Na
Asteria Muhozya, Mara
Waziri wa Madini
Angellah Kairuki amesema Wizara italigawa kwa Wachimbaji Wadogo wa Madini eneo
lote la mgodi wa Buhemba linalomilikiwa na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO),
ikiwa Serikali itanufaika ipasavyo na
makusanyo kutokana na shughuli za wachimbaji hao.
Kauli ya Waziri
Kairuki imekuja kufuatia maombi yaliyotolewa na Chama Cha Wachimbaji Madini
Mkoa wa Mara (MAREMA) kupitia kwa Mwenyekiti wa Chama hicho Stephano Mseti
ambaye alimuomba Waziri Kairuki kulitoa eneo lote la STAMICO kwa wachimbaji hao
kwa kuwa wana uhakika wa kuchangia zaidi kodi za serikali ikiwa watamilikishwa
eneo husika.
Aidha, Mseti alimweleza Waziri Kairuki kuwa wachimbaji katika eneo hilo wamejiandaa
kikamilifu katika kuhakikisha kuwa wanalipa kodi stahiki kwa kuwa, ndani ya
mwezi mmoja waliopewa kufanya kazi katika eneo husika, wamekusanya kiasi cha
shilingi milioni 107 kama mrahaba.
Katika hatua nyingine,
wakati akisikiliza kero za wachimbaji hao, Waziri Kairuki aliiagiza Tume ya
Madini na Wataalam kutoka Wizara hiyo kuchunguza kwa kina suala la migogoro ya
migodi yote iliyopo katika eneo la
Buhemba iliyotolewa awali na STAMICO kwa wachimbaji hao na kukamilisha kazi husika ndani ya kipindi
cha wiki 3 ikiwemo kutoa mapendekezo aweze kujua hatua za kuchukua.
Akizungumzia mikakati
ya kuwaendeleza wachimbaji wadogo, Waziri Kairuki alieleza kuwa, tayari
serikali imeanza kujenga kituo cha umahiri katika mkoa huo ili kuwezesha
wachimbaji wadogo kujifunza uchimbaji
bora na kuwataka wachimbaji mkoani humo kukitumia kikamilifu kituo hicho mara
baada ya kukamilika kwake.
Akizungumzia muda wa
uhai wa leseni, alisema kuwa suala hilo limebainishwa kisheria kuwa ni ndani ya
kipindi cha miaka saba na kufafanua kuwa, ipo haki ya kuhuisha muda wa leseni na hivyo kuwataka wamiliki
wote wa leseni kuzingatia muda husika uliowekwa kisheria.
Pia, aliwataka
wachimbaji hao kutoa taarifa za kuwepo Maafisa Madini wanaomiliki leseni za
uchimbaji madini au wanaomiliki leseni hizo kupitia kwa kutumia majina tofauti ili hatua stahiki
ziweze kuchukuliwa.
Akizungumzia kuhusu
suala la migogoro, alisema kuwa Serikali haifurahishwi na migogoro inayotokea
katika maeneo ya migodi na hususani ile inayohatarisha maisha na kuongeza kuwa,
serikali haipendi kufunga migodi hiyo kutokana na umuhimu wa migodi hiyo kwa
pande zote.
Pia, Waziri Kairuki
alisisitiza kuhusu suala la uchimbaji salama
migodini na Mpango wa Uwajibikaji kwa Jamii na kuongeza kuwa, suala hilo
ni lazima litekelezwe na wamiliki wote wa leseni wakiwemo wachimbaji wadogo.
Awali, Mkuu wa Mkoa
wa Mara Adam Malima, alisema Mkoa huo umejipanga kuwa na Gold Exchange ili kuwezesha mkoa huo pia kunufaika na rasilimali
hiyo.
Aidha, alisisitiza
suala la uchimbaji salama wa madini ikiwemo utunzaji wa mazingira na kuwataka
wachimbaji hao kubadilika kwa kuhakikisha wanafanya shughuli zao kisasa.
Naye, Naibu Waziri wa
Madini Stanslaus Nyongo alisema kuwa, Serikali inawaona wachimbaji wadogo kwa
jicho la kipekee na inajua kuwa, ikiwawezesha itapata fedha nyingi kutokana na
rasilimali hiyo.
Alisema kuwa, mkoa
huo una migogoro mingi ikilinganishwa na mingine na kumshauri Waziri Kairuki
kupokea vizuri malalamiko yote ya wanaolalamika
kwani si wote wanalalamika kihalali.
Pia, aliwashauri
Maafisa Madini nchini kuhakikisha kuwa, wanapotatua migogoro zawanavishirikisha
Vyama vya Wachimbaji katika kutatua migogoro hiyo ikiwemo katika suala la
ukusanyaji kodi za serikali.
Akizungumza katika
mkutano huo, Rais wa Chama Cha Wachimbaji Madini Tanzania (FEMATA), John Bina,
aliiomba Serikali kuiwezesha Tume ya
Madini ili iweze kuwafikia wachimbaji katika ngazi za chini.
Pia, aliwataka
wachimbaji kuwa wakweli na kuacha ubifasi, na kueleza kuwa, kuna watu ndani ya
umoja huo wananufaika pindi panapokuwa na migogoro na kuongeza kuwa, migogoro
katika jamii ya wachimbaji ni mdudu anayekua kila siku.
Awali, akiwasilisha
taarifa ya chama hicho, Katibu Mkuu wa MAREMA, Milele Mundeba, alisema Chama
hicho kinakusudia uanzishaji wa biashara ya vifaa vya uchimbaji madini.
Mbali na wachimbaji
mkutano huo uliofanyika tarehe 16 Agosti, ulihudhuriwa na benki ya CRDB, SIDO,
Benki ya Posta Tanzania, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Benki ya NMB, FINCA,
Shirika la Bima la Taifa ( NHIF),
Mamlaka ya Maji, Musoma (MUWASA), Migodi ya Wachimbaji wa Kati ya CATA
Mining, ACACIA na Shirika la Hifadhi ya
Jamii (NSSF).
![]() |
Waziri wa Madini
Angellah Kairuki akipokewa na viongozi mbalimbali MAREMA na FEMATA.
![]() |
Waziri wa Madini
Angellah Kairuki katika picha ya pamoja
na Baadhi ya Viongozi na Wanachama wa MAREMA na Chama cha Wachimbaji
Wadogo wa Madini, ( FEMATA).
![]() |
Waziri wa Madini Angellah Kairuki akizungumza jambo wakati wa mkutano na Chama cha Wachimbaji Madini Mkoa wa Mara (MAREMA).
No comments:
Post a Comment