Tuesday, February 27, 2018

Biteko atangaza kiama kwa waliohujumu ruzuku


Serikali imetoa onyo kali kwa waliojinufaisha na kutumia ruzuku ya uchimbaji madini kinyume na makusudio yake ambao hadi sasa hawajarejesha licha ya kutakiwa kufanya hivyo.

Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko alitoa onyo hilo Februari 26, 2018 kwenye mkutano na wananchi na wachimbaji wadogo wa madini katika kijiji cha Isanga, Kata ya Lusu Wilaya ya Nzega.

Awali kabla ya kutoa onyo hilo, wachimbaji hao waliiomba Serikali kuwapatia ruzuku ili iwasaidie katika shughuli zao za uchimbaji madini ndipo Naibu Waziri Biteko alipoweka bayana suala hilo la ruzuku.

Alisema Serikali ilisimamisha utoaji wa ruzuku kwa wachimbaji wadogo wa madini nchini baada ya kubaini kwamba imeshindwa kuleta mafanikio yaliyokusudiwa na kwamba ilikwishaagiza wale wote waliojipatia ruzuku na kuitumia kinyume na makusudio wanapaswa kuirejesha mara moja vinginevyo hatua kali za kisheria zitachukuliwa.

“Wapo ambao tayari wameanza kurejesha na wengine bado hawajafanya hivyo. Ninawahakikishia wale ambao bado, tutawachukulia hatua kali za kisheria,” alisema Biteko.

Alisema haiwezekani watu wachache wasiokuwa na huruma kwa wanyonge wakatumia fedha ya Watanzania kinyume na makusudio yake.

Biteko alisema kuwa lengo la Serikali la utoaji wa ruzuku lilikuwa ni kuhakikisha wachimbaji wadogo wa madini nchini wanaweza kuendeleza machimbo yao kwa kufanya shughuli zenye tija kwao na Taifa kwa ujumla hata hivyo, makusudio hayo hayakufikiwa kama ilivyotarajiwa.

Alibainisha kuwa Serikali inakuja na mpango mwingine wa kuwasaidia wachimbaji wadogo kupata manufaa kutokana na shughuli zao lakini sio kuwapatia fedha kama ilivyokuwa hapo awali. “Tunanunua vifaa vya uchimbaji ambavyo vitatumika kuwasaidia na sio kuwapatia fedha,” alisema Biteko.

Aidha, Biteko aliwataka wachimbaji kote nchini kujiunga kwenye vikundi ili kujipatia manufaa mbalimbali ikiwemo urahisi wa kupata huduma za kifedha, kukopesheka na kuelimishwa njia bora na sahihi ya uchimbaji.

Alisema wachimbaji watakapojiunga wataweza kuwa na uchimbaji wenye tija na hivyo kutoa ajira nyingi kwa Watanzania wenzao, kulipa ushuru na tozo mbalimbali za Serikali na hivyo kujiletea maendeleo wao binafsi lakini pia maendeleo kwa Taifa kwa ujumla.

Katika ziara hiyo, Naibu Waziri Biteko aliambatana na mwenyeji wake Mbunge wa Jimbo la Nzega Vijijini na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamis Kigwangala ambapo walitembelea maeneo ya Chuo cha Dodoma Kampasi ya Nzega (MRI) ambapo zamani palikuwa ni mgodi wa Reolute.

Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (kulia) akikagua mazingira ya Chuo cha Madini Dodoma, Kampasi ya Nzega ili kujionea hali ya Kampasi hiyo.

Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Isanga, Kata ya Lusu Wilaya ya Nzega (hawapo pichani).

Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (kushoto) akiongozana na mwenyeji wake Mbunge wa Nzega Vijijini na Waziri wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hamis Kigwangala (kulia) walipofanya ziara kwenye Chuo cha Madini Dodoma, Kampasi ya Nzega ili kujionesa hali ya Kampasi hiyo.

Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (wa pili kushoto) akikagua mazingira ya Chuo cha Madini Dodoma, Kampasi ya Nzega.

Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (katikati) alipotembelea Chuo Cha Madini Dodoma, kampasi ya Nzega.

No comments:

Post a Comment