Monday, January 21, 2019

Kamati ya Bunge yaipongeza Wizara ukusanyaji maduhuli


Na Asteria Muhozya, Dodoma

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imeipongeza Wizara ya Madini kwa ukusanyaji maduhuli ambapo katika kipindi cha nusu Mwaka wa Fedha 2018/19, cha kuanzia mwezi Julai hadi 31 Disemba, 2018, ilikusanya shilingi 167,742,947,332 kati ya shilingi 310,598,007,000 iliyopangiwa.

Akiwasilisha taarifa kwa Kamati hiyo kwa niaba ya Katibu Mkuu, Kamishna wa Madini Mhandisi David Mulabwa, amesema kuwa, shilingi 310,320,0004,000 zilipangwa kukusanywa kupitia Tume ya Madini, na shilingi 278,003, 000 katika Makao Makuu ya Wizara na Chuo cha Madini Dodoma.

“ Mhe. Mwenyekiti, hivyo lengo la makusanyo kwa kipindi cha nusu mwaka Julai hadi Disemba 2018 ni shilingi 155,299,003,500. Hadi kufikia tarehe 31 Disemba, 2018, wizara ilifanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi 167,742,947,332 sawa na asilimia 108.01 ya lengo,” amesema Kamishna Mulabwa.

Akizungumzia juhudi za wizara katika kuvutia uwekezaji katika sekta ya madini, amesema wizara iliandaa kongamano la kutangaza fursa za uwekezaji katika sekta ya madini nchini lililojulikana kama China Tanzania mining Forum lililenga kutangaza fursa za uwekezaji zilizopo katika sekta ya madini nchini, ikiwemo kutafuta soko la madini hayo nchini China na kuangalia fursa za ushirikiano kati ya Wizara ya madini Tanzania na Wizara ya maliasili ya China.

“ Mhe. Mwenyekiti kongamano hilo pia lilitumika kuwakutanisha wachimbaji wa Tanzania na watengenezaji wa mitambo mbalimbali ambayo hutumika kwenye shughuli za uchimbaji na uchenjuaji wa madini,”amesema Kamishna Mulabwa.

Kamishna Mulabwa ameongeza kuwa, katika kongamano hilo jumla ya wachimbaji wadogo 40 na wakubwa 4 kutoka Tanzania walishiriki kongamano hilo.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo akijibu hoja za Kamati kuhusu suala la ukusanyaji wa maduhuli amesema bado Wizara haijaridhika na kiwango kilichokusanywa na kuongeza kuwa, kama wizara katika mipango yake yenyewe ya ndani, imepanga kukusanya zaidi ya kiwango cha bilioni 310 iliyopangiwa.

“ Mhe. Mwenyekiti sisi wenyewe ndani tumejiwekea malengo yetu ya kukusanya zaidi ya kiasi tulichopangiwa. Tunajiongeza tuongeze kiwango hicho sisi wenyewe.  Tunafanya hivyo ili mwakani hata kama tutaongezewa kiwango basi tuwe tayari tumekwisha jipanga,” amesisitiza Naibu Waziri Nyongo.

Akizungumzia udhibiti wa madini, amesema kuwa, Wizara inaendelea za jitihada na kudhibiti utoroshaji madini ambapo kwa upande wa madini ya tanzanite udhibiti unaendelea na kusema kuwa, kwa sasa madini hayo yanapita katika mfumo unaoeleweka.

“Kesho Januari 22, tutakuwa na mkutano wa Kisekta, watakuja wachimbaji na wafanyabiashara naamini watamweleza Mhe. Rais kero zao na tutasikia. “Lakini pia tumewaalika wakuu wa Mikoa ambayo shughuli za madini zinafanyika, tunataka kuweka mazingira mazuri kwa sekta.

Kuhusu changamoto za masoko ya madini, amesema wizara inataka kuhakikisha kwamba biashara ya madini inakuwa wazi na halali huku ikijipanga kukusanya zaidi kodi za serikali na kuongeza kuwa, wizara inajipanga kuweka mfumo mzuri wa soko la madini jambo ambalo litazinufaisha pande zote.

“ Mhe. Rais anataka tununue tuweke reserve. Lakini pia Serikali ikinunua kwa bei ya soko, hata wachimbaji watafurahi,” amesema Nyongo.

Akizungumzia suala la uhifadhi wa mazingira amesema kuwa wizara imeweka utaratibu wa pindi wawekezaji wanapoanzisha mgodi ni lazima waweke mpango wa namna watakavyofunga migodi huku suala la uhifadhi wa mazingira likipewa umuhimu wake.

Ameongeza kuwa, wizara inaweka mkazo kwa migodi kueleza mpango wa ufungaji migodi ambao utaacha mazingira yakiwa salama.

Wakizungumza katika kikao hicho kwa nyakati tofauti, wajumbe wa Kamati hiyo, licha ya kuipongeza wizara kwa ukusanyaji wa maduhuli, wameitaka wizara kuweka mikakati madhubuti katika suala uongezaji thamani madini kutokana na zuio la usafirishaji madini ghafi nje ya nchi.

Aidha, wajumbe hao wameitaka Wizara kuendelea kukiimarisha Kituo chake cha Jimolojia Tanzania (TGC) ili kuweza kutoa wataalam wa kutosha katika tasnia hiyo ya uongezaji tthamani madini.

No comments:

Post a Comment