Na Greyson Mwase, Dodoma
Septemba
06, 2018
Mwenyekiti
wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula amemwagiza Mwenyekiti wa Chama cha
Wachimbaji Wadogo wa Madini mkoani Dodoma (DOREMA), Kulwa Mkalimoto na Kaimu Afisa Madini Mkazi
wa Mkoa wa Dodoma, Nicas Sangaya kuhakikisha wanakipatia kikundi cha wachimbaji
wadogo wa madini kijulikanacho kwa jina
la “Hapa Kazi Tu” kinachoendesha shughuli za uchimbaji wa madini aina ya
sunstone katika kijiji cha Suguta wilayani Kongwa mkoani Dodoma leseni ya
uchimbaji madini ndani ya mwezi mmoja kwa kufuata kanuni na sheria za madini.
Profesa
Kikula alitoa agizo hilo tarehe 05 Septemba, 2018 katika machimbo ya madini hayo yaliyopo katika
kijiji hicho kwenye ziara yake ya siku mbili katika wilaya za Kongwa na Mpwapwa
yenye lengo la kukagua shughuli za uchimbaji madini zinazofanywa na wachimbaji
wadogo, kusikiliza na kutatua kero zinazowakabili.
Katika
ziara hiyo, Profesa Kikula aliambatana na Makamishna wa Tume, Profesa
Abdulkarim Mruma na Haroun Kinega, Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Wadogo wa
Madini mkoani Dodoma (DOREMA), Kulwa
Mkalimoto, Kaimu Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Dodoma, Nicas Sangaya pamoja na
waandishi wa habari.
Mara
baada ya kusikiliza kero za wachimbaji wadogo hao Profesa Kikula mbali na
kutoa agizo hilo alimwelekeza Mwenyekiti
wa Chama cha Wachimbaji Wadogo wa Madini mkoani Dodoma (DOREMA), Kulwa Mkalimoto, kuhakikisha anasaidia
kikundi cha wachimbaji wadogo hao katika taratibu zote za usajili wa kikundi kabla ya kuanza kushirikiana na Kaimu Afisa
Madini Mkazi wa Mkoa wa Dodoma katika upatikanaji wa leseni ndani ya mwezi
mmoja.
Aidha,
Profesa Kikula alimtaka Mwenyekiti huyo kuwasaidia wachimbaji hao katika
usajili kwenye vyama vya wachimbaji
madini Tanzania pamoja na utafutaji wa masoko na bei elekezi kwenye masoko ya
kimataifa.
“Kutokana
na kuwa na mtandao mkubwa na uelewa kwenye masoko na bei elekezi za madini
kwenye masoko ya kimataifa, nakuelekeza kama Mwenyekiti wa wachimbaji
kuhakikisha unawasaidia wachimbaji hawa hususan kwenye maeneo ya masoko na bei
elekezi ili uchimbaji wao uwanufaishe wao na Serikali kupata mapato stahiki,”
alisema Profesa Kikula.
Profesa
Kikula alisema Serikali kupitia Tume ya Madini imeweka mikakati mbalimbali ya
kuhakikisha kuwa sekta ya madini inakuwa na mchango mkubwa kwenye ukuaji wa
uchumi wa nchi kupitia uboreshaji wa sheria na kanuni za madini pamoja na
utoaji wa elimu kwa wachimbaji wadogo kuhusu sheria na kanuni hizo.
Katika
hatua nyingine, Profesa Kikula aliwataka wachimbaji wadogo nchini kuhakikisha
kupitia viongozi wao kwenye vyama vya
wachimbaji madini wanashirikiana kwa karibu na viongozi wa vijiji,
wilaya na ofisi za madini ili uchimbaji wao ulete tija zaidi kwenye ukuaji wa
uchumi wa nchi.
Awali,
wakiwasilisha kero mbalimbali wachimbaji hao walisema kuwa wamekuwa wakikutana
na vikwazo mbalimbali kwenye usajili wa kikundi chao hali iliyopelekea
ucheleweshwaji wa maombi ya leseni.
Akizungumza
kwa niaba ya kikundi hicho, Job Pandila alisema awali waliwasilisha maombi yao
kwenye ofisi ya mkuu wa wilaya kwa ajili ya taratibu za usajili lakini kumekuwa
na ugumu katika usajili wa kikundi chao kutokana na kutokuwa na uelewa wa namna
bora ya kuwasilisha viambatisho kwenye maombi ya usajili wa kikundi.
