Monday, July 23, 2018

Migodi nchini yatakiwa kuweka mitambo ya kuchejulia madini


Na Greyson Mwase, Tunduru

Naibu Waziri wa Madini, Dotto Biteko amewataka wamiliki wa migodi nchini kuhakikisha wanaweka mitambo ya kuchenjulia madini ili kuyaongezea thamani kabla ya kusafirishwa nje ya nchi.

Naibu Waziri Biteko ametoa wito huo kwenye mkutano wake na wachimbaji wadogo alioufanya katika kijiji cha Mbesa kilichopo wilayani Tunduru mkoani Ruvuma mara baada ya kutembelea Mgodi wa Shaba wa Mbesa kama moja ya ziara yake ya ukaguzi wa shughuli za madini katika mikoa ya Kusini ili kubaini changamoto pamoja na kuzitatua.

Katika ziara hiyo Naibu Waziri Biteko aliambatana na wataalam kutoka Wizara ya Madini, Mkuu wa Wilaya ya Tunduru, Juma Homera, Mbunge wa Tunduru Kusini, Daimu Mpakate pamoja na Vyombo vya Ulinzi na Usalama vya Wilaya ya Tunduru.

Alisema kuwa, wamiliki wa migodi wanatakiwa kuhakikisha wanaweka mitambo ya kuchenjulia madini ili mbali na kuongeza mapato nchini watoe ajira kwa wananchi wanaozunguka migodi.

Katika hatua nyingine, Biteko aliwataka wamiliki wa migodi kununua bidhaa za ndani badala ya kuagiza kutoka nje ya nchi pamoja na kutoa ajira kwa wazawa ili wananchi wanufaike na rasilimali za madini hayo.

Pia aliwataka wamiliki wa migodi kuhakikisha wanasajili mikataba yao kwenye Ofisi za Wizara ya Madini kama Sheria ya Madini inavyotaka.

Awali wakiwasilisha changamoto mbalimbali kwa Naibu Waziri Biteko, wachimbaji hao walitaja kuwa ni pamoja na mitaji midogo kwa ajili ya shughuli za uchimbaji wa madini, vifaa duni vya uchimbaji pamoja na leseni za madini kulipiwa kwa fedha za kigeni.

Walitaja changamoto nyingine kuwa ni pamoja na kutokuwepo kwa maabara za kupima madini migodini na baadhi ya wachimbaji kufutiwa leseni zao.

Wakati huo huo akielezea shughuli za uchimbaji madini ya shaba katika eneo la Mbesa lililopo Tunduru mkoani Ruvuma, Afisa Madini wa Tunduru Mjiolojia Abraham Nkya  alisema Serikali ilitenga eneo la Mbesa lenye ukubwa wa kilometa za mraba 156.053 ambalo liko umbali wa takribani kilometa 66 kutoka Tunduru Mjini.

Alisema leseni nyingi zimekuwa hazifanyiwi kazi hali iliyopelekea leseni zaidi ya 1000 kufutwa.

Aliendelea kufafanua kuwa kwa sasa Mbesa ina jumla ya leseni 441 za wachimbaji madini wadogo ambazo kati ya hizo 158 ni hai na 283 zina makosa mbalimbali ikiwemo kutokulipa ada ya pango, kutowasilisha taarifa ya utendaji kazi kwa kila robo mwaka n.k.

Akielezea faida za uchimbaji madini ya shaba katika kijiji cha Mbesa Mjiolojia Nkya alieleza kuwa ni pamoja na ulipaji wa kodi mbalimbali ikiwemo mrabaha, ajira kwa vijana wa kijiji cha Mbesa pamoja na vijiji vya jirani.

Aliendelea kutaja faida nyingine kuwa ni pamoja na uchangiaji wa shughuli za kijamii ikiwa ni pamoja na ujenzi wa soko, uchimbaji wa kisima katika shule ya sekondari ya Mbesa, hospitali na ajira kwa wakinamama wanaohudumia eneo la uchimbaji.


Naibu Waziri wa Madini, Dotto Biteko (wa pili kulia) pamoja  na msafara wake wakiendelea na ziara katika Mgodi wa Shaba wa Mbesa uliopo katika  wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma tarehe 20 Julai, 2918.
Mkurugenzi wa Mgodi wa Shaba wa Mbesa, Ziadi Igangula (kulia) akimwonesha Naibu Waziri wa Madini, Dotto Biteko (kushoto) jiwe lenye madini ya shaba mara alipofanya ziara kwenye mgodi huo.
Sehemu ya wananchi wa kijiji cha Mbesa kilichopo wilayani Tunduru mkoani Ruvuma wakimsikiliza Naibu Waziri wa Madini, Dotto Biteko (hayupo pichani) kwenye mkutano wa hadhara.
Naibu Waziri wa Madini, Dotto Biteko (kulia) pamoja na Mkuu wa wilaya ya Tunduru, Juma Homera (kushoto) wakisikiliza kero ,mbalimbali zilizokuwa zinawasilishwa na wananchi kwenye mkutano wa hadhara.
Naibu Waziri wa Madini, Dotto Biteko  (kushoto) akiagana na Mkuu wa wilaya ya Tunduru, Juma Homera (kulia) mara baada ya kukamilika kwa ziara kwenye wilaya hiyo.

No comments:

Post a Comment