Monday, August 13, 2018

Waziri Kairuki ataka wafanyabiashara wa madini wazaliwe upya


Na Asteria Muhozya, Arusha

Waziri wa Madini Angellah Kairuki amewataka Wafanyabiashara wa Madini nchini kuzaliwa upya kwa kufuata Sheria, Kanuni na  taratibu kwa kufanya biashara halali ya madini  ili kuziwezesha pande zote yaani Serikali na  Wafanyabishara  kunufaika na rasilimali hiyo.

Waziri Kairuki ameyasema hayo jana wakati akizungumza na wafanyabiashara wa madini  wa jijini Arusha waliohudhuria mkutano huo  ulioratibiwa na Chama Cha Wafanyabiashara wa Madini Tanzania, (TAMIDA).

Kairuki alisema zama zimebadilika na hivyo  kuwatahadharisha wale wote wanaofanya vitendo vilivyo kinyume na taratibu na kueleza kuwa,  hawatasalimika na mkono wa sheria kwa kuwa serikali imedhamiria kuhakikisha kwamba rasilimali madini inawanufaisha watanzania na taifa.

“Nimekuja hapa tubatizane. Naomba tuzaliwe upya. Tushirikiane vizuri. Naahidi kuwa balozi wenu mzuri. Nitatekeleza yale yenye manufaa kwetu sote. Lakini watakaokwenda kinyume, serikali ina macho yanayoona sana na yenye lenzi za hatari,” alisisitiza Kairuki.

Kairuki alisisitiza kuwa, tayari anazo taarifa za kila mfanya biashara wa madini wa jijini Arusha na kuwataka wote wanaokwenda kinyume kujitafakari upya na kuchukua hatua  sahihi kwani anamfahamu kila mmoja.

Alisema, serikali inatambua na kuthamini mchango wa biashara ya madini katika pato la taifa na katika kuzalisha ajira na kuongeza kuwa, itaendelea kuweka mazingira mazuri ya biashara ya madini na kuwataka wale wote waliokuwa wakitenda kinyume ikiwemo kukwepa kodi kujisalimisha kwake ili kuepuka kuingia katika makosa ya uhujumu uchumi.

“Kama unadhani ulikuwa unakwepa kodi, unakwenda kinyume, njoo uniambie. Haitapendeza upate kosa la uhujumu uchumi, kumbukeni kuwa kosa hilo halina dhamana,” alisisitiza Waziri Kairuki.

Akizungumzia suala la utoaji leseni za usafirishaji madini nje ya nchi, alisema serikali italifanyia haraka suala hilo ili kuleta ufanisi katika biashara ya madini huku akisisitia kuwa, watakaopatiwa leseni hizo ni wale tu watakaokidhi vigezo.

Aidha, Waziri Kairuki alitumia fursa hiyo kukaribisha wawekezaji katika sekta ndogo ya Uongezaji thamani madini na kueleza kuwa, serikali imedhamiria kuhakikisha kwamba shughuli za uongezaji  madini  zinafanyika nchini ikilenga kuongeza  mchango wa madini katika pato la taifa na kuzalisha ajira.

Aliwataka wafanya biashara wa madini wenye nia  kuwekeza katika viwanda vya ukataji na unga’rishaji madini ya vito kufanya hivyo  na kuwasilisha mapendekezo serikalini ili kuna namna bora ya kufanikisha suala husika.

Kairuki aliongeza kuwa, masuala ya uongezaji thamani madini nchini ni moja ya mapendekezo katika Sheria mpya ya madini  na kuelea kuwa, mwongozo wa namna ya shughuli za uongezaji thamani madini zitakavyofanyika utatolewa na serikali baada ya kukamilisha suala hilo.

“ Lakini pia hatukatazi wageni kuwekeza nchini. Isipokuwa tunataka waje kihalali,” alisisitiza Waziri Kairuki.

Awali, akisoma risala ya wafanyabiashara hao, Mwenyekiti wa TAMIDA Sam Mollel, alisema, TAMIDA inaunga mkono suala la uongezaji thamani madini kufanyika nchini kwa kuwa shughuli hizo zitasaidia  kuongeza thamani ya madini, fedha za kigeni kuhamisha teknolojia, kupanua wigo wa ajira na kufungua viwanda vingi vya uongezaji thamani na hatimaye kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha madini barani Afrika.

Vilevile, alisema kuwa, chama hicho kinaunga mkono  kutosafirisha madini ghafi ya Tanzanite nje ya  nchi na kupendekeza kuwa madini ya tanzanite yanayozidi gramu 1  yakatwe  hapa nchini na kwa yale yaliyo  nusu uzito  yaongezwe umbile kisha yaruhusishwe kusafirishwa yakiwa ghafi kwa kuwa bado hakuna ujuzi wa kukata madini  katika kiwango hicho.

“Mhe. Waziri tunapendekeza mchakato  huo ufanyike hivyo  wakati tukiendelea na kupata ujuzi na wataalam katika suala hilo na baada ya muda basi liwekwe zuio,” alisema Mollel.

Pia, alisema Tamida inapendekeza Kamati Pamoja ya kupanga bei elekezi za madini huku ikishirikisha serikali na wadau wa madini na pia kuiomba serikali kuangalia mifumo ya kodi.

Akizungumzia ujenzi wa ukuta unaozunguka migodi ya tanzanite Mirerani, alisema kuwa, Tamida inaunga mkono jitihada zilizofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Magufuli na kueleza kuwa, ukuta huo umesaidia kulinda rasilimali na udhibiti wa madini hayo.

Mollel aliongeza kuwa, ukuta wa mirerani umezuia uingiaji holela katika migodi hiyo kwa kuwa kila mwingiaji inampasa kuwa na kitambulisho na uwepo wa geti moja tu.

Pia, alisema kuwa, ukuta huo umeongeza Imani kubwa kwa walaji wa madini hayo zikiwemo nchi za Marekani na Ulaya na kuongeza kuwa, “ukuta umedhibiti ajira za watoto migodini na kuondoa wizi wa vifaa  migodini”.

Waziri wa Madini Angellah Kairuki akipokea taarifa iliyowasilishwa na Mwenyekiti wa Wafanyabiashara wa Madini Tanzania (TAMIDA) Sam Mollel kwa niaba ya wafanyabiashara hao.

Mwenyekiti wa Wafanyabiashara wa Madini Tanzania (TAMIDA) Sam Mollel akizungumza jambo wakati wa mkutano baina ya Waziri wa Madini Angellah Kairuki na Wafanyabiashara wa madini wa jijini Arusha. Wa pili kulia ni Kamishna wa Madini nchini, Mhandisi David Mulabwa, wa kwanza kulia ni Kamishna Msaidizi wa Madini wa Mkoa wa Arusha Musa Shanyangi. Kushoto ni Viongozi wa TAMIDA. 
Sehemu ya wafanyabishara wa madini wa jijini Arusha wakifuatilia mkutano baina yao na Waziri wa Madini Angellah Kairuki (hayupo pichani).


Mmoja wa wafanyabishara madini akimwonesha Waziri wa Madini Angellah Kairuki madini  aina ya Ruby na kumweleza kuhusu ukubwa tofauti wa madini hayo na suala zima la uongezaji thamani madini hayo kabla ya kusafirishwa. 

Sehemu ya wafanyabishara wa madini wa jijini Arusha wakifuatilia mkutano baina yao na Waziri wa Madini Angellah Kairuki (hayupo pichani).

No comments:

Post a Comment