Wednesday, November 22, 2017

Wachimbaji madini Maswa, waomba kufanyiwa utafiti


Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo, akijibu kero mbalimbali za wakazi wa kitongoji cha Mwanguhi kilichopo wilayani Maswa mkoani Simiyu (hawapo pichani) katika mkutano wa hadhara.

Sehemu ya wakazi wa kitongoji cha Mwanguhi kilichopo wilayani Maswa mkoani Simiyu wakifuatilia maelezo yaliyokuwa yanatolewa na Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo (hayupo pichani) katika mkutano wa hadhara

 Mmoja wa wachimbaji wadogo wa madini, Sylivester Fundikira akiwasilisha kero yake mbele ya Naibu  Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo (hayupo pichani). 

Wachimbaji wa madini ya  dhahabu katika wilaya ya Maswa mkoani Simiyu  wameiomba Serikali kupitia Wizara ya Madini kufanya utafiti wa madini katika maeneo yao ili waweze kuwa na uhakika wa  uchimbaji wa madini na uzalishaji wao kuwa na tija.

Wameyasema hayo leo  tarehe 29 Oktoba, 2017 katika ziara ya Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo katika wilaya ya Maswa mkoani Simiyu yenye lengo la kukusanya kero za wananchi mbalimbali hususan katika shughuli za uchimbaji madini.

Akizungumza kwa niaba yao, Sylivester Fundikira alisema kuwa wameunda jumla ya vikundi 30 ambapo kila kikundi kina mashimo yake na kueleza kuwa wamekuwa wakipata changamoto ya upatikanaji   wa madini ya  uhakika kutokana na maeneo yao kutofanyiwa utafiti kwa muda mrefu.
Akijibu kero hiyo Naibu  Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo alisema kuwa Wizara ya Madini kupitia Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) imekuwa ikifanya  tafiti sehemu mbalimbali nchini na kusisitiza  kuwa Serikali  kupitia Wizara ya Madini ipo tayari kuwasaidia.

Alisema Serikali inatambua mchango mkubwa wa wachimbaji wadogo wa madini na kuongeza kuwa imeweka mikakati ya kuwawezesha wachimbaji wadogo wa madini kwa kuwapatia  vifaa kupitia ruzuku ili uchimbaji wao uwe na mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa nchi.
“ Tuna mpango wa kuhakikisha kuwa rasilimali za madini zinakuwa na mchango mkubwa sana katika ukuaji wa uchumi wa nchi, hivyo  tutahakikisha tunasimamia ipasavyo kwa kuhakikisha kuwa mazingira ya uchimbaji madini yanakuwa rafiki,” alieleza Naibu Waziri Nyongo.

Katika hatua nyingine, Nyongo alisema kuwa kazi yake pamoja na  Waziri wa Madini, Angellah Kairuki ni kuhakikisha kuwa sekta ya madini inakua kwa kasi na kuwa na mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa nchi.

Alisema kuwa sekta ya madini imekuwa na changamoto kubwa hususan katika upotevu wa mapato  kutokana na wawekezaji wasio waaminifu na kukwamisha juhudi za serikali katika ukusanyaji wa mapato. Aliendelea kusema kuwa tangu Rais John Magufuli ameanza kupambana na wezi wa rasilimali za madini kumekuwa na mabadiliko makubwa kwa kuwa uzalishaji na mapato umebadilika kutokana na Serikali kuhakikisha kiwango sahihi kinapatikana na kulipiwa kodi serikalini.
Alisema Serikali imeweka Sheria Mpya ya Madini ya mwaka 2017 na kuwataka wachimbaji madini nchini kufuata sheria hiyo pamoja na kanuni zake.

No comments:

Post a Comment