Tuesday, March 26, 2019

Wizara ya Madini yaieleza Kamati ya Bunge utekelezaji wa bajeti kwa mwaka wa fedha 2018/19


Ø YATAJA MAFANIKIO YALIYOPATIKANA

Ø TUME YA MADINI YAPONGEZWA

Wizara ya Madini na Taasisi zake leo Machi 25, imewasilisha kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Taarifa ya Utekelezaji wa Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2018/19, kwa  kipindi  cha kuanzia  mwezi Julai 2018 hadi Februari, 2019.

Akiwasilisha kwa Kamati hiyo taarifa ya utekelezaji wa Wizara, Katibu Mkuu wa Madini Prof. Simon Msanjila pamoja na mambo mengine, ameelezea Mafanikio ya utekelezaji  wa bajeti kuwa ni pamoja na wizara kuvuka lengo la makusanyo ya maduhuli kwa asilimia 5.6 kwa kipindi cha Julai 2018 hadi Februari 2019. Lengo la makusanyo kwa kipindi kinachorejewa lilikuwa shilingi 207,065,336,001 ambapo makusanyo halisi yamekuwa shilingi 218,650,392,234.

Pia, amesema Serikali imeondoa kodi kwenye uchimbaji mdogo kwa kuwafutia kodi ya ongezeko la thamani (VAT 18), na kodi ya zuio
(Withholding tax  asilimia 5).

Pia, amesema kuzinduliwa kwa Soko la Madini katika mkoa wa  Geita ni juhudi za kuhakikisha uwepo wa masoko ya madini na bei inayoridhisha kwa wachimbaji wa madini hususan wachimbaji wadogo ili kudhibiti uuzaji holela na utoroshaji madini hayo.

"Mhe. Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alizindua rasmi soko hilo tarehe 17 Machi, 2019," amesema Prof. Msanjila.

Vilevile, ameeleza kwamba, kufuatia Kongamano lililofanyika nchini China lililojulikana kama China Tanzania Mining Forum, kampuni tatu zimewasilisha maombi ya miradi ya ubia (JV) kati ya watanzania na wageni Ofisi ya TIC Kanda ya Kati kwa ajili ya kupatiwa Cheti cha Vivutio vya Uwekezaji kwenye ujenzi wa viwanda vya kuchataka madini ya Graphite. Miradi hiyo inatarajiwa kuwekeza zaidi ya Dola za Marekani milioni 30 na kuzalisha ajira mpya 600 itakapokamilika.

Naye, Waziri wa Madini Waziri wa Madini Doto Biteko, akizungumza katika kikao hicho, ameishukuru Kamati hiyo kwa kuendelea kuisimamia na kuishauri vizuri na kueleza kwamba, Dira Kuu ya wizara ni kuongeza mchango kwenye uchumi wa nchi unaotokana na rasilimali madini.

Pia, Waziri Biteko ameiomba Kamati hiyo kuendelea kuishauri wizara ikiwemo kuikosoa kwa lengo la kuwezesha kuongeza tija zaidi kwenye sekta ya madini.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini Dustan Kitandula, amepongeza  jitihada zilizofanywa na wizara hususan kwa kuwezesha mkutano wa Kisekta baina ya serikali na wadau wa madini uliofanyika Januari 22 mwaka huu chini ya Uenyekiti wa Rais wa Jamhuri wa Muungano  wa Tanzania Dkt. John Magufuli na kueleza kwamba, mkutano huo ulifungua ukurasa mpya wa ushirikiano kati ya Serikali na wadau na hivyo kuutaka ushirikiano huo kuendelezwa ili uwezeshe kuendeleza sekta ya madini nchini.

Amesema matarajio ya Rais Magufuli kwenye sekta ya madini ni makubwa na hivyo kutaka jitihada zaidi kufanyika ili kukidhi maratajio hayo.

Aidha, wakichangia hoja kwa nyakati tofauti, wajumbe wa Kamati hiyo wameipongeza Tume ya Madini kwa ukusanyaji maduhuli na kwa utekelezaji wa majukumu yake ikiwemo ukaguzi migodini.

No comments:

Post a Comment