Meneja
Mkuu wa Mgodi wa Dhahabu wa Buckreef, Peter Zizhou (kulia) akielezea teknolojia
ya zamani ya uchenjuaji wa dhahabu kwa Waziri wa Madini, Angellah Kairuki (katikati)
mara alipofanya ziara kwenye mgodi huo uliopo mkoani Geita kwa ajili ya
kujionea maendeleo ya shughuli zake tarehe 27 Oktoba, 2017. Kushoto ni Naibu
Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo.
Waziri
wa Madini, Angellah Kairuki (kulia) akimshukuru
Kaimu Afisa Mtendaji kutoka Kampuni ya
Tanzanian Royalty Exploration, Jeffrey Duval (katikati) mara baada ya
kampuni hiyo kupitia Mgodi wa Buckreef
ulioko mkoani Geita kutoa mchango wa madawati 105 yenye thamani ya shilingi
milioni saba kwa ajili ya shule ya sekondari moja na shule za msingi nne
zilizopo katika kata ya Busanda wilayani
Geita mkoani Geita. Wa pili kulia ni Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo
na kushoto ni Afisa Mtendaji wa Kata ya Busanda, Justa Mabala.
Mmiliki
wa Mgodi wa Busolwa Mining Limited, Christopher Kadeo (wa pili kulia mbele)
akielezea shughuli zinazofanywa na mgodi huo kwa Waziri wa Madini, Angellah
Kairuki (katikati) na Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo ( kushoto mbele)
mara walipofanya ziara katika mgodi huo.
Waziri wa Madini, Angellah Kairuki amesema Serikali inatarajia
kuwasilisha majina ya wananchi 1062 waliofanyiwa tathmini katika eneo
la Kiseme wilayani Geita ili kulipwa fidia kwa ajili ya kupisha
shughuli za uchimbaji madini za Mgodi wa Dhahabu wa Buckreef katika
Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ili kufanyiwa uhakiki na
kubaini uhalali wa umiliki wake kabla ya kuanza kwa taratibu za malipo.
Waziri Kairuki aliyeambatana na Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus
Nyongo ameyasema hayo mapema leo katika Mgodi wa Dhahabu wa Buckreef
uliopo wilayani Geita mkoani Geita mara baada ya kuhitimisha ziara yake
ya siku moja katika mgodi huo ili kujionea maendeleo ya mgodi huo na
kutatua changamoto zake.
Ziara hiyo ni mwendelezo wa ziara zake pamoja na Naibu Waziri wa
Madini, Stanslaus Nyongo katika migodi ya serikali, binafsi na
wachimbaji wadogo katika mikoa ya Kagera na Geita ili kufahamu kwa
undani mafanikio na namna ya kutatua changamoto zilizopo katika sekta
ya madini.
Alisema kuwa, kabla ya kuanza kwa ulipaji wa fidia, ni lazima Wizara
ya Madini ihakikishe majina ya wanaodai fidia yanafikishwa katika
Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa ajili ya kufanyiwa
uhakiki na wataalam wa wizara hiyo ili kuepuka udanganyifu kwenye
umiliki wa ardhi.
Katika hatua nyingine, Kairuki alitaka Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) lenye umiliki wa asilimia 45 katika mgodi huo kwa niaba ya Serikali kuhakikisha linafanya tathmini ya vifaa vyote vinavyotumika katika uchimbaji na uchenjuaji madini pamoja na mikataba kati yake na mbia wake ambaye ni kampuni ya Tanzam 2000 mwenye asilimia 55.
“Mkumbuke kuwa mmepewa dhamana na Serikali ya kusimamia mgodi huu, hivyo ni jukumu lenu kuhakikisha kuwa maslahi ya Taifa yanaangaliwa huku mkifanya kazi kwa ubunifu wa hali ya juu ili uchimbaji ulete tija,” alisema Kairuki.
Wakati huo huo Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo akizungumza katika kikao na uongozi na wafanyakazi wa mgodi wa dhahabu wa Busolwa Mining Limited, alisema kuwa Serikali ipo tayari kuwasaidia wachimbaji wadogo ili uzalishaji wao ulete manufaa kwenye uchumi wa nchi.
Alisema kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imejipanga katika kuhakikisha kuwa wachimbaji wa madini hususan wazawa wanafanya shughuli zao katika mazingira rafiki na kupata faida kubwa na kutoka kwenye lindi la umaskini
Alisisitiza wachimbaji wa madini kufuata kanuni na sheria katika shughuli zao na kuongeza kuwa Serikali kupitia Wizara ya Madini itaendelea kutoa elimu kuhusu kanuni na sheria za madini.
No comments:
Post a Comment