Na Mohamed Saif, Rukwa
Serikali
imewataka Wawekezaji kwenye Sekta ya Madini Nchini kutawanya manufaa ya
shughuli zao za uchimbaji madini kwa Watanzania.
Naibu
Waziri wa Madini, Doto Biteko ametoa wito huo 23 Februari, 2018 alipofanya
ziara kwenye Mgodi wa Makaa ya Mawe wa Edenville Tanzania Ltd uliopo
katika Kijiji cha Mkomolo, Wilaya ya Nkasi Mkoani Rukwa.
Katika
ziara hiyo, alikagua shughuli zinazofanyika mgodini hapo na kuzungumza na
wafanyakazi na wananchi wa vijiji jirani na mgodi huo ambapo masuala mbalimbali
yalijadiliwa ikiwemo manufaa ya mgodi kwa wananchi.
Biteko
alisema Sheria mpya ya Madini inamtaka Mwekezaji ahakikishe huduma zote za
muhimu zinazopatikana hapa nchini azipate hapa hapa Tanzania badala ya kuagiza
kutoka nje ya nchi ili manufaa yatokanayo na shughuli zake yawafaidishe
Watanzania wenyewe.
"Kama
ni utoaji wa huduma za chakula, mbogamboga, vifaa na hata huduma za kitaalam
zinazoweza kufanywa na watanzania zifanywe na wazawa ili kusudi manufaa yake
tuyapate," alisema Biteko.
Biteko
aliupongeza mgodi huo kwa hatua iliyochukua ya kutumia Wakandarasi Wazalendo
ambao alielezwa wamesaidia kupunguza gharama za uendeshaji wa shughuli za mgodi
ilikinganishwa na kutumia wakandarasi wa nje ambao mara nyingi gharama zao
zinakua juu.
Akizungumzia
suala la ajira, Biteko alisisitiza kuwa shughuli zote ambazo Watanzania
wanazimudu zisitolewe kwa wageni na kwamba kipaumbele cha kwanza wapewe
wananchi waishio katika vijiji vya jirani na migodi.
Aidha,
Biteko aliwataka Watanzania wanaonufaika na ajira migodini kuhakikisha
wanafanya kazi kwa uaminifu ili kuepusha migogoro na wawekezaji na wakati huo
huo kutunza heshima ya Taifa.
Naibu
Waziri Biteko vilevile alisema kuwa Mwekezaji anawajibika kwa jamii kisheria
kupitia mpango wa Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) ambayo inamtaka mwekezaji
kusapoti miradi ya maendeleo inayofanyika kwenye maeneo ulipo mgodi.
Biteko
vilevile alipiga marufuku Halmashauri zenye migodi kutumia Tozo hizo kwa
manufaa binafsi ikiwemo kulipana posho badala yake zitumike kuanzishia miradi
endelevu kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.
"Tozo
inayolipwa kwa Halmashauri itumike kuanzishia Miradi endelevu na yenye kuoneka
ili hata wajukuu zetu hapo baadaye waje kunufaika na madini yanayochimbwa
sasa," alisema Biteko(sustainable & visible projects)
Kwa upande
mwingine Biteko alimuagiza Afisa Madini, Mhandisi Juma Sementa afuatilie ahadi
zilizotolewa na Mgodi huo wa Edenville Tanzania Ltd kwa Vijiji
vinavyozunguka mgodi huo kupitia mpango wake wa CSR sambamba na kupitia
mikataba ya ajira kwa wafanyakazi.
"Afisa
Madini unapokuja kukagua Mgodi hakikisha unapitia Mikataba ya ajira kwa
wafanyakazi ili ujiridhishe kama inakidhi matakwa ya Sheria," aliagiza
Naibu Waziri Biteko.
Biteko alifanya
ziara ya kutembelea migodi na kuzungumza na wachimbaji ili kujadiliana nao juu
ya changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo kwenye utekelezaji wa majukumu
yao kwa lengo la kuzitafutia ufumbuzi.
No comments:
Post a Comment