Friday, January 4, 2019

Nishati waunga mkono jitihada za Rais kuwezesha wachimbaji madini wadogo


ü Naibu Waziri Biteko apongeza wachimbaji kuunganishwa na huduma umeme

 Na Veronica Simba, Geita

Wizara ya Nishati inatekeleza mkakati wa kuwaunganishia umeme wa uhakika wachimbaji wadogo wa madini kote nchini, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono jitihada za Rais John Magufulu kuiwezesha sekta hiyo izalishe kwa tija kwa manufaa yao binafsi na ya Taifa kwa ujumla.

Akizungumza katika hafla ya uwekaji jiwe la msingi wa kiwanda cha kuchenjua dhahabu, kinachomilikiwa na kampuni ya Padalu, kijijini Lumasa, Chato; Waziri wa Nishati ambaye pia ni Mbunge wa eneo hilo, Dkt Medard Kalemani, alisema serikali imefunga transfoma tano zenye uwezo wa KVA 400 hadi 1,000 ili kuwawezesha wachimbaji wadogo wa Geita kuzalisha kwa tija.

“Umeme huu mkubwa utawawezesha wachimbaji kuchimba ,kuchenjua na kuongeza thamani dhahabu yao ili kuiongezea thamani, iwapatie faida na waweze kulipa kodi na mrabaha serikalini,” alisema.

Akieleza zaidi, Waziri Kalemani alisema yako maeneo mkoani humo ambayo bado hayajafikiwa na huduma hiyo lakini akabainisha kuwa utaratibu wa kufunga transfoma nyingine tano zenye uwezo uleule, unafanyika ili kuyafikia maeneo ya wachimbaji yaliyosalia ikiwemo Mbogwe na Nyakafuru.

Aidha, alifafanua kuwa, umeme uliounganishwa kwa ajili ya kiwanda hicho cha kuchenjua dhahabu, utawanufaisha pia wananchi wa maeneo jirani ambao wataanza kuunganishiwa huduma hiyo kuanzia wiki ijayo.

Waziri pia alitumia fursa hiyo kufafanua kuhusu gharama za umeme katika maeneo ya vijijini ambapo alibainisha kuwa serikali imedhamiria wananchi wa vijijini watozwe shilingi 27,000 tu kwa ajili ya huduma ya kuunganishiwa umeme.

“Wananchi maeneo yote ya vijijini nchi nzima, gharama za kuunganishiwa umeme ni shilingi 27,000 tu. Msikubali kutozwa zaidi. Iwe ni umeme wa REA au wa TANESCO, gharama ni hiyo na siyo zaidi,” alisisitiza Waziri.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko ambaye alikuwa Mgeni Rasmi katika hafla hiyo alipongeza jitihada ambazo zimekuwa zikifanywa na Wizara ya Nishati katika kuhakikisha wachimbaji madini wadogo nchini wanakuwa na uchimbaji wenye tija kwa kuwapelekea huduma ya umeme.

Awali, uongozi wa kiwanda hicho cha uchenjuaji dhahabu ulieleza kuwa, ujenzi wake ulifanyika kufuatia agizo la Rais Magufuli la kuwataka wachimbaji kuyaongeza thamani madini yao hapa nchini kabla ya kusafirisha nje ya nchi.


Sehemu ya umati wa wananchi wakimsikiliza Waziri wa Nishati ambaye pia ni Mbunge wa Chato, Dkt Medard Kalemani (hayupo pichani), wakati wa hafla ya uwekaji jiwe la msingi katika kiwanda cha kuchenjua dhahabu cha Padalu kilichopo jimboni humo, Chato Geita, Januari 2, 2019.

Msimamizi wa Kiwanda cha kuchakata dhahabu cha Padalu, kilichopo Chato Geita, Abel Lucas (kushoto), akitoa maelezo jinsi kinavyofanya kazi kwa Waziri wa Nishati ambaye pia ni Mbunge wa Chato, Dkt Medard Kalemani (wa kwanza kulia) pamoja na Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko (wa pili – kulia), wakati wa hafla ya uwekaji jiwe la msingi wa kiwanda hicho, Januari 2, 2019.

Waziri wa Nishati ambaye pia ni Mbunge wa Chato, Dkt Medard Kalemani (kushoto) na Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (kulia), wakifungua kitambaa maalum kilichofunika jiwe la msingi la kiwanda cha uchenjuaji dhahabu cha Padalu, kilichopo Chato Geita, kuashiria uzinduzi rasmi. Hafla hiyo ilifanyika Januari 2, 2019.

Waziri wa Nishati ambaye pia ni Mbunge wa Chato, Dkt Medard Kalemani (katikati), akisalimiana na Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko (kushoto), walipowasili kwenye hafla ya uwekaji jiwe la msingi katika kiwanda cha kuchenjua dhahabu cha Padalu kilichopo Chato Geita, Januari 2, 2019.Kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Chato, Mhandisi Msafiri Mtemi.

No comments:

Post a Comment