Na Mohamed Saif,
Serikali imewahakikishia
Wananchi wa Tarime wanaostahili kulipwa fidia na Mgodi wa North Mara uliopo wilayani
humo ambao walifanyiwa tathmini kuwa watalipwa.
Naibu Waziri wa
Madini, Stanslaus Nyongo alisema hayo Desemba 28, 2017 wakati wa ziara yake
katika Kijiji cha Nyabichune, Kata ya Matongo Wilayani Tarime kwenye mkutano na
wananchi na wachimbaji wadogo.
Wakizungumza kwa
nyakati tofauti, wananchi wa maeneo hayo walimueleza Naibu Waziri malalamiko
mbalimbali ikiwemo suala la ulipaji wa fidia, ajira, mahusiano duni na mgodi na
mgodi kushindwa kununua bidhaa zinazozalishwa na wananchi wa maeneo hayo.
Akijibu hoja hizo, Naibu
Waziri Nyongo aliuagiza mgodi huo wa North Mara kuhakikisha unawalipa wananchi
fidia wanayostahili. “Haiwezekani mmefanya tathmini halafu baadaye mnageuka
kwamba hamtolipa, ubabaishaji wa aina hiyo haupo maana mlikua mmekwisha waandaa
wananchi kisaikolojia kwamba mtawalipa,” alisema.
Kwa upande mwingine
aliwaonya wananchi wanaofanya udanganyifu kuacha tabia hiyo mara moja kwani
kufanya hivyo kunasababisha malipo ya fidia kuchelewa kwa wananchi
wanaostahili.
“Hapa nimeelezwa
tathmini ya kwanza ilikua na kiasi kidogo cha fidia kilichokuwa kinadaiwa
tofauti na tathmini ya mara ya pili na hapa inaonekana kuna baadhi yenu
wamefanya udanganyifu,” alisema.
Aliwataka wananchi
hao kuwatambua waliofanya udanganyifu ili kuharakisha zoezi la ulipaji wa fidia
kwa mujibu wa sheria na makubaliano.
“Tathmini ya mara ya
pili imeonekana ina kiwango kikubwa, tunaomba ushirikiano wenu kuwabaini
waliojiongeza ili zoezi la ulipaji fidia likamilike kwa wakati bila kuwepo
udanganyifu,” aliagiza Naibu Waziri Nyongo.
Akizungumzia suala la
ajira, Naibu Waziri Nyongo aliuagiza mgodi huo kuhakikisha unatoa kipaumbele
kwa wananchi wa maeneo yanayozunguka mgodi na hapohapo aliwaasa wananchi
watakaonufaika na ajira hizo kufanya kazi kwa uadilifu.
“Ajira zitolewe kwa
wenyeji wenye sifa na nyie ndugu zangu mkipewa kazi fanyeni kwa uadilifu,
msiwaharibie wengine wenye nia ya kufanya kazi,” alisema Nyongo.
Kuhusu suala la
manunuzi ya bidhaa na huduma kutoka kwa wenyeji, Nyongo alisisitiza mgodi
kutumia huduma na bidhaa zinazozalishwa na wenyeji wa hapo jambo ambalo alisema
likifanyika kwa weledi litachangia katika uboreshaji wa mahusiano baina ya
pande hizo mbili.
Aidha, alitoa rai kwa
Halmashauri kuwa fedha wanazopokea za ushuru wa huduma (service levy) kutoka
mgodini hapo ambazo zinatakiwa kuleta maendeleo hapo Nyamongo zirudishwe hapo
kufanya maendeleo.
“Halmashauri isimamie
vema ili kupata ushuru wa huduma kwa kiasi kinachostahili kutoka kwenye mgodi
kwa ajili ya maendeleo,” aliagiza Nyongo.
Naibu Waziri Nyongo
alisisitiza suala la uboreshaji wa mahusiano, umuhimu wa kutii na kufuata
sheria, kuepuka vurugu, amani, usalama na upendo na vilevile mgodi kuachia
maeneo ambayo hayafanyiwi kazi kwa ajili ya uchimbaji mdogo.
No comments:
Post a Comment