Thursday, August 9, 2018

Maafisa madini watakiwa kufuata sheria, kanuni katika utoaji leseni


Na Greyson Mwase, Morogoro

Maafisa madini nchini wametakiwa kufuata sheria na kanuni katika utoaji wa leseni za madini ili kuondoa changamoto ya migogoro kwenye migodi ya madini.

Hayo yamesemwa leo tarehe 08 Agosti, 2018 na Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Profesa Shukrani Manya alipokuwa akitoa mafunzo juu ya taratibu za utoaji wa leseni za madini kwenye mafunzo ya kazi kwa viongozi na maafisa waandamizi wa Tume ya Madini yanayoendelea mjini Morogoro.

Alisema kuwa, ni vyema taratibu za utoaji wa leseni za  utafutaji wa madini zikafuatwa ambazo ni pamoja na mwombaji kubaini eneo linalomfaa kwa utafiti, kujaza fomu ya maombi na kuwasilisha Tume ya Madini kwa njia ya mtandao na nakala halisi (hard copies) na ombi kushughulikiwa, kuhakikiwa na kutathiminiwa.

Aliendelea kueleza taratibu nyingine  kuwa ni pamoja na ombi kupendekezwa na kukubaliwa kupewa leseni, mmiliki wa leseni kuomba ridhaa kwa mmiliki halali wa ardhi ya kuingia kwenye eneo la utafutaji madini, mmiliki wa leseni kwa kushirikiana na mamlaka za halmashauri/wilaya kuandaa mpango wa utoaji wa huduma za jamii.

Akielezea taratibu za maombi ya leseni za uchimbaji mdogo wa madini, Profesa Manya alieleza kuwa ni pamoja na mwombaji kubaini eneo linalomfaa, mwombaji kujaza fomu ya maombi na kuwasilisha katika Ofisi ya Afisa Madini Mkazi kwa njia ya mtandao na nakala halisi, ombi kupendekezwa na kukubaliwa kupewa leseni, mmiliki wa leseni kuomba ridhaa kwa mmiliki halali wa ardhi ya kuingia kwenye eneo la utafutaji wa madini na mmiliki wa leseni kwa kushirikiana na mamlaka za halmashauri/wilaya kuandaa mpango wa utoaji wa huduma za jamii.

Katika hatua nyingine akielezea taratibu za utoaji wa leseni za uchimbaji  wa kati na mkubwa Profesa Manya alitaja kuwa ni pamoja na  mwombaji kubaini eneo la leseni ya utafutaji, kujaza fomu ya maombi na kuwasilisha Tume ya Madini Makao Makuu kwa njia ya mtandao na nakala halisi (hard copies) na uthibitisho wa uwepo wa mradi wa uchimbaji, upembuzi yakinifu (feasibility Study) na hati ya utunzaji wa mazingira.

Alieleza taratibu nyingine kuwa ni pamoja na ombi kushughulikiwa, kuhakikiwa na kutathminiwa na ombi kupendekezwa kupewa leseni na kuendelea kufafanua kuwa hatua nyingine ni pamoja na ombi la leseni kuidhinishwa na Baraza la Mawaziri kwa leseni ya uchimbaji mkubwa, (Special Mining Licence), ombi la leseni  kukubaliwa kupewa leseni na mmiliki wa leseni kuomba ridhaa kwa mmiliki halali wa ardhi ya kuingia kwenye eneo la uchimbaji.

“ Mmiliki wa leseni atatakiwa kuomba ridhaa ya uwekezaji kwenye mamlaka ya serikali za mitaa, mmiliki wa leseni kwa kushirikiana na mamlaka za halmashauri/wilaya  kuandaa mpango wa utoaji wa huduma kwa jamii” alisisitiza Profesa Manya.

Akizungumzia kuhusu utoaji wa leseni za uchenjuaji wa madini, Profesa Manya alisema leseni hutolewa kwa kipindi kisichozidi miaka 10 na Tume ya Madini kwa mtu au kampuni/ushirika katika eneo ambalo lipo nje ya eneo la mmiliki wa leseni ya uchimbaji wa madini.

Aidha,  akielezea leseni za uyeyushaji wa madini, Profesa Manya alisema kuwa leseni hutolewa kwa kipindi  kisichozidi miaka 25 kwa mtu, kampuni au ushirika.

Wakati huo huo akielezea sifa za mwombaji wa leseni, Profesa Manya alieleza kuwa ni pamoja na mwombaji kuwa na umri usio chini ya miaka 18  na mwenye uwezo wa kifedha, kutokuwa na makosa katika umiliki wa leseni ya madini iliyo hai au iliyoisha muda au iliyofutwa ambayo hayakurekebishwa, kutokuwa na makosa yoyote likiwamo la kutokuwa mwaminifu na kampuni husika kuwa na anwani  ya posta na ofisi.


Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Profesa Shukrani Manya akielezea taratibu za utoaji wa leseni za madini kwenye mafunzo ya kazi kwa viongozi na maafisa waandamizi wa Tume ya Madini yanayoendelea mjini Morogoro tarehe 08 Agosti, 2018.

Sehemu ya washiriki wa mafunzo hayo wakifuatilia ufafanuzi uliokuwa unatolewa na Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Profesa Shukrani Manya (hayupo pichani).

Sehemu ya washiriki wa mafunzo hayo wakifuatilia ufafanuzi uliokuwa unatolewa na Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Profesa Shukrani Manya (hayupo pichani).

Sehemu ya washiriki wa mafunzo hayo wakifuatilia ufafanuzi uliokuwa unatolewa na Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Profesa Shukrani Manya (hayupo pichani).

No comments:

Post a Comment