Monday, January 21, 2019

Maafisa madini watakiwa kutobagua Migodi


Na Asteria Muhozya, Mbinga

Maafisa Madini nchini wametakiwa kutobagua migodi midogo kwa kuelekeza nguvu kwenye migodi mikubwa  tu  huku wakisisitizwa kutatua migogoro kwenye maeneo yao ya kazi na kuelezwa kuwa,  watakaobainika wakibagua migodi hiyo na kutotatua migogoro wataondolewa  kwenye nafasi zao.

Hayo yalibainishwa Januari 17 na Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo wakati  akizungumza na wachimbaji wadogo wa madini aina ya Sapphire wakati wa  ziara yake katika kijiji cha Masuguru, Wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma.

 Naibu Waziri Nyongo alifanya ziara hiyo ikilenga kukagua shughuli za uchimbaji madini wilayani humo pamoja na kusikiliza kero za wachimbaji katika migodi hiyo,  ambapo wachimbaji waliwasilisha kero za kutaka kutengewa maeneo kwa ajili ya shughuli za uchimbaji, bei elekezi za madini  ikiwemo kuunganishwa na  huduma ya umeme kwenye migodi yao.

Akizungumza kijijini hapo, alimtaka Afisa Madini mkoa wa Ruvuma hukakikisha anaishughulikia kero hiyo na kuitatua  mara moja na kuongeza kuwa, Rais wa Jamhuri ya Muungano anataka wachimbaji nchini wachimbe madini, hivyo,  maafisa madini   kote nchini wahakikishe wanashughulikia kero katika maeneo yao ya kazi ikiwemo kusuluhisha migogoro.

“Sisi ni matajiri, tumebarikiwa madini ya vito. Wachimbaji chimbeni lakini mchimbe katika maeneo yaliyoruhusiwa kuchimbwa”.alisisitiza.

Alisema kuwa, kama mgogoro ni mkubwa wapo viongozi wa vyama vya wachimbaji wahakikishe kuwa  wanafikisha migororo hiyo na kusema “tuleteeni na sisi lakini  usipoishughulikia migogoro hiyo tutakuondoa.
Aliongeza kwamba, serikali inalenga katika kuwatoa wachimbaji wadogo kutoka katika uchimbaji mdogo kwenda uchimbaji wa  kati na hatimaye mkubwa na ndiyo sababu inaendelea na ujenzi wa vituo vya umahiri  katika maeneo mbalimbali nchini ikilenga katika kutoa elimu ya uchimbaji bora, uchenjuaji bora, biashara ya madini na ujasiliamali ili kuhakikisha kwamba wachimbaji wadogo wanakua.

Aliongeza kuwa,  elimu  ya ujasiliamali ni muhimu kwa wachimbaji wadogo kwa kuwa itawaandaa kuwa na uchimbaji endelevu na wenye tija.

Akijibu ombi la ruzuku,  aliwataka wachimbaji wadogo kujiunga katika vikundi vidogo vidogo  ili iwe rahisi kwa wachimbaji hao kufikiwa  ikiwemo kupatiwa huduma za leseni, elimu, vifaa, kuwamilikisha, kuwapatia mikopo na  kuwafuatilia  jambo ambalo litapelekea wafanye kazi kwa urahisi na kwa kulipa kodi za serikali na  wao kubaki na kipato  kitakachowezesha maisha bora.

Alisema uwepo wa mazingira mazuri migodini utasaidia vijana kufanya kazi na hivyo kuwa na taifa lenye watu wanaofanya kazi.  Aliwataka maafisa madini wote kuhakikisha wanashughulikia migogoro ya wachimbaji wadogo na kueleza kwamba, endapo serikali itakuta migogogoro ya wachimbaji wadogo  katika maeneo yao wataondolewa.

Aliongeza kwamba, wizara imejipanga na tayari kuna baadhi ya maeneo yametengwa kwa ajili ya wachimbaji  na kuwasisisitiza kuhakikisha wanauza madini  wanayoyachimba katika maeneo rasmi.

Akizungumzia suala la broker, aliwataka kuhakikisha wanakuwa na leseni ya kufanya shughuli hizo ikiwemo vifaa vya kupimia madini na kuwataka kulipa kodi. Pia, aliwatahadharisha wachimbaji wanaoshirikiana na broker wasiokuwa  na leseni   kuacha kwani kwa kufanya hivyo ni kwamba  kwamba wote wanaliibia taifa.” Maafisa madini hakikisheni mnawajua ma broker wote  na wawe na leseni na walipe kodi, “ alisisitiza Nyongo.

 Akijibu ombi la  ruzuku lililowasilishwa  kwake,  alisema fedha za ruzuku zilizokuwa zikitolewa awali  hazikuwafikia walengwa wote  na kueleza kuwa, wapo waliopata ruzuku hizo lakini hawakuwa wachimbaji na kuongeza kwamba, hivi sasa wizara inaangalia namna bora ya kuwasaidia wachimbaji.

Kwa upande wake, Afisa Madini Mkoa wa Ruvuma  Abraham  Nkya alisema kuwa, mkoa huo tayari umetenga maeneo kwa ajili ya wachimbaji wadogo na kwamba watashirikiana na wachimbaji hao ili  suala hilo liweze kuwasilishwa Tume ya Madini kwa  ajili ya hatua zaidi.

Awali , kiongozi wa wachimbaji   aliwasilisha ombi kwa Naibu Waziri   la wachimbaji kupatiwa  ruzuku. Alisema mkoa huo umebarikiwa madini ya ujenzi, nishati, viwanda    huku eneo la Masuguru likibariwa madini ya Sapphire. Alisema eneo hilo liliombwa kwa ajjili ya uchimbaji mdogo lakini mpaka  sasa bado halijatengwa.

Pia, alisema ipo changamoto ya kukosekana elimu kwa watendaji vijijini ambao wamesababisha mgizo mkubwa wa kodi kwa wachimbaji.

Sehemu ya Wachimbaji Wadogo wa Madini ya Saphire wakiwa wameshika mabango yenye ujumbe Maalum kwa Naibu Waziri Stanslaus Nyongo baada ya kuwasili katika kijiji cha Masuguru  Wilaya ya Mbinga Mkoani Ruvuma.

Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo mwenye sweta (nyekundu) katika picha ya pamoja na baadhi ya wachimbaji wadogo wa madini ya Sapphire katika kijiji cha Masuguru Wiaya ya Mbinga mkoa wa Ruvuma

Mkuu wa Wilaya ya Mbinga Cosmas Ishenyi akizungumza jambo wakati wa  mkutano wa hadhara katika kijiji cha Masuguru. Katikati ni Naibu Waziri wa  Madini Stanslaus Nyongo.

Mmoja wa wachimbaji wananwake katika kijiji cha Masuguru akiwasilisha kero yake kwa Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo  na Mkuu wa  Wilaya ya Mbinga Cosmas Ishenyi ( hawapo  pichani) wakati  wa ziara ya viongozi hao kijijini hapo.

No comments:

Post a Comment