacho kimewezeshwa na  mgodi huo kwa kupatiwa mafunzo  ya namna ya kuandaa makaa hayo maalum kwa matumizi ya majumbani na kuongeza kuwa, hivi karibuni kikundi hicho kimepata  Cheti cha ubora kutoka shirika la Viwango nchini (TBS) jambo ambalo litawezesha kikundi hicho kuuza  makaa yake kwa ajili ya matumizi ya majumbani na hivyo kupunguza matumizi ya mkaa unaotokana na kukatwa miti.

Pia, Mhandisi Kamenya alimweleza Naibu Waziri Nyongo kuwa, mbali na kupatiwa mafunzo kikundi hicho pia kimepatiwa mashine ambayo inauwezo wa kuzalisha tani mbili za makaa hayo kwa saa.

Akishukuru kwa niaba ya kikundi, Meneja Usimamizi wa Mbarawala, Joyce Haule alisema kuwa,  wanaishukuru kampuni hiyo kwa kuwawezesha na  kwamba kikundi kinalenga kuzalisha tani 10 kwa siku na kuongeza kuwa, hadi sasa tayari kimepata wateja kutoka maeneo mbalimbali zikiwemo nchi za Rwanda ambao  awali walitaka kwanza kikundi hicho  kuwa na cheti cha ubora wa makaa hayo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Mbinga, Cosmas Ishenyi alimweleza Naibu Waziri kuwa, kama Wilaya itahakikisha kuwa, inashirikiana na mamlaka zinazohusika kuweka mazingira bora ya kuwezesha mundombinu bora ya barabaraba  ili TANCOAL iweze kufanya shughuli zake kwa ufanisi zaidi.

Katika hatua nyingine, akizungumza na Katibu Tawala Mkoa wa Ruvuma, Prof. Riziki Shemdoe, ofisini kwake Januari 18, Naibu Waziri alimweleza Prof. Shemdoe umuhimu wa kuwezesha miundombinu ya barabra kuelekea katika mgodi huo wa Ngaka.

Pia, Naibu Waziri alimweleza Prof. Riziki kuhusu mipango ya Serikali ya kuwa na vituo kwa ajili ya biashara ya madini na umuhimu wa mikoa kutenga maeneo kwa ajili ya shughuli hizo. “ Tunataka kuwa na utaratibu wa kuwa na maeneo ya kuuza na kununua madini ili kuwa na  utaratibu maalumu,” aliongeza.

Kwa upande wake, Prof. Shemdoe alimwomba Naibu Waziri kusaidia upatikanaji wa wawekezaji kwa ajili ya viwanda vya kuchenjua dhahabu mkoani humo na kukumbushia suala la uchimbaji madini katika Mto Muhuwesi.

TANCOAL ni kampuni yenye ubia na Serikali kupitia Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) ambapo serikali inamiliki hisa kwa asilimia 30.

Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo (wa tatu kushoto) akiongozwa na Meneja wa mgodi wa  Makaa ya Mawe TANCOAL, David  Kamenya  (aliyenyoosha mikono) kutembelea maeneo  ambapo uchimbaji wa makaa hayo unafanywa katika machibo yaliyopo Wilayni Mbinga mkoa wa Ruvuma.

Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo akieleza jambo baada ya kutembelea eneo ambalo shughuli za upakiaji makaa ya mawe zinafanywa na mgodi wa TANCOAL kwa ajili ya makaa hayo kusafirishwa maenezo mbalimbali ndani na nje ya nchi.

Baadhi ya magari yakisubiri kupakia makaa ya mawe tayari kwa kusafirishwa maeneo mbalimbali ndani nan je ya nchi,

Sughuli za upakiaji Mkaa ya Mawe zikiendelea katika Mgodi wa TANCOALtayari kwa ajili ya kusafirishwa maeneo mbalimbali.

Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo katika picha ya pamoja na baadhi ya wafanyakazi wa mgodi wa Makaa ya Mawe wa TANCOAL. Wengine ni baadhi ya Wataala kutoka ofisi ya Madini Songea na baadhi viongozi wa wachimbaji wadogo  Mkoa wa Ruvuma.

No comments:

Post a Comment