ü Naibu
Waziri Biteko apongeza wachimbaji kuunganishwa na huduma umeme
Na
Veronica Simba, Geita
Wizara ya
Nishati inatekeleza mkakati wa kuwaunganishia umeme wa uhakika wachimbaji
wadogo wa madini kote nchini, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono jitihada za Rais
John Magufulu kuiwezesha sekta hiyo izalishe kwa tija kwa manufaa yao binafsi
na ya Taifa kwa ujumla.
Akizungumza
katika hafla ya uwekaji jiwe la msingi wa kiwanda cha kuchenjua dhahabu,
kinachomilikiwa na kampuni ya Padalu, kijijini Lumasa, Chato; Waziri wa Nishati
ambaye pia ni Mbunge wa eneo hilo, Dkt Medard Kalemani, alisema serikali
imefunga transfoma tano zenye uwezo wa KVA 400 hadi 1,000 ili kuwawezesha
wachimbaji wadogo wa Geita kuzalisha kwa tija.
“Umeme huu
mkubwa utawawezesha wachimbaji kuchimba ,kuchenjua na kuongeza thamani dhahabu
yao ili kuiongezea thamani, iwapatie faida na waweze kulipa kodi na mrabaha
serikalini,” alisema.
Akieleza
zaidi, Waziri Kalemani alisema yako maeneo mkoani humo ambayo bado hayajafikiwa
na huduma hiyo lakini akabainisha kuwa utaratibu wa kufunga transfoma nyingine
tano zenye uwezo uleule, unafanyika ili kuyafikia maeneo ya wachimbaji
yaliyosalia ikiwemo Mbogwe na Nyakafuru.
Aidha, alifafanua
kuwa, umeme uliounganishwa kwa ajili ya kiwanda hicho cha kuchenjua dhahabu,
utawanufaisha pia wananchi wa maeneo jirani ambao wataanza kuunganishiwa huduma
hiyo kuanzia wiki ijayo.
Waziri pia
alitumia fursa hiyo kufafanua kuhusu gharama za umeme katika maeneo ya vijijini
ambapo alibainisha kuwa serikali imedhamiria wananchi wa vijijini watozwe
shilingi 27,000 tu kwa ajili ya huduma ya kuunganishiwa umeme.
“Wananchi
maeneo yote ya vijijini nchi nzima, gharama za kuunganishiwa umeme ni shilingi
27,000 tu. Msikubali kutozwa zaidi. Iwe ni umeme wa REA au wa TANESCO, gharama
ni hiyo na siyo zaidi,” alisisitiza Waziri.
Kwa upande
wake, Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko ambaye alikuwa Mgeni Rasmi katika
hafla hiyo alipongeza jitihada ambazo zimekuwa zikifanywa na Wizara ya Nishati
katika kuhakikisha wachimbaji madini wadogo nchini wanakuwa na uchimbaji wenye
tija kwa kuwapelekea huduma ya umeme.
Awali,
uongozi wa kiwanda hicho cha uchenjuaji dhahabu ulieleza kuwa, ujenzi wake
ulifanyika kufuatia agizo la Rais Magufuli la kuwataka wachimbaji kuyaongeza
thamani madini yao hapa nchini kabla ya kusafirisha nje ya nchi.
No comments:
Post a Comment