Wednesday, January 16, 2019

Naibu Waziri aagiza wanunuzi haramu wa dhahabu Ulata kukamatwa


Na Asteria Muhozya,

Kufuatia kukaidi Wito wa kuonana na Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo na Mkuu wa Wilaya ya Iringa Richard Kasesela kutokana na kufanya ununuzi haramu wa madini ya dhahabu ikiwemo kufadhili uchimbaji haramu, Naibu Waziri Nyongo amevitaka vyombo vya  Ulinzi na Usalama mkoani Iringa kuwakamata Mansoor Almasi na Jacob Mwapinga iwapo watashindwa kuripoti wenyewe katika Mamlaka zinazohusika.

Naibu Waziri Nyongo ametoa agizo la kukamatwa wahusika hao baada ya kukiuka agizo la kuonana na viongozi hao  kwa hiari ambapo walielekezwa kuonana na Naibu Waziri na Mkuu wa Mkoa  Januari 15.
Pia, kabla ya wito wa Naibu Waziri, awali, wahusika hao walitakiwa kuonana na Mkuu wa Wilaya ya Iringa wakiwemo Maafisa Madini kwa ajili ya kuupatia suluhisho mgogoro huo katika mgodi wa dhahabu wa Ulata, kijiji cha Ulata wilaya ya Iringa unaomilikiwa na Ibrahimu Msigwa.

Naibu Waziri Nyongo alibaini kuwa Mansoor na Mwapinga wanafanya ununuzi wa madini  kinyume cha Sheria  ikiwemo kufadhili  shughuli za uchimbaji katika mgodi ambao siyo wamiliki wake.

Pia, Naibu Waziri ameelekeza baada ya  wahusika hao kukamatwa wanatakiwa kutoa maelezo  kueleza ni lini watalipa kodi wanazodaiwa na serikali  baada ya kufanya shughuli hizo bila kulipa kodi.

Akizungumza  katika mkutano wa hadhara na wachimbaji hao, Naibu Waziri Nyongo aliwaeleza kuwa, Serikali inamtambua Ibrahimu Msigwa kama mmiliki halali baada ya kuwa na vibali vya kumiliki leseni ya mgodi huo na hivyo kutoa wito wa kuonana na pande zote ili kuhakikisha  kuwa anatoa suluhisho la mgogoro uliopo baina ya Msigwa, Mansoor, Mwapinga na wachimbaji.

Akihitimisha ziara yake mkoani Iringa Januari 15, Naibu Waziri Nyongo amesema kuwa, amebaini ukwepaji mkubwa wa kodi katika migodi  ya Ulata na  Nyakavangala.

Amesema wamiliki wa leseni wanaotumia mrabaha kwa ajili ya kufanya masuala mengine ya kijamii wanakiuka taratibu na kueleza kuwa, fedha za kufanyia shughuli za maendeleo zinapaswa kutoka katika fedha za Uwajibikaji kwa jamii ambazo halmashauri zinapanga kupitia Baraza la Madiwani.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Richard Kasesela amesema wahisika  Mwapinga na Almasi wana kiburi na kwamba waliitwa kwa ajili ya kuongea ili ku[ata fursa ya kujieleza na a kueleza ni lini watalipa mrabaha  lakini wamekaidi hivyo kinachofuatia ni wahusika kukamatwa.

Naibu Waziri Nyongo alifanya ziaea katka mgodi wa Ulata Janauri 14 akilenga kukagua shughuli za uchimbaji madini katika mgodi huo ikiwemo kutatua mgogoro uliokuwep katika mgodi huo baina ya mmiliki halali Ibrahimu Msingwa, wanunuzi  haramu  wa madini hayo Mansoor Almasi na Jacob Mwapinga.

Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo (katikati) akioneshwa jambo na wachimbaji katika mgodi wa Nyakavangala unaomilikiwa na Thomas Masuka and Partners.  Naibu Waziri alifika mgodini hapo kukagua hali ya uchimbaji madini inavyoendelea.

Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo, akikagua moja ya mgodi  katika mgodi wa Nyakavangala wakati wa ziara yake mgodini hapo. Wa tatu kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Richard Kasesela.

Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo akimweleza jambo mmoja wa wachimbaji wakati akikagua mazingira ya uchimbaji madini katika mgodi wa Nyakavangala. Wanaomfuata ni baadhi ya wachimbaji wadogo wanaochimba katika mgodi huo.

Naibu Waziri wa Madini Stansaus Nyongo akisisitiza jambo wakati wa ziara yake ya kukagua mgodi wa Nyakavangala. Nyuma yake ni Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Richard Kasesela.

Mkuu wa Wilaya ya Iringa Richard Kasesela akimwonesha jambo Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo wakati wa ziara yake ya kukagua migodi ya Nyakavangala.

No comments:

Post a Comment