Watumishi wa Wizara ya Madini wameungana na watumishi wengine nchini
kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli kwa
uamuzi wake wa kutangaza kutumika kwa kikokotoo cha zamani cha mafao ya
Wastaafu.
Watumishi hao wameungana katika maandamano ya amani yaliyoanzia katika
Ofisi za Bunge na kupokelewa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Kassim Majaliwa katika Bustani za Nyerere Square, jijini
Dodoma.
Akizungumza na watumishi kutoka sekta mbalimbali, Waziri Mkuu Majaliwa
amesema Serikali itaendelea kushirikiana na Vyama vya Wafanyakazi katika hatua
zote za majadiliano ya suala hilo hadi pale pande zote zitakaporidhika.
Ameongeza kuwa, maombi yaliyowasilishwa na Shirikisho la Vyama vya
Wafanyakazi nchini (TUCTA) yameanza kufanyiwa kazi na mengine yanaendelea
kufanyiwa kazi.
Akizungumzia ombi la mishahara mipya ya wafanyakazi amesema Tume
ya Mishahara na Motisha inaendelea kulifanyia kazi suala hilo na pindi
litakapokamilika, taarifa itatolewa.
Kuhusu madeni ya watumishi amesema serikali inaendelea kulipa madeni
hayo ikiwemo malimbikizo mbalimbali ya watumishi.
Kuhusu kupandishwa madaraja, amesema tayari Ofisi ya Rais
Menejimenti ya Utumishi wa Umma imeanza kushughulikia suala hilo ambapo
tayari utekelezaji umekwisha anza kwa baadhi ya sekta na kuongeza kwamba
serikali itaharakisha suala hilo ili wenye sifa wapate madaraja mapya.
Aidha, amesisitiza kwamba serikali iko pamoja na watumishi wote na haitowaangusha
na kuwataka watumishi kuendelea kufanya kazi kwa weledi.
"Tuendelee kujituma. Kazi zinazofanyika zinaonekana. Hata utoaji
huduma unaendelea vizuri. Uko umoja wa wafanyakazi unaonekana na watumishi
wanawahudumia wananchi," amesema Waziri Mkuu.
Katika hatua nyingine ameendelea kusisitiza suala la kutowahamisha
watumishi bila kulipwa fedha za uhamisho.
Awali, akisoma hotuba ya Wafanyakazi, Katibu Mkuu wa TUCTA
amemweleza Waziri Mkuu kuwa bado kiwango cha mishahara wanayolipwa
watumishi hakitoshi na kuongeza kuwa bado wafanyakazi wanabeba mzigo wa kodi ya
mapato hususan wale wenye viwango vya juu vya madaraja.
Aidha, amemweleza Waziri Mkuu kuwa viongozi waache kunyanyasa
wafanyakazi na pindi wanapoondolewa kwenye utumishi waondolewe taratibu za
kazi.
Mwisho ameiomba serikali kufanya uchunguzi wa matumizi ya mifuko hiyo.
Wafanyakazi wa Madini wakishiriki maandamano ya kumpongeza Rais wa Jamhuri wa Muungano wa
Tanzania uamuzi wake wa kutangaza
kutumika kwa kikokotoo cha zamani cha mafao ya Wastaafu.
|
Wafanyakazi wa Madini wakishiriki maandamano ya kumpongeza Rais wa Jamhuri wa Muungano wa
Tanzania uamuzi wake wa kutangaza
kutumika kwa kikokotoo cha zamani cha mafao ya Wastaafu.
|
No comments:
Post a Comment