Thursday, September 6, 2018

Naibu Waziri Biteko afanya ziara ya kushtukiza mgodi wa MMG na kubaini madudu


·        Abaini raia wa kigeni 10 wasio na vibali vya kazi waliokuwa wamejificha ndani ya mgodi
·        Atoa wiki moja mikataba ya ajira kwa wafanyakazi

Na Greyson Mwase, Musoma

Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko leo tarehe 29 Agosti, 2018 amefanya ziara ya kushtukiza katika Mgodi wa Dhahabu wa MMG unaomilikiwa na kampuni ya Waarmenia uliopo katika Wilaya ya Musoma mkoani Mara.

Mara baada ya kuwasili katika mgodi huo na kupata maelezo ya namna ya uendeshaji wa mgodi huo kutoka kwa Meneja Uendeshaji,  Sezgey Sazgyyan aliendelea na  ukaguzi wa mgodi na kubaini ukiukwaji wa  kanuni za usalama migodini ikiwa ni pamoja na watumishi kufanya  kazi katika mazingira hatarishi pasipokuwa na  vifaa vya usalama mgodini.

Mara baada ya kutoa maelekezo, Naibu Waziri Biteko alifanya kikao na uongozi wa mgodi pamoja na wafanyakazi wa mgodi huo lengo likiwa ni kusikiliza kero mbalimbali pamoja na kuzitatua.

Akitoa maelezo kuhusu idadi ya wataalam wa kigeni na wa kitanzania katika mgodi huo wakati wa uwasilishaji wa  taarifa ya utekelezaji wa shughuli za mgodi huo tangu kuanzishwa kwake mwaka 2017 Afisa Utumishi wa mgodi huo,  Rose Masanja alisema mgodi mpaka sasa una wafanyakazi 126 wa kitanzania ambao ni pamoja na vibarua kutoka katika vijiji vilivyopo pembezoni mwa mgodi na wataalam watatu kutoka nje ya nchi.

Mara baada ya kupokea taarifa hiyo, Naibu Waziri Biteko alimbana Masanja na kumtaka kutoa taarifa sahihi kuhusu  idadi ya wataalam wa kigeni wanaofanya kazi kwa kuwa taarifa zote anazo kiganjani mwake kabla ya kufanya ziara katika mgodi huo.

Mara baada ya kauli ya Naibu Waziri Biteko, Masanja alieleza kuwa kuna wafanyakazi wa kigeni takribani 10 wasio na vibali vya kazi na wamejificha ndani ya vyumba na kuelekeza kwenye vyumba walivyojificha.

Naibu Waziri Biteko akiambatana na Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Vicent Anney, Meneja Uendeshaji wa Mgodi huo, Sezgey Sazgyyan  alielekea kwenye vyumba walivyojificha na kufanya msako na kubaini watumishi wa kigeni wasio kuwa na vibali wamejificha kwenye vitanda.

Aidha, Biteko alibaini baadhi ya wafanyakazi wa mgodi huo waliokuwa wamefungiwa chooni kwa takribani masaa matatu na uongozi ili kuficha aibu ya kutokuwa na vifaa usalama migodini. 

Biteko alimwelekeza Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Vicent Anney kuwachukulia hatua za kisheria wafanyakazi hao ambapo bila kusita Mkuu wa Wilaya huyo alielekeza Ofisi ya Wilaya ya Uhamiaji kufika muda huohuo kuwakamata na kuwafikisha kwenye ofisi hizo kwa ajili ya kutoa maelezo.

Katika hatua nyingine, Biteko alisikiliza kero mbalimbali za watumishi wa mgodi huo ambapo alielezwa kuwa watumishi wamekuwa wakifanya kazi katika mazingira ya shida ikiwa ni pamoja na kukosa huduma zote muhimu kama maji salama na matibabu.

