Tuesday, June 5, 2018

Wataalamu wa madini nchini wajifunza uzoefu kutoka Australia


Na Veronica Simba, Dodoma

Wataalam mbalimbali kutoka sekta ya madini nchini wameshiriki warsha maalum iliyotolewa na wataalamu kutoka Australia, kwa lengo la kujifunza uzoefu kutoka nchi hiyo ambayo imepiga hatua kubwa katika sekta husika.

Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko alifungua rasmi warsha hiyo ya siku mbili, Juni 4 jijini Dodoma na kusema kuwa Tanzania inahitaji kujifunza zaidi kutoka nchi zilizofanikiwa katika sekta ya madini kama Australia, ili iweze kukuza zaidi mchango wake katika katika Pato la Taifa.

“Wenzetu Australia, sekta yao ya madini ina mchango mkubwa sana; zaidi ya asilimia 40 kwenye Pato lao la Taifa. Kwa hiyo, tunakutana nao kubadilishana uzoefu, ni namna gani wao wamefanya kuwezesha sekta husika kuchangia kwa kiasi hicho kwenye Pato la Taifa.”

Aidha, Naibu Waziri alisema kuwa, suala muhimu ambalo Wizara ya Madini inalisimamia ni kuhusu usimamizi wa rasilimali za madini.

Alisema kuwa, lengo jingine la warsha hiyo ni kujifunza Australia imefanya nini katika kusimamia na kutatua migogoro kwenye sekta ya madini, ili Tanzania itumie mbinu hizo kutatua migogoro iliyopo kwenye sekta husika.

Biteko alitumia fursa hiyo kuiomba serikali ya Australia kuangalia uwezekano wa kuendesha warsha husika kwa wachimbaji wadogo nchini ili wapate maarifa ya namna bora ya usimamizi wa rasilimali za madini.

Akizungumzia mchango wa sekta ya madini kwenye uchumi wa viwanda, Biteko alieleza kuwa, rasilimali za madini ni tegemeo kubwa katika kukuza uchumi huo.

“Ndiyo maana mtaona kwamba tunayo miradi mikubwa ya makaa ya mawe, ambayo inazalisha nishati ya umeme utakaotumika kwenye viwanda vyetu. Kwa hiyo lazima tuisimamie vizuri,” alifafanua.

Aidha, aliongeza kwamba, Tanzania ina madini mengi ya teknolojia yakiwemo ya Neobium yanayohitajika sana duniani kwa ajili ya viwanda.

Alitaja madini mengine muhimu kwa viwanda kuwa ni Graphite pamoja na Marble, ambayo yote yanapatikana kwa wingi Tanzania.

Kwa upande wake, Kamishna wa Madini Tanzania, Mhandisi David Mulabwa, alisema kuwa, warsha hiyo ni muhimu sana katika kuwaongezea watumishi ujuzi na maarifa kwa ajili ya kukabiliana na changamoto za kisekta.

“Kuna mambo ya mazingira, tozo na kodi mbalimbali katika sekta. Kwa hiyo, jinsi watumishi wanavyokuwa na ujuzi na maarifa, tunaamini watakuwa katika nafasi nzuri ya kufanya ya kufanya maamuzi ambayo yatasaidia kuhakikisha kwamba rasilimali za nchi hii zinalinufaisha Taifa ipasavyo.”

Awali, mmoja wa waratibu wa warsha hiyo, ambaye ni Afisa kutoka Ubalozi wa Australia kutoka Ofisi ya Nairobi, Deanna Simpson, alieleza kuwa; Serikali ya nchi yake imekuwa ikitoa warsha za aina hiyo katika nchi mbalimbali za Afrika, zikiwemo Kenya, Madagascar, Ethiopia na Sudan.

Aidha, aliongeza kuwa, Australia Magharibi ina kampuni zaidi ya 100 zinazoendesha miradi mbalimbali ya madini zaidi ya 350 katika nchi za Afrika takribani 30 ikiwemo Tanzania.

Warsha hiyo ya madini imehitimishwa Juni 5, mwaka huu.


Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko (kushoto), akijadiliana jambo na Mtaalamu wa Madini kutoka Australia, Rick Rogerson, muda mfupi baada ya Naibu Waziri kufungua rasmi warsha ya wataalam wa madini nchini, iliyotolewa na wataalam kutoka Australia; Juni 4 na 5 mwaka huu, jijini Dodoma.


Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini Tanzania, Prof Shukrani Manya (kulia), akisalimiana na wataalamu wa madini kutoka Australia, Danielle Risbey na Rick Rogerson, muda mfupi kabla ya kuanza kwa warsha ya wataalam wa madini nchini, iliyotolewa na wataalam kutoka Australia; Juni 4 na 5 mwaka huu, jijini Dodoma.


Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko (waliokaa-katikati), akiwa katika picha ya pamoja na wataalamu mbalimbali wa madini nchini, walioshiriki warsha maalum iliyotolewa na wataalamu kutoka Australia. Naibu Waziri alifungua rasmi warsha hiyo ya siku mbili, Juni 4 mwaka huu jijini Dodoma.


Kutoka kushoto ni Kamishna wa Madini Tanzania, Mhandisi David Mulabwa; Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko na Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini Tanzania, Prof Shukrani Manya wakijadiliana jambo, wakati wa ufunguzi rasmi wa warsha ya wataalam wa madini nchini, iliyotolewa na wataalam kutoka Australia; Juni 4 na 5 mwaka huu, jijini Dodoma.


Mtaalamu wa Madini kutoka Australia, Rick Rogerson, akiwasilisha mada katika warsha ya wataalam wa madini nchini (hawapo pichani), iliyofanyika Juni 4 na 5 mwaka huu, jijini Dodoma.


Wataalamu mbalimbali wa sekta ya madini nchini, wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zikiwasilishwa na wataalamu wa madini kutoka Australia, katika warsha iliyofanyika Juni 4 na 5 mwaka huu jijini Dodoma.


Wataalamu mbalimbali wa sekta ya madini nchini, wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zikiwasilishwa na wataalamu wa madini kutoka Australia, katika warsha iliyofanyika Juni 4 na 5 mwaka huu jijini Dodoma.


Wataalamu mbalimbali wa sekta ya madini nchini, wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zikiwasilishwa na wataalamu wa madini kutoka Australia, katika warsha iliyofanyika Juni 4 na 5 mwaka huu jijini Dodoma.


Wataalamu mbalimbali wa sekta ya madini nchini, wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zikiwasilishwa na wataalamu wa madini kutoka Australia, katika warsha iliyofanyika Juni 4 na 5 mwaka huu jijini Dodoma.


Wataalamu mbalimbali wa sekta ya madini nchini, wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zikiwasilishwa na wataalamu wa madini kutoka Australia, katika warsha iliyofanyika Juni 4 na 5 mwaka huu jijini Dodoma.

No comments:

Post a Comment