Pandila
aliendelea kusema kuwa uchelewaji wa usajili wa kikundi umepelekea kushindwa
kuomba leseni ya madini na kuomba msaada katika usajili wa kikundi pamoja na
maombi ya leseni ili waendelee na uchimbaji wa madini na kujipatika kipato.
Awali
kabla ya kufika katika kijiji cha Suguta, Profesa Kikula alikutana na Mkuu wa
Wilaya ya Kongwa, Deogratius Ndejembie na kuelezwa changamoto mbalimbali kwenye
shughuli za uchimbaji madini zilizopo katika wilaya ya Kongwa.
Katika
kikao hicho, Mkuu wa Wilaya ya Kongwa, Deogratius Ndejembie alisema kumekuwepo
na mgogoro kwenye eneo la Suguta lililopo wilayani Kongwa mkoani Dodoma
kutokana na wachimbaji wengi kutokuwa na leseni za uchimbaji madini pamoja na
uelewa mdogo wa sheria na kanuni za uchimbaji madini.
Aidha, Ndejembie alimpongeza Profesa Kikula na timu
yake kwa kutembelea wilaya ya Kongwa na kusisitiza kuwa ziara hiyo mbali na
kutoa elimu kwa wachimbaji madini, itapunguza migororo isiyo na lazima
iliyokuwa ikijitokeza.
Wakati
huo huo katika kikao chake na Mkuu wa Wilaya ya Kongwa, Profesa Kikula
aliwataka Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa Nchini kuandaa utaratibu wa utoaji wa
mafunzo kwa wachimbaji madini kuhusu sheria na kanuni za uchimbaji madini.
Katika
ziara hiyo Profesa Kikula pamoja na ujumbe wake, walitembelea pia machimbo ya
Rays Metal Corporation na Tambi Minerals Resources yaliyopo katika kijiji cha
Tambi wilayani Mpwapwa mkoani Dodoma.
Mwenyekiti
wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula (kulia) akisaini kitabu cha wageni mara
baada ya kuwasili kwenye Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Kongwa, Deogratius
Ndejembie. Kushoto ni Kamishna wa Tume ya Madini, Haroun Kinega.
Mwenyekiti
wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula (kushoto) akibadilishana mawazo na Mkuu
wa Wilaya ya Mpwapwa, Deogratius Ndejembie (kulia) mara baada ya kumalizika kwa
kikao kwenye Ofisi ya Mkuu wa Wilaya hiyo.
Kutoka
kushoto, Kaimu Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Dodoma, Nicas Sangaya, Kamishna wa
Tume ya Madini, Profesa Abdulkarim Mruma, Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji
Wadogo wa Madini mkoani Dodoma (DOREMA), Kulwa Mkalimoto, Mwenyekiti wa Tume ya
Madini, Profesa Idris Kikula, Mkuu wa Wilaya ya Mpwapwa, Deogratius Ndejembie
na Kamishna wa Tume ya Madini, Haroun Kinega wakiwa katika picha ya pamoja mara
baada ya kumalizika kikao hicho.
Mwenyekiti
wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula (kushoto) na Kamishna wa Tume ya
Madini, Profesa Abdulkarim Mruma (kulia) wakiangalia moja ya mawe ili kubaini
madini yaliyomo kwenye machimbo ya Suguta yaliyopo wilayani Kongwa mkoani
Dodoma.
Sehemu
ya wachimbaji wadogo wa madini wakifuatilia ufafanuzi uliokuwa unatolewa na
Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula (hayupo pichani) kwenye
machimbo ya Suguta yaliyopo wilayani Kongwa mkoani Dodoma.
Mwenyekiti
wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula (mbele) pamoja na msafara wake
wakiendelea na ziara kwenye kwenye machimbo ya Suguta yaliyopo wilayani Kongwa
mkoani Dodoma.
Mmoja
wa watendaji wa migodi ya shaba ya Rays Metal Corporation na Tambi Minerals
Resources iliyopo katika kijiji cha Tambi wilayani Mpwapwa mkoani Dodoma akitoa
ufafanuzi kwa Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula (katikati).
Kulia ni Kamishna wa Tume ya Madini, Haroun Kinega.
Sehemu
ya mgodi wa shaba wa Rays Metal Corporation uliopo katika kijiji cha Tambi
wilayani Mpwapwa mkoani Dodoma.
No comments:
Post a Comment