Monday, September 10, 2018

Profesa Kikula atoa mwezi mmoja utatuzi wa mgogoro wachimbaji madini Winza


Na Greyson Mwase, Dodoma

Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula ametoa mwezi mmoja kwa Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Wadogo wa Madini mkoani Dodoma (DOREMA), Kulwa Mkalimoto na Kaimu Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Dodoma, Nicas Sangaya kuhakikisha mgogoro katika machimbo ya madini aina ya rubi yaliyopo katika kijiji cha Winza kilichopo wilayani Mpwapwa mkoani Dodoma unamalizika ili wachimbaji hao waendelee na shughuli zao za uchimbaji madini na kujipatika kipato.

Profesa Kikula ametoa agizo hilo mara baada ya kupokea kero za wachimbaji wadogo wa madini katika eneo hilo katika ziara yake katika wilaya ya Mpwapwa yenye lengo la kukagua shughuli za uchimbaji wa madini, kusikiliza na kutatua kero mbalimbali za wachimbaji wadogo wa madini.

Katika ziara hiyo Profesa Kikula aliambatana na Makamishna wa Tume, Profesa Abdulkarim Mruma na Haroun Kinega, Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Wadogo wa Madini mkoani Dodoma (DOREMA),  Kulwa Mkalimoto, Kaimu Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Dodoma, Nicas Sangaya pamoja na waandishi wa habari.

Alimtaka Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Wadogo wa Madini mkoani Dodoma (DOREMA),  Kulwa Mkalimoto na  Kaimu Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Dodoma, Nicas Sangaya kushirikiana kwanza kwa kuchukua alama za eneo (coordinates) ili kubaini maeneo yasiyo na leseni na kuwapatia wachimbaji hao ili wafanye uchimbaji bora wenye kufuata sheria na kanuni za madini.

Aliendelea kufafanua kuwa, kwa maeneo yenye leseni wachimbaji wadogo wa madini wanaweza kuangalia namna ya kushirikiana na wamiliki wa leseni kwa kuingia ubia na kujipatia kipato pasipo migogoro isiyo ya lazima.

Profesa Kikula alisisitiza kuwa lengo la Serikali kupitia Tume ya Madini ni kuona wachimbaji wadogo wa madini wanafanya shughuli zao katika mazingira mazuri kwa kufuata kanuni na sheria za madini.

Katika hatua nyingine, Profesa Kikula aliwataka wachimbaji hao kuunda vikundi vidogo na kuomba leseni na kusisitiza kuwa Tume ya Madini ipo tayari  kuwasaidia kwa njia zote kupitia wataalam wake ikiwa ni pamoja na namna ya kuomba leseni za madini, elimu kuhusu kanuni na sheria za madini.

Wakiwasilisha kero zao kwa Mwenyekiti Kikula kwa nyakati tofauti, wachimbaji hao walisema kuwa wamekuwa wakifanya shughuli zao kwa muda mrefu pasipokuwa na leseni huku kukiwepo na watu wanaojitokeza na kudai kuwa ni wamiliki halali wa leseni za madini.

Awali akielezea historia ya ugunduzi wa madini aina ya rubi katika eneo hilo, mgunduzi ambaye ni mwenyeji wa kijiji hicho,  Shabani Kigelulye alisema kuwa, kati ya mwaka 2005 na 2006 akiwa shambani kwake katika eneo hilo aligundua mawe aliyohisi kuwa ni madini ya rubi.

Alieleza kuwa, katika harakati za utafiti wa  madini hayo mwaka 2007 alipeleka sampuli za mawe hayo aliyohisi kuwa ni madini ya rubi kwa ndugu wake walioko Dodoma Mjini na Arusha na kuelezwa kuwa yalikuwa ni madini ya rubi.

Aliendelea kueleza kuwa kwa kushirikiana na ndugu zake alipeleka sampuli hizo za mawe kwenye Ofisi za Madini na kushauriwa kuomba leseni na kupata.

Aliongeza kuwa  mwaka 2008 aliingia ubia na  wenzake Roja Sezinga, Johnson Kamara na Perfect Shayo na kuanza uchimbaji wa madini, na kusisitiza kuwa mwaka 2009 wakazi wengi wa kijiji hicho waliingia na kuanza kuchimba kiholela pasipokuwa na leseni hali iliyopelekea mgogoro.

Katika hatua nyingine Profesa Kikula alitembelea eneo lililopangwa kujengwa mtambo wa kuyeyushia shaba na kukuta jengo lililotelekezwa tangu mwaka 2004

Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Wadogo wa Madini mkoani Dodoma (DOREMA), Kulwa Mkalimoto alimweleza Profesa Kikula na timu yake kuwa, kampuni ya Igozomo kutoka China ilipanga kujenga mtambo wa kuyeyushia shaba lakini baadaye walisitisha uwekaji wa mtambo huo baada ya kutoelewana na wazawa.

