Monday, January 22, 2018

Biteko aitaka STAMICO kujitathmini

Na Rhoda James, DSM

Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko amelitaka Shirika la Madini la Taifa  (STAMICO) kujitathmini ili kujua kama linatakiwa kuendelea kuwepo.

Naibu Waziri wa Madini, Biteko ameyasema hayo tarehe 16 Januari, 2018, wakati wa ziara yake Makao Makuu ya STAMICO ambayo ililenga kufahamiana na Bodi, Menejimenti pamoja na Watumishi wa shirika hilo.

Biteko amesema Serikali ililenga kulitumia shirika hilo ili kuhakikisha kuwa linasimamia na kutekeleza miradi mbalimbali ya madini nchini ukiwemo Mgodi wa Buckreef. “Mnazungumzia mradi wa Buckreef mmefanya nini kuhusu mradi huu? amehoji Biteko.

Vilevile, Biteko katika kikao hicho ameitaka STAMICO kuhakikisha inadhibiti utoroshwaji wa madini ya Tanzanite nchini kwa kuhakikisha kuwa inaweka mikakati madhubuti ya kudhibiti utoroshaji huo.

“STAMICO ni mbia katika Kampuni ya TanzaniateOne ni lazima muweke mikakati ya namna gani ya kudhibiti utoroshwaji wa madini haya,” amesema Biteko.
Aidha, amewataka watumishi wa STAMICO kufikiria namna ambayo itawezesha shirika husika kuchangia katika Pato la Taifa kwa kuwa mchango wa Sekta ya Madini bado ni kidogo.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Utafiti na Uchorongaji anaye Kaimu nafasi ya Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO, Alex Rutagwelela akitoa taarifa ya shirika hilo amesema kuwa lengo kuu la STAMICO ni kuhakikisha kuwa inarudi kama ilivyokuwa hapo awali.

Rutagwelela amemweleza Naibu Waziri kuwa, Shirika linafanya shughuli mbalimbali ikiwemo kusimamia na kutekeleza miradi mbalimbali, kutoa ushauri kwa wachimbaji wadogo pamoja na biashara ya kukodisha mitambo ya Uchorongaji.

Ameongeza kuwa, STAMICO inaendelea na uchimbaji wa Makaa ya Mawe katika eneo la Kiwira – Kabulo, Kukarabati maabara ya Makaa ya Mawe ya Kiwira ambayo itatumika kupima ubora wa makaa hayo.


Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya STAMICO Balozi Alexander Muganda amemweleza Naibu Waziri Biteko kuwa, watayafanyia kazi maagizo yote na kumshukuru kwa kutembelea shirika hilo katika ziara ambayo imelenga kuboresha utendaji, kuongeza ubunifu ili  shirika hilo liweze kuchangia zaidi katika pato la Taifa.

Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (wa pili kulia) akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kufika Makao Makuu ya Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) Dar es Salaam kwa lengo la kufahamiana na Bodi, Uongozi na Watumishi wa shirika hilo. Kulia kwake ni Mwenyekiti wa Bodi ya STAMICO Balozi Elexander Muganda, Kamishna wa Madini, Profesa Shukrani Manya ambaye pia ni Kaimu Mtendaji Mkuu wa Tume ya Madini na kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa Utafiti na Uchorongaji, Alex Rutagwelela.
Kamishna wa Madini, Profesa Shukrani Manya ambaye pia ni Kaimu Mtendaji Mkuu wa Tume ya Madini akifafanua jambo katika kikao hicho.
  Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (katikati mbele) akisikiliza mada iliyokuwa ikiwasilishwa na Kaimu Mkurugenzi wa utafiti na Uchorongaji, Alex Rutagwelela wakati wa kikao hicho. Wengine ni Uongozi na Watumishi wa Shirika la STAMICO.

No comments:

Post a Comment