Monday, June 4, 2018

Waziri Kairuki azindua Tume ya Madini


ü Aikabidhi Vitendea kazi
ü Prof. Kikula asisitiza uadilifu

Na Asteria Muhozya, Dodoma

Waziri wa Madini Angellah Kairuki amezindua Tume ya Madini sambamba na kukabidhi vitendea Kazi kwa Mwenyekiti wake Prof. Idris Kikula pamoja na Makamishna wa Tume hiyo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Waziri Kairuki alisisitiza kuwa, ni imani yake, imani ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa  Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli na Watanzania wote kuwa Tume hiyo itabadilisha simulizi za Sekta ya madini kutoka kuwa za kukatisha tamaa na kuwa za matumaini na hivyo kuibadili historia ya sekta ya madini kutoka kuwa ya miguno na manung'uniko na kuwa ya kujipongeza na kujivunia.

"Nataka mtambue kuwa ninyi sasa ndiyo macho, masikio, pua na mikono yetu kwenye sekta ya madini," alisisitiza Waziri Kairuki.

Aliongeza kuwa,Watanzania wana matarajio makubwa na Tume hiyo na kueleza kuwa, wanataka kulala usingizi wakiamini kuwa sekta ya madini iko katika mikono safi na salama kwa kuwa wanaamini  Tume itatenda haki, itasimamia ukweli na kuzingatia maslahi ya  kesho, kesho kutwa na vizazi vijavyo.

Aidha, Waziri Kairuki alitumia fursa hiyo kuishauri Tume ya Madini kuyafanyia kazi masuala kadhaa ambayo yatakuwa na tija kwa sekta ya Madini na kuyataja kuwa ni pamoja na  kukamilisha kwa wakati zoezi la kupitia maombi ya leseni huku akisisitiza zoezi hilo kuendana na upekuzi wa kina juu ya waombaji wa leseni ya haki miliki ya madini ili kujiridhisha na kuhakikisha kwamba wanaopatiwa leseni ni wale tu wenye sifa, vigezo na uwezo wa kuwekeza.

"Zoezi hili lihakikishe kwamba kila anayefanya biashara ya madini ana leseni na leseni hai iliyolipiwa," alisisitiza Kairuki.

Pia, aliishauri Tume kuhakikisha inawadhibiti watu au makampuni ambayo yanashikilia leseni walizopewa kwa muda mrefu bila kuziendeleza kinyume na masharti waliyopewa wakati.

Ushauri mwingine nikuhakikisha kwamba mrefu awadhibiti watu au makapuni ambayo yanashikilia leseni walizopewa kwa muda mrefu bila kuziendeleza kinyume na msharti waliyopewa wakati wa kuidhinishiwa leseni.

Vilevile, alishauri  muhimu wa kuwepo uataratibu wa kufanya ukaguzi wa mara kwa mara kuona maendeleo ya uwekezaji katika migodi ambayo imepatiwa leseni.

"Kwa kufanya hivyo mtaweza kujiridhisha kwamba mlichoahidiwa na mwekezaji ndicho kinachofanyika na pia mtaweza kushughulikia changamoto mapema," alisisitiza Kairuki.

Pamoja na hayo alishauri kuhusu uwezekano wa kuweka utaratibu wa kutoa bei elekezi za madini aina mbalimbali iwe madini ya ujenzi, madini ya viwandani na mengine na kuongeza kuwa, utaratibu huo utasaidia  sana wachimbaji wadogo na wa kati." Zoezi hili liende na kuhakikisha kwamba tunasimamia vyema uwasilishaji wa taarifa za mienendo ya biashara ya madini na uzalishaji," aliongeza Kairuki.

Ushauri mwingine ulitolewa kuwa, Tume iangalie uwezekano wa kuanzisha rejista za uzalishaji unaofanyika na pia kuwa na rekodi za maafisa madini wanaokagua uzalishaji  na uthamini wa madini.

Akizungumzia upande wa vibali alishauri mauzo ya madini nje ya nchi ni vyema yakafanyika kwa mapitio ama vibali ili kuhakikisha panakuwepo maelezo na taarifa za kina za madini yanayosafirishwa kuhusu yalikotoka.

"Vilevile kwa kushirikiana na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama  tuangalie mbinu za kisasa  za kudhibiti utoroshaji wa madini ili kudhibiti biashara haramu ya madini," alisema Waziri Kairuki.

Halikadhalika, alizungumzia kuhusu Serikali kupata mapato stahiki ambapo alishauri kufanyika ukaguzi na uhakiki wa kiasi na ubora wa madini yanayozalishwa na migodi mikubwa, ya kati,  na midogo na kuhakikisha  wachimbaji wadogo ambao wanafanya uchimbaji bila kutambulika wafanyiwe utaratibu ili warasimishwe.

Mwisho alisisitiza kuhusu Tume kuwachukua watumishi watakaoonekana kufaa wa uliokuwa Wakala wa Ukaguzi wa Madini Tanzania (TMAA) kwa kuwa majukumu ya Tume hiyo  yanahitaji weledi, uzalendo na uaminifu wa hali ya juu.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Tume ya Madini Profesa Idrisa Kikula aliwataka watumishi wa Tume kuwa waadilifu na kuonesha weledi kwenye utendaji wao ili kulinda heshima iliyopewa Tume.

Aliongeza kuwa, Tume imepokea kwa dhati maelekezo yote na maangalizo yote muhimu ambayo yameshauriwa kufanyiwa kazi ili sekta ya madini ilete tija iyokuwa kusudiwa.

Pia, aliongeza kuwa, tayari Tume imepokea  taarifa nyingi hasa za migogoro ambayo kiuhalisia inatakiwa kupata ufumbuzi na kuongeza kuwa, Tume itatengeneza kanzidata ya migogoro.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini Dustan Kitandula alisema kuwa, watanzania wana matumaini makubwa na sekta ya madini baada ya kuundwa Tume na kuamini kuwa, itawaondoka kwenye umaskini.

Uzunduzi wa Tume ulifanyika tarehe 30 Mei, 2018 jijini Dodoma. Kwa mujibu wa maelezo ya Waziri Kairuki, Tume inaundwa na Ofisi za madini zilizoko Mikoani, ofisi zitakazokuwa migodini, Maabara na Makao Makuu ya Tume.


Waziri wa Madini Angellah Kairuki katika picha ya Pamoja na       Makamishna wa Tume ya Madini. Wengine ni Naibu Mawaziri wa Wizara ya  Madini na 


Waziri wa Madini Angellah Kairuki katika picha ya Pamoja na       Mawaziri na Naibu Mawaziri kutoka Wizara mbalimbali      walishiriki uzinduzi wa Tume.






Waziri wa Madini Angellah Kairuki kushoto akimkabidhi         Vitendea kazi Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Idrisa     Kikula.

No comments:

Post a Comment