Monday, August 6, 2018

Leseni za Madini sasa kutolewa kwa Masharti Magumu-Kairuki


Na Asteria Muhozya, Simanjiro

Waziri wa Madini Angellah Kairuki amesema kuanzia sasa Serikali itaanza kutoa Leseni za madini biashara ya madini kwa masharti magumu huku ikimtaka kila mwombaji  kutoa taarifa za mauzo ya uzalishaji, usafirishaji pamoja na mnyororo mzima wa biashara ya madini ikiwemo fedha zinazoingia nchini kutokana na biashara hiyo.

Pia, ameiagiza Tume ya Madini kuchukua hatua stahiki kwa kuhakikisha kila jambo katika mnyororo huo linasimamiwa kikamilifu na kuongeza kuwa, yeye kama waziri mwenye dhamana atahakikisha anafuatilia kila hatua itakayochukuliwa  na tume hiyo.

“Tume ichukue hatua. Nitakuwa na ninyi. Msiache hata mmoja atakayekwenda kinyume na haya. Nilifanya hivyo katika Sekta ya Utumishi wa Umma hata huku kwenye sekta ya madini, sitashindwa kufanya hivyo,” alisisitiza Waziri Kairuki.

Waziri kairuki aliyasema hayo jana tarehe 3 Agosti, Wilayani Simanjiro Mkoa wa Manyara wakati akipokea taarifa ya Kamati Maalum iliyoundwa kuchunguza mnyororo wa madini ya vito nchini.

Kamati hiyo ilifanya kazi yake kwa muda wa siku 30  kuanzia tarehe 26 Aprili, 2018 kwa  jukumu la kuchunguza  mnyororo wa madini ya vito  kuanzia kuzalisha hadi usafirishaji nje ya nchi pamoja na kubaini sababu za utoroshaji wa madini na kupendekeza hatua za kuchukuliwa ili kuzuia utoroshaji.

Pia, aliiagiza tume ya madini kuanzia tarehe 4 Agosti, kuhakikisha inapata taarifa za uzalishaji za migodi yote inayozalisha huku akitaka migodi husika ieleze mahali inakouzia madini yao, anayeuziwa madini hayo na kuongeza kuwa, zoezi husika linawajumuisha pia dealers.

Waziri Kairuki alisema, wizara yake imeamua kusimamia suala husika ikiwa ni jitihada za kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli za kuhakikisha kuwa rasilimali madini zinawanufaisha watanzania wote.

“ Lazima watanzania tutambue kuwa madini haya yanamilikiwa na watanzania wote. Tunatakiwa kuyalinda kwa ajii ya maendeleo yetu na kwa manufaa ya vizazi vijavyo,” alisema Kairuki.

Akizungumzia biashara ya madini ya tanzanite katika ukuta unaozunguka migodi ya tanzanite mirerani, alisema hakuna serikali inayotaka watu wake wasifanye biashara, hivyo, lengo la ukuta huo ni kuhakikisha kwamba inadhibiti utoroshaji wa madini na kuweka mfumo mzuri ambao utawezesha madini hayo kuzinufaisha  pande zote.

Alisema tayari wizara imeandaa Kanuni za Mirerani (Mirerani Contolled Area) ambazo hivi sasa zinafanyiwa maboresho  baada ya kuwepo changamoto kadhaa katika utekelezaji wake.

Katika hatua nyingine, Waziri Kairuki alisema serikali imebaini  baadhi ya wenye leseni za ‘broker’ kukaribisha wageni kutoka nje kufanya biashara hiyo kinyume na taratibu na  hatimaye kusafirisha madini hayo, hivyo, aliwataka wote wanaofanya hivyo kuacha mara moja na kuwataka watanzania wote wenye taarifa kuhusu suala hilo kutoa taarifa  katika mamlaka zinazohusika.

“Kamati hii imefanya uzalendo na imefanya kazi kubwa sana. Nimeipokea taarifa ya kamati lakini natamani wangenitajia majina ya watoroshaji. Nilitamani sana kuona majina lakini naamini itaniuma sikio,” alisisitiza Waziri Kairuki.

Pia, aliongeza kuwa serikali itazifuta leseni za  uchimbaji madini kwa wale wote ambao wameshindwa kuyaendeleza maeneo yao na kupewa wengine wenye nia ya dhati ya kuendeleza shughuli za uchimbaji madini nchini.

Akizungumzia mkakati wa serikali katika kuhamasisha shughuli za uongezaji thamani nchini, alisema kuwa serikali inaendelea kukiimarisha kituo cha TGC kilichopo jijini Arusha, kwa kuongeza wataalam katika masuala ya ukataji na unga’rishaji wa madini ya vito.
“Tayari tumepata walimu  7 kutoka nchini India, lakini bado tunafuatilia wengine kutoka nchini Thailand,”alisema Kairuki.

