Monday, November 26, 2018

Naibu Waziri Biteko atembelea Mgodi wa Buzwagi


Na Greyson Mwase

Leo tarehe 25 Novemba, 2018 Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko amefanya ziara katika Mgodi wa Dhahabu wa Buzwagi uliopo wilayani Kahama mkoani Shinyanga lengo likiwa ni kukagua shughuli za uchimbaji madini, kusikiliza na kutatua kero mbalimbali  zinazoukabili mgodi huo. Katika ziara hiyo Naibu Waziri Biteko aliambatana na  Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Anamringi Macha, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kahama,  Anderson Msumba, Katibu Tawala wa Wilaya ya Kahama, Timothy Ndaya,  Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Kahama, Mhandisi Abdulrahman Milandu, Afisa Mgodi Mkazi wa Mkoa wa Kahama, Modest Tarimo, Mkaguzi wa Migodi kutoka Tume ya Madini Mhandisi Frederick Mwanjisi,wataalam kutoka Wizara ya Madini, Tume ya Madini pamoja na waandishi wa habari.

 Mara baada ya  kufanya ziara na kupokea taarifa ya hatua za kufunga mgodi wa Buzwagi, Naibu Waziri Biteko alitoa  maagizo mbalimbali ikiwa ni pamoja na:- mgodi kuwasilisha upya mpango wa ufungaji wa shughuli zake kwa Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini ili aweze kuwasilisha kwenye Kamati ya Kitaifa ya Ufungaji wa Migodi  kwa ajili ya kuidhinishwa ili  utekelezaji wake uanze mara moja, pawepo na utaratibu wa kupitia upya kiwango cha fedha    zilizotengwa kwa ajili ya ukarabati wa mazingira (rehabilitation bond) na kuweka mkakati wa kuhakikisha kuwa shughuli za kiuchumi za wakazi wanaozunguka mgodi huo haziathiriki na ufungaji wa mgodi husika.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri Biteko aliutaka uongozi wa mgodi huo kufuata sheria na kanuni za ufungaji wa mgodi kwa wakati na kuepuka kufanya kazi kwa zimamoto.

Meneja Mkuu wa Migodi ya Dhahabu ya Buzwagi na Bulyanhulu, Benedict Buzunzu alisema kama mgodi wamepokea maelekezo na kuahidi kuwa watayafanyia kazi.


Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (kushoto) akimsikiliza Afisa Mgodi Mkazi wa Mkoa wa Kahama, Modest Tarimo ( wa pili kulia) mara alipowasili kwenye ofisi yake iliyopo katika eneo la Mgodi wa Dhahabu wa Buzwagi uliopo katika Wilaya ya Kahama Mkoani Shinyanga. Kulia ni Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Kahama, Mhandisi Abdulrahman Milandu. 

Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (wa tatu kulia mbele) pamoja na msafara wake wakiendelea na ziara katika Mgodi wa Dhahabu wa Buzwagi uliopo katika Wilaya ya Kahama Mkoani Shinyanga. 

Mtaalam kutoka Mgodi wa Dhahabu wa Buzwagi, Jonathan Joseph (kulia) akifafanua jambo kwa Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (wa pili kushoto). 

Sehemu ya Mgodi wa Dhahabu wa Buzwagi uliopo katika Wilaya ya Kahama Mkoani Shinyanga. 

Meneja Mkuu wa Migodi ya Dhahabu ya Buzwagi na Bulyanhulu, Benedict Buzunzu (kushoto) akielezea mikakati ya Mgodi wa Buzwagi kwenye ufungaji  wa shughuli zake kwa Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (kulia). 

Uchimbaji wa wazi wa dhahabu (open pit) ukiendelea katika Mgodi wa Dhahabu wa Buzwagi uliopo katika Wilaya ya Kahama Mkoani Shinyanga.

No comments:

Post a Comment