Akizungumza kwa niaba ya watumishi wenzake,  Afisa Usalama wa Mgodi huo,  Stephen Wambura alisema watumishi wa kitanzania wamekuwa wakifanya kazi katika mazingira yasiyo salama bila kuwa na mikataba ya ajira na pale alipokuwa akiushauri uongozi wa mgodi kutatua changamoto hizo alikuwa akiambulia matusi.

“Mheshimiwa Naibu Waziri, tunashukuru sana kwa kufanya ziara katika mgodi huu kwani tumekuwa tukifanya kazi kama watumwa huku tukikosa huduma muhimu hali inayohatarisha usalama wa afya zetu,” alisema Wambura.

Naye Zuwena Swedi ambaye ni muuguzi wa kituo cha huduma ya kwanza cha mgodi huo aliongeza kuwa amekuwa akifanya kazi katika mazingira magumu ikiwa ni pamoja na kutopewa muda wa kutosha kupumzika hasa ikizingatiwa kuwa ni mama wa mtoto mchanga.

Wakati huo huo akihitimisha kikao hicho, Naibu Waziri Biteko alitoa wiki moja kwa uongozi wa Mgodi kuhakikisha umesaini mikataba na watumishi.

Alisema kuwa Serikali inawakaribisha wawekezaji kufanya shughuli za utafutaji na uchimbaji wa madini nchini, hivyo wawekezaji wanaowekeza nchini wanatakiwa kufuata sheria na kanuni za utafiti na uchimbaji wa madini.

“Ni lazima wawekezaji wakahakikisha kuwa wanafuata kanuni na sheria za madini ikiwa ni pamoja na kuhakikisha watumishi wa kitanzania wanafanya shughuli za utafutaji na uchimbaji madini katika mazingira yaliyo salama kwa afya na kupata stahiki zao kwa wakati,” alisisitiza Biteko.

Alisema kuwa, katika kuhakikisha kuwa sekta ya madini inaongeza mchango wake kwenye pato la taifa, serikali imeboresha sheria na kanuni za madini ambazo zitakuwa na manufaa kwa watanzania na wawekezaji kutoka nje ya nchi.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Mara, Vicent Anney akizungumza katika kikao hicho aliwataka watumishi wa mgodi kutoa taarifa zozote za ukiukwaji wa sheria na kanuni za nchi na madini na kuongeza kuwa Serikali ya Awamu ya Tano ipo tayari kwa ajili ya kuwatetea.

Pamoja na ziara katika mgodi huo, Naibu Waziri Biteko alifanya ziara katika machimbo ya wachimbaji wadogo yaliyopo katika eneo la Ikungwi, Musoma Vijijini  na kuwataka wachimbaji hao kutotumia zebaki katika uchenjuaji wa madini.


Meneja Uendeshaji wa Mgodi wa Dhahabu wa MMG, Sezgey Sazgyyan (kulia) akitoa ufafanuzi kwa Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (kushoto) mara  baada ya kuwasili kwenye mgodi huo kwa ajili ya ziara yake tarehe 29 Agosti, 2018. 

Sehemu ya watumishi wa Mgodi wa Dhahabu wa MMG wakisikiliza maelekezo yaliyokuwa yanatolewa na Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (hayupo pichani) katika kikao chake na uongozi na watumishi hao. 

Afisa Usalama wa Mgodi wa Dhahabu wa MMG, Stephen Wambura akiwasilisha kero yake mbele ya Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (hayupo pichani). 

Sehemu ya raia wa kigeni waliokuwa wakifanya kazi katika Mgodi wa Dhahabu wa MMG pasipokuwa na vibali vya kazi nchini.
Sehemu ya Mgodi wa Dhahabu wa MMG uliopo wilayani Musoma mkoani Mara.

1 comment:

  1. Wachimbaji wadogo wanakumbana na changamoto ya chemicals kupanda bei kiholela mfano sodium cyanide ilikua ina uzwa 390000 kwa mwezi wa 7lakini kwa sasa ni 470000, wizara fanyeni kuwasaidia wachimbaji wadogo maana wanaumia na pili wanachangia kodi

    ReplyDelete