Profesa Kikula alishauri wawekezaji wote wenye nia ya kuwekeza kwenye shughuli za madini nchini kukutana na wenyeviti wa vyama vya wachimbaji madini ambao wanaweza kuwapa taratibu sahihi za uwekezaji nchini hivyo kuepuka kuingia kwenye mikono ya matapeli.

Wakati huohuo akiwa katika Ofisi ya Katibu Tawala wa Wilaya ya Mpwapwa, Sarah Komba, Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula alisema kuwa suala ushiriki wa huduma za jamii (corporate social responsibility) kwa makampuni ya madini nchini si la hiari bali ni moja ya sheria.

Aliendelea kufafanua kuwa ni vyema kukawepo  mikataba kati ya wakuu wa wilaya na kampuni za madini kuhusu maeneo yanayohitaji katika uboreshaji wa huduma za jamii na kuhakikisha kuwa wananchi wananufaika na huduma zilizoainishwa kwenye mikataba na kupunguza migogoro.

“ Serikali kupitia Tume ya Madini imeweka  mikakati ya kuhakikisha wananchi wote wananufaika na rasilimali za madini kupitia ushirikishwaji wananchi kwenye utoaji wa huduma kwenye kampuni za madini (local content) na kupata huduma bora za jamii kutokana na uwekezaji unaofanywa na kampuni za madini,” alisisitiza Profesa Kikula.

Akielezea mikakati ya kumaliza migogoro kwenye maeneo yenye shughuli za uchimbaji madini nchini, Profesa Kikula alisema kuwa Tume ya Madini inaandaa rasimu ya mfumo wa utatuzi wa migogoro  kuanzia kwenye ngazi ya kijiji, kata na wilaya kabla ya kufikia ngazi ya tume.

Naye Katibu Tawala wa Wilaya ya Mpwapwa, Sarah Komba alimpongeza na kumshukuru Profesa Kikula pamoja na timu yake kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kutatua changamoto kwenye maeneo ya wachimbaji wadogo wa madini na kutoa elimu kuhusu sheria na kanuni za madini

Aidha Komba aliwataka wachimbaji wadogo wa madini kutoa taarifa za wavamizi wasiokuwa na leseni za madini ili hatua kali za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi yao.

Kwa upande wake Kamishna wa Tume ya Madini, Profesa Abdulkarim Mruma akizungumza katika mahojiano maalum na vyombo vya habari aliwataka wananchi wanaogundua madini kwenye maeneo yao kutoa taarifa kwenye ofisi za vijiji na vyama vyama vya wachimbaji madini na kufika kwenye Ofisi za Madini  kwa ajili ya utambuzi wa madini na  kuelekezwa namna ya kuomba leseni.

Alisema kutokana na wagunduzi wengi kuchimba bila kushirikisha uongozi wa kijiji, wilaya na vyama vya wachimbaji madini wamejikuta wakitoa mwanya kwa wajanja kuomba leseni hivyo kuzalisha migogoro isiyokwisha.

Alisema kuwa Serikali kupitia Tume ya  Madini imeweka utaratibu mzuri sana wa kumlinda mgunduzi wa madini tangu anapogundua madini hayo hadi kupata leseni.


Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula (kushoto) akisalimiana na Katibu Tawala wa Wilaya ya Mpwapwa, Sarah Komba (kulia) mara baada ya kuwasili kweye Ofisi ya Katibu Tawala huyo. 

Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula akielezea mikakati ya Tume ya Madini kwenye uwezeshaji wa wachimbaji wadogo wa madini nchini kwenye ofisi ya Katibu Tawala wa Wilaya ya Mpwapwa, Sarah Komba. 

Kamishna wa Tume ya Madini, Profesa Abdulkarim Mruma akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili kwenye Ofisi ya kijiji cha Winza kilichopo wilayani Mpwapwa mkoani Dodoma. 

Jengo lililojengwa kwa ajili ya kusimikwa mtambo wa kuyeyushia shaba na kampuni ya Igozomo ya China lililopo katika kijiji cha Winza wilayani Mpwapwa mkoani Dodoma. 

Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula (kulia) akizungumza na wachimbaji wadogo wa madini katika machimbo ya Winza yaliyopo wilayani Mpwapwa mkoani Dodoma. 

Kamishna wa Tume ya Madini, Haroun Kinega (kushoto) akifafanua jambo alipokuwa akizungumza na wachimbaji wadogo wa madini katika machimbo ya Winza yaliyopo wilayani Mpwapwa mkoani Dodoma.

No comments:

Post a Comment