Monday, October 29, 2018

FEMATA kuimarisha sekta ya madini kupitia kodi


Na Greyson Mwase, Dodoma

Mtendaji Mkuu wa  Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Wadogo wa  Madini Nchini (FEMATA) na Kamishna kutoka Tume ya Madini, Haroun Kinega amesema kuwa, shirikisho hilo kwa kushirikiana na Serikali kupitia Wizara ya Madini limeweka mikakati katika kuhakikisha wachimbaji wadogo wanakuwa na mchango mkubwa kwenye ukuaji wa Sekta ya Madini kupitia kodi na tozo mbalimbali.

Kinega ameyasema hayo leo tarehe 29 Oktoba, 2018 katika mkutano mkuu wa uchaguzi wa viongozi wa FEMATA Nchini uliofanyika jijini Dodoma wenye lengo la kuchagua viongozi wapya pamoja na kujadili changemoto mbalimbali wanazokabiliana nazo kwenye shughuli za uchimbaji wa madini nchini.

Akielezea mikakati ya ongezeko la mapato kutokana na kodi zinazolipwa na wachimbaji wadogo wa madini, Kinega alisema kuwa FEMATA kwa kushirikiana na Tume ya Madini imeweka mikakati ya kuhakikisha maeneo zaidi yanatengwa na kutolewa leseni kwa ajili ya wachimbaji wadogo wa madini na kuwataka wachimbaji wadogo wa madini kuunda vikundi, kusajili ili kuomba leseni na uchimbaji wao kuwa rasmi.

“Lengo letu ni kuhakikisha kuwa asilimia kubwa ya wachimbaji wadogo wa madini nchini wanakuwa rasmi kwa kupatiwa leseni za madini ili kurahisisha ukusanyaji wa mapato ya serikali, ninaamini tunaweza kufikia lengo kupitia mikakati tuliyojiwekea.

Wakati huo huo akielezea mikakati ya Serikali katika kuwasaidia wachimbaji wadogo wa madini,  Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Dodoma,  Jonas Mwano alisema kuwa mbali na Serikali kupitia Wizara ya Madini kutenga maeneo kwa ajili ya wachimbaji wadogo wa madini, elimu imekuwa ikitolewa kwa wachimbaji wadogo kuhusu sheria na kanuni za uchimbaji wa madini pamoja na usalama migodini.

Alisema kuwa elimu ambayo imekuwa ikitolewa kwa  wachimbaji wadogo wa madini imepunguza kwa kiasi kikubwa migogoro iliyokuwa ikijitokeza kwenye maeneo yao ya uchimbaji wa madini.

Naye Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Wadogo wa  Madini Nchini (FEMATA), John Bina mbali na kupongeza juhudi zilizofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano kupitia Wizara ya Madini  aliiomba Serikali kuhamasisha wawekezaji kutoka nje kwa ajili ya kujenga mitambo ya kuchenjulia madini nchini na kukuza pato la taifa.

Katika uchaguzi huo wa viongozi wa FEMATA nafasi zinazogombewa ni pamoja na Rais, Makamu wa Rais,  Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu, Mweka Hazina, Mweka Hazina Msaidizi, Mwakilishi  wa Wanawake na Mwenyekiti wa Kamati ya Madini ya Dhahabu.

Nafasi nyingine ni pamoja na Mwenyekiti wa Kamati ya Madini ya Nishati, Mwenyekiti wa Kamati ya Madini ya Viwanda, Mwenyekiti wa Kamati ya Madini ya Chumvi, Mwenyekiti wa Kamati ya Madini ya Tanzanite, Mwenyekiti wa Kamati ya Madini ya Almas, Mwenyekiti wa Kamati ya Madini Mengine ya Vito na  Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili, Usuluhishi na Kanuni.

Aidha, Nafasi nyingine ni pamoja na Mwenyekiti wa Kamati ya Ujenzi, Mjumbe wa Afya, Mazingira na Usalama Migodini, Mwakilishi wa Wafanyabiashara, Mwakilishi wa Wachimbaji Wasio Rasmi, Mjumbe wa Mpango wa Kuongeza Uwazi na Uwajibikaji katika Rasilimali za Madini, Gesi na Mafuta (TEITI) na Bodi ya Wadhamini nafasi tano.


Mtendaji Mkuu wa  Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Wadogo wa  Madini Nchini (FEMATA) na Kamishna kutoka Tume ya Madini, Haroun Kinega (kushoto) akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya ufunguzi wa mkutano wa uchaguzi wa viongozi wa Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Wadogo wa Madini Nchini (FEMATA) uliofanyika tarehe 29 Oktoba, 2017 

Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Wadogo wa Madini Nchini (FEMATA), John Bina akielezea mafanikio ya shirikisho hilo mbele ya wawakilishi wa vyama vya wachimbaji wadogo wa madini mikoani (hawapo pichani) 

Sehemu ya wawakilishi wa vyama vya wachimbaji wadogo wa madini mikoani wakifuatilia hotuba iliyokuwa inatolewa na Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Wadogo wa Madini Nchini (FEMATA), John Bina (hayupo pichani) 

Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Dodoma, Jonas Mwano (kulia) akielezea mikakati ya Serikali kwenye uwezeshaji wa wachimbaji wadogo wa madini kwa waandishi wa habari. 

Sehemu ya wajumbe wa meza kuu wakifuatilia ufafanuzi uliokuwa unatolewa na Mtendaji Mkuu wa  Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Wadogo wa  Madini Nchini (FEMATA) na Kamishna kutoka Tume ya Madini, Haroun Kinega (hayupo pichani)

No comments:

Post a Comment