Akiwasilisha  taarifa ya Kamati kwa niaba ya Mwenyekiti wa Kamati hiyo,  Mratibu wa Kituo cha Jimolojia Tanzania (TGC), Eric Mpesa alisema Kamati husika ilipata fursa ya kutembelea mgodi wa Mundarara mpaka wa Namanga, Uwanja wa ndege wa KIA, Machimbo ya Tanzanite Mirerani, TGC, Ofisi ya Afisa Madini Mkazi Morogoro na Machimbo ya Epanko, Morogoro.

Akiwasilisha mapendekezo ya kamati husika Mpesa alisema kuwa, kamati inapendekeza Serikali kutengeneza mpango wa makazi katika eneo lililozungushiwa ukuta wa Mirerani ikizingatia uwepo wa eneo la uchimbaji, biashara, uanzishwaji wa kituo cha One Stop Centre, huduma za kijamii, maegesho ya vyombo vya usafiri, maeneo ya starehe na maeneo ya utalii.

Pia, alisema serikali ihakikishe kuweka mfumo wa ulinzi katika eneo lililozungushiwa ukuta na pia ilishauri serikali kuongeza wataalam wa Wizara katika maeneo ya migodi ili kurahisisha ufanyaji biashara na kuwezesha kuzuia utoroshaji wa madini ya vito.

Pendekezo lingine ni serikali kuwawezesha wachimbaji wadogo kupata teknolojia za kisasa pamoja na tafiti za kijiolojia kufanywa na watalaam  kutoka Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) kwa malipo ya gharama nafuu yatakayolipwa  baada ya uzalishaji kupatikana.

Pia, Kamati ilipendekeza seriakali kuishawishi mifuko ya jamii isaidie wadau  kuanzisha benki ya Madini itakayowapa wachimbaji na wafanyabiashara mikopo yenye masharti nafuu.

Akizungumzia mcchango wa sekta ya madini, alisema sekta hiyo inachangia fedha za kigeni cha kiasi cha wastani wa dola za Marekani milioni 27.8 kwa mwaka isipokuwa almasi na kati ya hizo, asilimia 27.8 ni madini yaliyosanifiwa na kunga’rishwa na asilimia 71.3 ni madini ghafi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Manyara  Alexander  Mnyeti alisema kwa muda mrefu serikali imekuwa ikichazewa kwa wadau katika migodi kutokulipa kodi stahiki za serikali.

Aliishauri wizara kufuta leseni za wale wote walioohodhi maeneo yao bila kuyafanyia kazi ili kuwezesha leseni husika kutumiwa na wengine wenye nia ya kuendeleza sekta ya madini.

Kuhusu suala la mikataba  ya ajira katika migodi hiyo aliishauri serikali na wadau kukaa pamoja na kujadili suala husika na kulitafutia ufumbuzi.

Kamati iliyoandaa taarifa husika ilikuwa na wajumbe 13 ikiongozwa na Mwenyekiti Sammy Mollel, Makamu Mwenyekiti Hamis Kim, Katibu Adam Rashid pamoja na wajumbe 10 na Sekretarieti.

Wajumbe wa Kamati hiyo walitoka TAMIDA, MAREMA, AREMA, RUVREMA, TAWOMA, BROKER pamoja na wajumbe kutoka Wizara ya Madini na TGC.


Mkuu wa Mkoa wa Manyara Alexander Mnyeti (kushoto) akiteta jambo na Mbunge wa Simanjiro James Ole Milya (katikati) na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Manyara Mhandisi Tumain Magesa (kulia). 

Waziri wa Madini Angellah Kairuki akiwa katika picha ya pamoja na Wabunge wa Kamati ya Nishati na Madini na wabunge wengine wa Mkoa wa Manyara, Kilimanjaro na Arusha. 

Waziri wa Madini Angellah Kairuki akifurahia jambo na Viongozi wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Manyara. Kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Alexander Mnyeti na kusshoto ni Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo. 

Waziri wa Madini Angellah Kairuki akiwa katika picha ya pamoja na Kamati iliyochunguza mnyororo wa madini ya vito  kuanzia kuzalisha hadi usafirishaji nje ya nchi pamoja na kubaini sababu za utoroshaji wa madini na kupendekeza hatua za kuchukuliwa ili kuzuia utoroshaji. Wa tatu kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Alexander Mnyeti.

Waziri wa Madini Angellah Kairuki akiwa katika picha ya pamoja na wawakilishi wa Vyama vya Wachimbaji madini.

No comments:

Post a Comment