Tuesday, July 31, 2018

Nyongo aiagiza TRA kuchunguza Kiwanda cha Goodwill katika ulipaji wa mrabaha serikalini


Na Zuena Msuya, Pwani

Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo, ameiagiza Mamlaka ya Mapato Tanzania kwa kushirikiana na maafisa madini nchini( TRA) kuchunguza na fuatilia kiwanda cha Goodwill  namna ya ulipaji wake  wa  mrabaha na tozo mbalimbali  serikalini kutokana na aina mbalimbali ya madini wanayotumia yakiwemo Kaolin katika uzalishaji wa bidhaa zake.

Madini ya Kaolin hutumika kwa kiasi kikubwa katika kutengeneza bidhaa mbalimbali zikiwepo Malumalu( Tiles), rangi za nyumba, karatasi, n.k.

Nyongo alitoa agizo hilo alipotembelea kiwanda hicho cha Goodwill  wakati akihitimisha ziara yake ya kukagua shughuli za uchimbaji wa madini ya ujenzi katika  ya Wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani, Julai 26, 2018 ambapo katika ziara hiyo alipata fursa ya kutembelea maeneo ya uchimbaji chumvi na katika kiwanda cha kutengeneza chimvi aina ya NEEL.

Nyongo alieleza kuwa , mara baada ya kutembelea kiwanda hicho, hakuridhishwa na majawabu aliyokuwa akipewa na uongozi wa kiwanda hicho juu ya mahesabu ya manunuzi ya madini kaolin, matumizi ya madini hayo katika uzalishaji wa bidhaa zake, pamoja na uwazi wa ulipaji wa mrabaha na tozo mbalimbali zilizowekwa kwa mujibu wa sheria ya madini, tangu kuanzishwa kwa kiwanda hicho mwezi April mwaka jana.

Hata hivyo aliweka wazi kuwa bei elekezi ya serikali katika uuzaji wa madini ya ujenzi,hasa mchanga ni shilingi elfu kumi( 10,000) kwa tani.
Aidha, Nyongo alishangazwa na bei ya madini ya Kaolin yanayotengeneza malumalu( tiles) kuwa ni shilingi elfu  tatu (3,000) kwa tani na mrabaha unaolipwa ni  3% ya bei kitu ambacho si sahihi, na baada ya kupiga hesabu za haraka waligundua kuwa, tani moja ya Kaolin ilipaswa kuuzwa shilingi 35,000, hivyo  serikali ingepata mrabaha wa shilingi 1,500  kutokana na ile 3% , tofauti na ilivyo sasa serikali inapata mrabaha wa shilingi Tisini (90) katika kila tani ya kaolin inayouzwa, kitu alichosema kuwa ni wizi.

Kutokana mkanganyiko huo aliwaagiza  Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kwenda kufanya mahesabu katika kiwanda cha Goodwill ili kufahamu wanunua au waandika  shilingi ngapi kwa tani ikiwa ni gharama za uzalishaji wa malumalu ( tiles),ili ikifahamika bei halisi ya tani moja, Wizara ya Madini itaanza kutoza mrabaha wa 3% katika kila mahesabu waliokuwa wakiyapeleka TRA.

" unaweza kukuta wamepeleka mahesabu makubwa TRA, lakini katika uchimbaji waandika wamenunua shilingi elfu 3 (3000) hii haiingii akilini kabisa, kila mtanzania anajua Malumalu( tiles) zinauzwa kwa bei juu sana na wakati mwingine watu wanaagiza kutoka nje kupunguza gharama, halafu madini ya kaolin ambayo ni malighafi muhimu katika kuzitengeza malumalu hizo yanauzwa shilingi elfu tatu kwa tani , huo ni wizi mkubwa na haiwezekani", alisisitiza Nyongo.

Alisisitiza kuwa endapo kiwanda hicho kitagundulika kukwepa kodi, kitalazimika kulipa fedha zote ambazo zimepotea katika kipindi chote cha uzalishaji na endapo watashindwa kufanya hivyo,sheria itachukuwa mkondo wake.

Tangu kiwanda hicho kianzishwe mwezi April mwaka jana hadi sasa, kumbukumbu zinaonyesha kuwa wametumia tani elfu sabini( 70,000) za madini ya Kaolin, kwa gharama ya shilingi milioni 6 na laki tatu,      (6,300,000) tu, ila kwa bei haraka iliyopigwa pale na wataalam inaonyesha kuwa zaidi ya shilingi milioni sabini ( 70,000,000,) zimepotea , hivyo wataalamu wa Wizara ya Madini kwa kushirikiana na TRA  wameagizwa kufuatilia jambo hilo kwa haraka na umakini mkubwa ili kuipatia serikali mapato stahiki.

Katika hatua nyingine, Nyongo alipiga marufuku uchimbaji wa mchanga na vifusi katika jiji la Dar es salaam, na kuwaagiza wachimbaji kwenda katika maeneo yalioanishwa katika Mkoa wa Pwani.

Alisisitiza kuwa Mkoa wa Pwani unamaeneo mengi yenye madini ya ujenzi ambayo yakichimbwa yanatosheleza majitaji ya mchanga na kokoto katika jiji la dar es salaam na mikoa mingine, hivyo wachimbaji wazingatie sheria za uchimbaji madini hayo.

Sambamba na hilo aliwaagiza Wakuu wa Wilaya zote wenye maeneo ya uchimbaji wa madini ujenzi pamoja na chumvi, kukamata wafanyabiashara na wachimbaji wa madini hayo wnaofanya kazi hiyo bila kufuata sheria ya madini ikiwemo kutosha madini hayo na kukwepa kulipa mrabaha na tozo mbalimbali serikalini na katika halmashauri.

Vilevile, alisema kuwa kila lori litakalokuwa limepakia madini mchanga lazima liwe na stakabadhi ya vocha inayoonyesha kuwa madini hayo yamelipiwa stahili zote zinazotakiwa kwa mujibu wa sheria ya madini.

Pia aliwaagiza maafisa madini kuangalia utaratibu bora utakaofaa kutumika katika kulipa tozo mbalimbali pamoja na mrabaha ikiwezekana zilipwe kwa mfumo wa kieletroniki ili kukwepa wafanyabiashara wasio waaminifu.


Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo, akiwa katika kiwanda cha goodwill. 

Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo (katikati) akikagua chumvi iliyovunwa tayari kupelekwa kiwandani. 

Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo,(katikati) akipata maelezo alipotembelea kiwanda cha kuzalisha chumvi katika wilaya ya Mkuranga.  

No comments:

Post a Comment