Na Greyson Mwase, Morogoro
Naibu
Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo amewataka viongozi na maafisa waandamizi
walioteuliwa kufanya kazi na Tume ya Madini iliyoanzishwa hivi karibuni kuwa
mstari wa mbele kwenye mapambano dhidi ya rushwa kwenye maeneo ya kazi.
Naibu
Waziri Nyongo aliyasema hayo leo tarehe 11 Agosti, 2018 alipokuwa akifunga
mafunzo ya siku sita yaliyofanyika mjini Morogoro kwa kushirikisha viongozi na
maafisa waandamizi walioteuliwa kufanya kazi na Tume ya Madini.
Alisema
kuwa, mara baada ya kumalizika kwa mafunzo hayo anatarajia kuona viongozi
pamoja na maafisa madini wakazi wa mikoa na maafisa migodi wanakuwa vinara
kwenye mapambano dhidi ya rushwa kwenye utoaji wa leseni na migodi.
Katika
hatua nyingine, Nyongo aliwataka watumishi hao kufanya kazi kwa ubunifu hususan
kwenye ukusanyaji wa maduhuli ili kuvuka lengo lililowekwa na Serikali.
“Ni
matarajio yangu kuwa kuanzia mwezi
Septemba, mtaanza kukusanya maduhuli kwa njia ya kieletroniki ili kudhibiti
upotevu wa fedha na kufikia lengo lililowekwa na Serikali,” alisema Naibu
Waziri Nyongo.
Aliendelea
kuwataka viongozi walioteuliwa kusimamia shughuli za madini mikoani kuhakikisha
wanatatua migogoro iliyopo kwenye maeneo
yenye shughuli za uchimbaji madini badala ya kusubiri viongozi wa ngazi za juu
kutatua kupitia ziara mbalimbali wanazofanya kwenye maeneo hayo.
Awali
akizungumza katika ufungaji wa mafunzo hayo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini,
Profesa Simon Msanjila aliwapongeza viongozi na mafisa waandamizi walioteuliwa kufanya
kazi na Tume ya Madini na kuwataka kuhakikisha wanafuata taratibu za
makabidhiano ya ofisi kabla ya kuripoti kwenye vituo vipya vya kazi.
Mafunzo
hayo yalilenga maeneo tofauti ikiwa ni pamoja na historia ya mabadiliko ya
sheria ya madini, sheria ya madini ya mwaka 2010 na marekebisho yake ya mwaka
2017, muundo wa tume ya madini na mawasiliano ya ndani na nje ya tume.
Maeneo
mengine ni pamoja na muundo na mfumo wa mawasiliano wa Tawala za Mikoa na
Serikali za Mitaa (TAMISEMI), taratibu za ofisi na makusanyo na maduhuli ya
Serikali kwa njia ya kieletroniki (GEPG), usimamizi na utunzaji wa mali za
umma, taratibu za utoaji wa leseni za shughuli za madini na ushirikishwaji wa
wananchi/wazawa katika shughuli za madini.
Aidha
maeneo mengine ni pamoja na ukaguzi wa madini na biashara, utatuzi wa migogoro
katika sekta ya madini, taratibu za uwasilishaji wa taarifa makao makuu ya Tume
na kwenye mamlaka nyingine zinazohusika, utunzaji wa siri katika utumishi wa
umma, masuala ya utawala na rasilimaliwatu, sheria, kanuni na taratibu za
fedha, usimamizi wa mifumo ya udhibiti wa ndani, maadili katika utumishi wa
umma na mfumo wa uwazi wa upimaji utendaji kazi (OPRAS).
Naibu
Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo akifunga mafunzo ya viongozi na maafisa
waandamizi wa Tume ya Madini yaliyomalizika mjini Morogoro tarehe 11 Agosti,
2018
|
Katibu
Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila akitoa ufafanuzi kwenye
ufungaji wa mafunzo hayo.
|
Mkurugenzi
wa Huduma za Tume, Jerry Sabi akitoa neno la shukrani mara baada ya hotuba ya
ufungaji wa mafunzo hayo, iliyotolewa na Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo
(hayupo pichani)
|
Kutoka
kulia waliokaa mbele, Meneja Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu wa Tume ya
Madini, Miriam Mbaga, Mkurugenzi wa Huduma za Tume, Jerry Sabi, Katibu Mtendaji
wa Tume ya Madini, Profesa Shukrani Manya, Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus
Nyongo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila, Mkurugenzi wa
Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu wa Wizara ya Madini, Issa Nchasi na
Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Migodi na Mazingira wa Tume ya Madini, Dk. Abrahaman
Mwanga wakiwa katika picha ya pamoja sekretarieti iliyoratibu mafunzo hayo.
|
No comments:
Post a Comment