Monday, January 7, 2019

Watumishi Madini waungana na wenzao kumpongeza Rais Magufuli kwa kutumika kikokotoo cha zamani


Watumishi wa Wizara ya Madini wameungana na watumishi wengine nchini kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli  kwa uamuzi wake wa kutangaza  kutumika kwa kikokotoo cha zamani cha mafao ya Wastaafu.

Watumishi hao wameungana katika maandamano ya amani yaliyoanzia katika Ofisi za Bunge na kupokelewa na  Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa katika Bustani  za Nyerere Square, jijini Dodoma.

Akizungumza na watumishi kutoka sekta mbalimbali, Waziri Mkuu Majaliwa amesema Serikali itaendelea kushirikiana na Vyama vya Wafanyakazi katika hatua zote za majadiliano ya suala hilo hadi pale pande zote zitakaporidhika.

Ameongeza kuwa, maombi  yaliyowasilishwa na Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi nchini (TUCTA)  yameanza kufanyiwa kazi na mengine yanaendelea kufanyiwa kazi.

Akizungumzia ombi  la mishahara mipya ya wafanyakazi amesema Tume ya Mishahara na Motisha inaendelea kulifanyia kazi suala hilo na pindi litakapokamilika, taarifa itatolewa. 

Kuhusu madeni ya watumishi amesema serikali inaendelea kulipa madeni hayo ikiwemo malimbikizo mbalimbali ya watumishi.

Kuhusu kupandishwa madaraja, amesema  tayari Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma imeanza kushughulikia suala  hilo ambapo tayari utekelezaji umekwisha anza kwa baadhi ya sekta na kuongeza kwamba serikali itaharakisha suala hilo ili wenye sifa wapate madaraja mapya.

Aidha, amesisitiza kwamba serikali iko pamoja na watumishi wote na haitowaangusha na kuwataka watumishi kuendelea kufanya kazi kwa weledi. 

"Tuendelee kujituma. Kazi zinazofanyika zinaonekana. Hata utoaji huduma unaendelea vizuri. Uko umoja wa wafanyakazi unaonekana na watumishi wanawahudumia wananchi," amesema Waziri Mkuu.

Katika hatua nyingine ameendelea kusisitiza suala la kutowahamisha watumishi bila kulipwa fedha za uhamisho.

Awali, akisoma hotuba ya Wafanyakazi,  Katibu Mkuu wa TUCTA  amemweleza Waziri Mkuu kuwa  bado kiwango cha mishahara wanayolipwa watumishi hakitoshi na kuongeza kuwa bado wafanyakazi wanabeba mzigo wa kodi ya mapato hususan wale wenye viwango vya juu vya madaraja.

Aidha, amemweleza Waziri Mkuu  kuwa viongozi waache kunyanyasa wafanyakazi na pindi wanapoondolewa kwenye utumishi waondolewe taratibu za kazi.

Mwisho ameiomba serikali kufanya uchunguzi wa matumizi ya mifuko hiyo.


Wafanyakazi wa Madini wakishiriki maandamano ya  kumpongeza Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania  uamuzi wake wa kutangaza  kutumika kwa kikokotoo cha zamani cha mafao ya Wastaafu. 

Wafanyakazi wa Madini wakishiriki maandamano ya  kumpongeza Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania  uamuzi wake wa kutangaza  kutumika kwa kikokotoo cha zamani cha mafao ya Wastaafu. 

No comments:

Post a Comment