Thursday, March 1, 2018

Manufaa ya madini ni kwa watanzania wote–Biteko


Na Mohamed Saif, Rukwa

Serikali imewataka Wawekezaji kwenye Sekta ya Madini Nchini kutawanya manufaa ya shughuli zao za uchimbaji madini kwa Watanzania.

Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko ametoa wito huo 23 Februari, 2018 alipofanya ziara kwenye Mgodi wa Makaa ya Mawe wa Edenville Tanzania Ltd uliopo katika Kijiji cha Mkomolo, Wilaya ya Nkasi Mkoani Rukwa. 

Katika ziara hiyo, alikagua shughuli zinazofanyika mgodini hapo na kuzungumza na wafanyakazi na wananchi wa vijiji jirani na mgodi huo ambapo masuala mbalimbali yalijadiliwa ikiwemo manufaa ya mgodi kwa wananchi.

Biteko alisema Sheria mpya ya Madini inamtaka Mwekezaji ahakikishe huduma zote za muhimu zinazopatikana hapa nchini azipate hapa hapa Tanzania badala ya kuagiza kutoka nje ya nchi ili manufaa yatokanayo na shughuli zake yawafaidishe Watanzania wenyewe.

"Kama ni utoaji wa huduma za chakula, mbogamboga, vifaa na hata huduma za kitaalam zinazoweza kufanywa na watanzania zifanywe na wazawa ili kusudi manufaa yake tuyapate," alisema Biteko.

Biteko aliupongeza mgodi huo kwa hatua iliyochukua ya kutumia Wakandarasi Wazalendo ambao alielezwa wamesaidia kupunguza gharama za uendeshaji wa shughuli za mgodi ilikinganishwa na kutumia wakandarasi wa nje ambao mara nyingi gharama zao zinakua juu.

Akizungumzia suala la ajira, Biteko alisisitiza kuwa shughuli zote ambazo Watanzania wanazimudu zisitolewe kwa wageni na kwamba kipaumbele cha kwanza wapewe wananchi waishio katika vijiji vya jirani na migodi.

Aidha, Biteko aliwataka Watanzania wanaonufaika na ajira migodini kuhakikisha wanafanya kazi kwa uaminifu ili kuepusha migogoro na wawekezaji na wakati huo huo  kutunza heshima ya Taifa.

Naibu Waziri Biteko vilevile alisema kuwa Mwekezaji anawajibika kwa jamii kisheria kupitia mpango wa Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) ambayo inamtaka mwekezaji kusapoti miradi ya maendeleo inayofanyika kwenye maeneo ulipo mgodi.

Biteko vilevile alipiga marufuku Halmashauri zenye migodi kutumia Tozo hizo kwa manufaa binafsi ikiwemo kulipana posho badala yake zitumike kuanzishia miradi endelevu kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

"Tozo inayolipwa kwa Halmashauri itumike kuanzishia Miradi endelevu na yenye kuoneka ili hata wajukuu zetu hapo baadaye waje kunufaika na madini yanayochimbwa sasa," alisema Biteko(sustainable & visible projects)

Kwa upande mwingine Biteko alimuagiza Afisa Madini, Mhandisi Juma Sementa afuatilie ahadi zilizotolewa na Mgodi huo wa Edenville Tanzania Ltd kwa Vijiji vinavyozunguka mgodi huo kupitia mpango wake wa CSR sambamba na kupitia mikataba ya ajira kwa wafanyakazi.

"Afisa Madini unapokuja kukagua Mgodi hakikisha unapitia Mikataba ya ajira kwa wafanyakazi ili ujiridhishe kama inakidhi matakwa ya Sheria," aliagiza Naibu Waziri Biteko.

Biteko alifanya ziara ya kutembelea migodi na kuzungumza na wachimbaji ili kujadiliana nao juu ya changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo kwenye utekelezaji wa majukumu yao kwa lengo la kuzitafutia ufumbuzi.


Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko akizungumza na wafanyakazi wa Mgodi wa Makaa ya Mawe wa Edenville Tanzania Ltd na wananchi wa vijiji vinavyozunguka mgodi huo (hawapo pichani) uliopo katika Wilaya ya Nkasi Mkoani Rukwa.

Baadhi ya wafanyakazi wa Mgodi wa Makaa ya Mawe wa Edenville Tanzania Ltd na wananchi wa vijiji vinavyozunguka mgodi huo uliopo katika Wilaya ya Nkasi Mkoani Rukwa wakimsikiliza Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (hayupo pichani). 

Baadhi ya wananchi wa vijiji vinavyozunguka mgodi wa Makaa ya Mawe wa Edenville Tanzania Ltd uliopo katika Wilaya ya Nkasi Mkoani Rukwa wakimsikiliza Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (hayupo pichani). 

No comments:

Post a Comment